SHERIA YA MABADILIKO YA KATIBA KUJADILIWA



Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimesema kinajipanga kutumia wanasheria, kujadili na kufanyia kazi baadhi ya vifungu vyenye utata vilivyopo katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Mkurugenzi wa Utetezi, Maboresho  na Sheria wa LHRC, Harold Sungusia alisema hayo jana Dar es Salaam.
Alisema vifungu hivyo  ni pamoja na Kifungu cha 25 (2) cha Mamlaka ya Bunge la Katiba na Kifungu cha 22 cha Sheria hiyo.
Kuhusu utata wa Kifungu cha 25 (2), alisema kifungu hicho kimekuwa na utata kuhusu Mamlaka ya Bunge la Katiba katika kujadili na kufuta baadhi ya vipengele katika rasimu ya Katiba.
“Kifungu hicho kinakuwa na utata kwani hakiko wazi kama Bunge hilo lina mamlaka ya kujadili na kufuta ama kujadili na kupitisha kile kilichofanywa na iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba,” alisema Sungusia.
Kuhusu Kifungu cha 22, alisema kinatoa mamlaka kwa Rais kuitisha Bunge Maalumu la Katiba, lakini hakielezi wazi kama ana mamlaka ya kulifuta linapokwenda kinyume na matarajio.
Alisema inavyoeleweka ni kwamba kama sheria inaweza kumpa kiongozi mamlaka ya kufanya jambo, halafu ikawa kimya kuhusu kufuta jambo hilo. Alisema ni lazima upo utata, unaohitaji kufanyiwa kazi.
 “Katika sheria hiyo hakuna kifungu kinachosema kama Rais hana mamlaka ya kulifuta Bunge hilo…sheria hiyo imekaa kimtegomtego, na kifungu chenye kueleza nani mwenye jukumu hilo kilitakiwa kuwepo humo,” alisema Sungusia.
Alisema katika sheria hiyo, hakuna kifungu kinachomkataza Rais kufanya hivyo  na  Mwanasheria Mkuu wa Serikali alipaswa kuona hilo na kuandaa muswada  wa kupelekwa bungeni kukiweka.
Akizungumzia sheria hiyo na mamlaka ya kufuta Bunge Maalumu la Katiba, juzi Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema alisisitiza kuwa sheria hairuhusu mtu yeyote, akiwemo Rais, kuvunja Bunge Maalumu la Katiba.

No comments: