Bunge Maalumu la
Katiba, limemwalika Mhadhiri mashuhuri wa masuala ya
Katiba, Profesa Issa Shivji, kuwasaidia aina ya Muungano na namna mambo yake
yatakavyoingizwa kwenye Katiba.
Pia Bunge hilo
limepokea mapendekezo ya nyongeza ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, yaliyokuwa
yamehifadhiwa, ili yatumike wakati wa kuunda katiba ya Tanganyika, yajadiliwe
na kamati hizo.
Uamuzi huo
ulifikiwa jana kwenye Kamati ya Uongozi, iliyokaa ambapo
Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta, aliunda Kamati Ndogo ya Kamati ya Uongozi,
kufanyia kazi kwa undani mambo ambayo kamati nyingi zimeshindwa kufikia
muafaka.
Mambo hayo ni
pamoja na Mahakama ya Kadhi, Muundo wa Bunge na kuangalia mambo ya muungano,
uraia pacha na Kamati ya Pamoja ya Fedha ya Muungano.
Akizungumza na
waandishi wa habari juu ya yaliyojiri kwenye Kamati hiyo ya
Uongozi wakati wa kupitia tathmini ya mwenendo wa Bunge, Sitta alisema Bunge
limeona limwalike Profesa Shivji kutokana na kuwa na maandiko mengi ya muundo
wa Muungano.
Kwa matarajio ya
Sitta, Profesa Shivji atasaidia aina ya Muungano unaofaa na
mambo yake yatazingatiwa wakati wa kutengeneza muundo huo.
Kamati hiyo
ndogo aliyounda ina wajumbe kumi, watano kutoka Tanzania
Bara na watano Zanzibar na itakuwa chini ya Makamu Mwenyekiti wa Bunge, Samia
Suluhu Hassan na kwa kuanza alisema: “Nimeagiza wataalamu wa ngazi za juu waje
kukutana na kamati ndogo kwa kina na kwa kamati ya fedha, watakuja makatibu
wakuu na magavana kutoka Serikali ya Jamhuri na ya Mapinduzi na magavana hao,
waje kabla ya Jumamosi (kesho kutwa)”.
Kwa upande wa
uraia pacha, alisema watakuja wataalamu kutoka Idara ya Uhamiaji akiwemo
mhadhiri wa masuala ya uraia pacha ambapo wote, watatoa elimu zaidi kuwasaidia
wajumbe kufikia muafaka wa masuala hayo.
Mwenyekiti huyo
wa Bunge Maalumu la Katiba alisema wamekubaliana kwenye Kamati ya Uongozi,
kupeleka kwenye kamati 12 za Bunge, andiko la Tume ya Jaji Joseph Warioba, ili
yazingatiwe wakati wa kuundwa kwa serikali ya Tanganyika.
Mambo hayo ni
ardhi, mazingira na rasilimali za Taifa ambapo Sitta amesema wameyachukua bila
kubagua aina ya serikali.
Alitaja mambo
mengine waliyoyachukua na kuwasilishwa kwa Kamati ili yajadiliwe na kuongezwa
kwenye rasimu hiyo, ni yaliyoletwa na Waziri wa Katiba na Sheria ya mapendekezo
kutoka Jumuiya ya Serikali za Mitaa (ALAT) ya kutambuliwa Serikali za Mitaa
kwenye Katiba.
Vilevile
wameyaingiza mapendekezo ya kuwepo maeneo mahususi kama kuwa na sehemu ya
kutosha kuelezea jukumu la serikali, katika kujenga uchumi imara hivyo
wameona kuanzishwe sura mpya ya Lengo la
Maendeleo ya Kiuchumi.
Pia yamo
mapendekezo ya haki za wachimbaji wadogo, wakulima na wavuvi. Pia haki za
kuwalinda watumiaji bidhaa na haki za makaburi ambapo marehemu watapewa
heshima, iliyowasilishwa na Yasmin Aloo.
Sitta alisema
kamati zote zinakwenda vizuri, ila tatizo ni baadhi ya wabunge wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano mahudhurio yao si mazuri kwa kuwa wanakwenda sana majimboni
lakini wawakilishi kutoka Zanzibar mahudhurio yao ni mazuri.
No comments:
Post a Comment