OFISA WANYAMAPORI MBARONI KWA UWINDAJI HARAMU

Ofisa Uhifadhi wa wanyamapori katika Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji, Rashid Ndimbe amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu,  akikabiliwa na mashitaka ya kuwinda bila kibali na kukutwa na nyama ya nyati.
Ndimbe, ambaye alirudishwa rumande baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kuwasilisha hati ya kuzuia dhamana, alikana mashitaka yanayomkabili.
Alifikishwa mahakamani hapo jana na kusomewa mashitaka matatu na Wakili Mwandamizi wa Serikali, Bernald Kongola mbele ya Hakimu Mkazi, Devotha Kisoka.
Wakili Kongola alidai kuwa katika tarehe tofauti kati ya Januari na Septemba mwaka jana, katika Wilaya ya Kilwa mkoani Lindi, Ndimbe alikamatwa akisafirisha nyara za serikali ambazo ni nyama ya nyati yenye thamani ya Sh 200,000, bila kuwa na kibali kutoka kwa Mkurugenzi wa wanyamapori.
Alidai kuwa Septemba 21 mwaka jana katika maeneo hayo, Ndimbe alikutwa akiwa na nyara hizo. Pia anadaiwa katika eneo la hifadhi la Kilwa alikamatwa akiwinda nyati bila ya kuwa na kibali.
Mshitakiwa alikana kutenda makosa hayo. Upande wa jamhuri ulidai upelelezi wa kesi hiyo, haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa. Hakimu Kisoka aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 14 mwaka huu, itakapotajwa tena na mshitakiwa alirudishwa rumande baada ya DPP kuwasilisha hati ya kuzuia dhamana yake.

No comments: