NBC YATOA MKOPO WA SHILINGI BILIONI 100 KWA STAR OILS

Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imetia saini makubaliano ya mkopo wa Sh bilioni 100 na kampuni ya kusambaza mafuta ya jijini Dar es Salaam ya Star Oils katika mpango mkakati wa kuendeleza sekta ya mafuta nchini.
Akizungumza katika hafla ya utiaji saini mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Mizinga Melu alisema  hiyo inahitimisha safari ya majadiliano na kampuni mama ya Star Oils, Mohammed Entrepries Tanzania Limited (METL) ya mkopo wa Sh bilioni 100.
"Star Oils ni kampuni dada ya METL ni moja ya kampuni zinazokwenda kasi katika biashara ya ushindani katika Afrika Mashariki na Kusini mwa Jangwa la Sahara na rekodi yao ya mauzo na biashara ni ya kuridhisha," alisema.
Alisema METL ni moja ya kampuni zenye rekodi nzuri katika biashara ya viwanda, nguo, vinywaji, bima na mafuta na wanastahili kuwezeshwa kwa kupata mikopo mikubwa na ya muda mrefu kupitia taasisi za kifedha nchini na nje ya nchi.
"Sisi Benki ya NBC tunayo furaha kubwa kwa kupata nafasi ya kufanya biashara na moja ya kampuni zinazokuja kwa kasi katika bara la Afrika na vile vile NBC ni benki ambayo ipo tayari kusaidia wateja wake,” aliongeza.
Melu alisisitiza baada ya NBC kujiridhisha na shughuli za kibiashara na mzunguko wa fedha wa METL, wameamua kutoa mkopo huo wapanue biashara yao katika masoko ya kimataifa.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa METL, Mohammed Dewji  alisema hatua ambayo kampuni hiyo imefikia ni kubwa kwa kuonesha dhamira ya kuwekeza na kufanya biashara ya mafuta Afrika Mashariki na kusini mwa Jangwa la Sahara.
"Sisi tuna mipango ya kuanza kusambaza mafuta na bidhaa za petroli katika nchini za Kusini mwa Afrika kama sehemu ya jitihada za kampuni za kupanua biashara zake katika soko la Afrika," alisema.
Star Oils kwa sasa inatekeleza awamu ya pili ya mradi mkubwa wa kuhifadhi mafuta ya petroli na baadaye kujenga usambazaji wa mafuta nchi nzima kwa njia ya mlolongo wa vituo vya karibu 200 ya petroli nchini.

No comments: