MAMLAKA YA ELIMU KUZIPATIA SHULE ZA DAR MADAWATI 2,000



Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), inatarajia kukabidhi madawati 2,000 kwa shule za msingi 10 zilizopo jijini Dar es Salaam katika kukabiliana na tatizo la upungufu wa madawati nchini.
Hayo yamesemwa na Meneja Habari, Elimu na Mawasiliano wa mamlaka hiyo, Sylvia Lupembe wakati wa mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana.
“Wanafunzi zaidi ya 6,000 watanufaika na madawati hayo ambayo yatagharimu zaidi ya Sh milioni 150,” alisema Lupembe.
Akifafanua, Lupembe amesema shule zitakazonufaika ni Chamazi, Mbande, Boko NHC, King’ong’o, Hekima, Bwawani, Bunju, Goba, Kombo na Kingugi.
Pia Lupembe alibainisha kuwa tathmini ya mwaka 2013 Tanzania ina upungufu wa madawati 1,147,471 hivyo ni jukumu la kila mdau kuunga mkono juhudi hizo ili kuondoa tatizo hilo kote nchini.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Uhusiano wa Benki ya KCB, Christina Manyenye amesema wamekuwa wakishiriki katika kuchangia madawati ambapo kwa mwaka jana walichangia zaidi ya madawati 700.
TEA kwa kushirikiana na Kampuni ya Mafuta ya TOTAL na wadau wengine kama Kenya Commercial Bank  (KCB), na Social Action Fund  wamekuwa katika ushirikiano tangu mwaka 2013 katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya elimu nchini.

No comments: