KIKWETE, MARAIS 46 AFRIKA WAKUTANA NA OBAMA

Rais Jakaya Kikwete yuko Marekani kwa ziara ya siku tisa nchini humo ambako miongoni mwa mambo mengine, atahudhuria Mkutano wa Kwanza wa Kihistoria wa Viongozi wa Bara la Afrika na Marekani ulioitishwa na Rais Barack Obama. 
Mkutano huo wa siku mbili unafanyika kuanzia leo ukianza na mkutano wa biashara kati ya Afrika na Marekani.  Unafuatiwa na mkutano wenyewe wa Marekani na Afrika utakaofanyika kwenye Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani.  
Kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dulles mjini Washington, Rais Kikwete alipokewa na Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Liberata Mulamula na maofisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani. 
Kwenye ziara hiyo, Rais Kikwete ameongozana na mkewe, Mama Salma Kikwete ambaye naye atakuwa na programu tofauti wakati wa ziara hiyo, kama watakavyokuwa wake wa viongozi wengine wa Afrika wanaohudhuria mkutano huo. 
Mkutano huo wa kwanza wa aina yake kati ya kiongozi wa Marekani na viongozi wa Afrika umepangwa kuhudhuriwa na viongozi kutoka nchi 47 ambazo zote zimealikwa na Rais Obama kushiriki mkutano huo. 
Mbali na shughuli zake nyingi za mjini Washington, Rais Kikwete atasafiri kwenda Dallas, Jimbo la Texas, ambako atakutana na Rais wa 43 wa Marekani, George W. Bush, kabla ya kuendelea na safari katika mji mwingine mkubwa wa jimbo hilo wa Houston. 
Mjini Houston, Rais Kikwete atafanya mkutano wa kimkakati wa kibiashara na wafanyabiashara maarufu mbalimbali hasa wa sekta ya gesi na mafuta kabla ya kumaliza ziara yake. 
Miongoni mwa shughuli zake, Mama Salma Kikwete atahudhuria mkutano wa wake wa marais wa Afrika na mke wa Rais wa Marekani, Michelle Obama utakaofanyika kwenye Kituo cha John F Kennedy.
Mkutano huo utahudhuriwa pia na mke wa Rais George W. Bush, Mama Laura Bush.

No comments: