HALMASHAURI 41 KUSHIRIKI NANENANE MWANZA

Halmashauri 41 za Kanda ya Ziwa na wadau 15 wa maonesho nya kilimo, wamethibitisha ushiriki wao kwenye Maonesho ya Wakulima (Nanenane) Kanda ya Ziwa, yaliyoanza jana.
Maonesho hayo yanafanyika katika viwanja vya Nyamhong’olo, nje kidogo ya jiji la Mwanza. Yatafunguliwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utumishi, Celina Kombani.
Kwa mujibu wa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya Nanenane Kanda ya Ziwa, Pascal Mabiti, uzinduzi rasmi utafanyika Agosti 3, mwaka huu.
Aliwataja wadau waliothibitisha kushiriki katika maonesho hayo kuwa ni Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Victoria Polybags & Moulders, Nyanza Bottling Ltd, SBC Tanzania, Yara Mila Co. Ltd na Star Times. Wengine ni Sahara Media Group, Taasisi ya Utafiti-Ukiriguru, Umwagiliaji Kanda, Tigo, Meru Agro Consultant, Bodi ya Pamba Tanzania, SIDO Mwanza, Mabatini Moulders na TCRA.
Alisema maonesho hayo ya wakulima, yatatoa fursa washiriki kupata elimu kupitia mada mbalimbali zitakazowasilishwa, zikiwemo za ugonjwa mpya wa mahindi, magonjwa ya mazao ya mihogo na migomba na udhibiti wake.
Pia, mada za matumizi sahihi ya mbolea na stakabadhi ya mazao ghalani, zitatolewa katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Mwanza.
Alisema asilimia 80 ya maandalizi, yamekamilika, hivyo kutoa fursa kwa mgeni rasmi kufungua maonesho hayo, yatakayokuwa na kaulimbiu inayosema “Matokeo Makubwa Sasa - Kilimo na Biashara”’.
Katika maadhimisho kama hayo mwaka jana, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Evarist Ndikilo aliwatahadharisha wakulima na wafugaji juu ya fedha bandia, zinazotumiwa na watu wasio waaminifu kununua bidhaa kwenye maonesho hayo.

No comments: