BABA MZAZI ASAKWA KWA KUMPA UJAUZITO BINTI YAKE

Mkazi wa Kijiji cha Bwekela wilayani Igunga mkoani Tabora, Kashinje Shima, anatafutwa na Uongozi wa kijiji hicho, kwa kumpa ujauzito mwanawe wa kumzaa mwenye umri wa miaka 17. 
Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Bwekela, ambaye pia ni Kaimu Ofisa Mtendaji wa Kata ya Igoweko, Robert Ruhende, alilaani kitendo kilichofanywa na mzazi wa mtoto huyo na kusisitiza kuwa sheria lazima ichukue mkondo wake.
Akisimulia kisa hicho, mke wa mkazi huyo ambaye pia ndiye mama mzazi wa mtoto huyo, Geni Njiro, alidai alibaini hali hiyo Julai 23 mwaka huu, baada ya mwanawe wa kiume kumfumania baba yake na dada yake.
Kwa sasa kwa mujibu wa Geni, mwanawe huyo ambaye inadaiwa amekiri kushiriki kitendo hicho, ana ujauzito wa miezi saba.
Geni alidai kabla ya kugundua kitendo hicho cha kinyama kilichokuwa kikifanywa na mumewe, alihisi kuwa baba wa mtoto huyo alikuwa akitumia mwanya wa yeye mama kutokuwepo nyumbani, kufanya vitu visivyo vya kawaida. 
Alidai kuwa alipata hofu kuhusu mwenendo wa mumewe na mtoto wake siku moja walipokuwa shambani wakiendelea na shughuli za kuvuna mazao,  ambapo mumewe aliaga kurudi nyumbani.
Kutokana na hofu hiyo, Geni alidai aliamua kumtuma mtoto wake mkubwa wa kiume, ambaye hakutaka kumtaja jina, akafuatilie nyumbani kupata uhakika wa kile alichokuwa akihofia.
Mama huyo alidai baada ya mtoto wake huyo  kufika nyumbani, ndipo alikuta baba yake wakifanya ngono na mdogo wake na kurudi shambani na kumpa taarifa mama yake.
Baada ya taarifa hiyo, mama huyo alidai kuwa aliamua kuita ndugu wa pande zote mbili, kwa ajili ya kuzungumzia unyama huo, ambapo baba huyo alipohojiwa katika kikao hicho cha  familia, alikana kuhusika na tuhuma hizo.
Hata hivyo, mama huyo alidai babu wa mtoto huyo, alishauri waende kupima hospitali kupata ukweli, ndipo baba huyo alipokubali kuwa anatembea na mtoto wake.
Baada ya kukubali, inadaiwa baba huyo alitakiwa kulipa adhabu ya faini ya ng’ombe wawili, ambao aliwalipa na suala hilo kuwa limekwisha.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mwina, Bundala Makelema, alikiri kuwepo kwa suala hilo. Alidai kuwa wakati mtuhumiwa huyo akilipa adhabu ya kimila ya ng’ombe wawili, yeye alishiriki kwa nafasi yake ya Kiongozi wa Kitongoji. 
Hata hivyo, inadaiwa familia anayotoka mama huyo, ilipinga uamuzi huo wa kifamilia na kumruhusu ndugu yao, kuchukua hatua zaidi, ikiwemo kutoa taarifa katika vyombo vya habari.
Taarifa hiyo ilipofika kwa Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Bwekela, ambaye pia ni Kaimu Ofisa Mtendaji wa Kata ya Igoweko, Ruhende ambaye aliahidi kwenda Polisi ili hatua zaidi zichukuliwe, mama huyo alidai ndipo mumewe alipoamua kutoroka nyumbani na kwenda kusikojulikana.

No comments: