ATUPA MTOTO WA SIKU MOJA KUNUSURU NDOA YAKE

Mtoto wa kike mwenye umri wa siku moja amenusurika kufa baada ya kuokolewa na wasamaria kutoka katika shimo alimotupwa na mama yake mzazi.
Imeelezwa kuwa mwanamke huyo alifanya hivyo ili kulinda ndoa yake changa, kwa kuwa mumewe hakuwa mhusika wa ujauzito huo.
Taarifa za tukio hilo zimethibitishwa na Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji cha Rwabigaga, Fron Nestory.
Alisema  tukio hilo ni la usiku wa kuamkia Jumapili iliyopita katika kijiji cha Rwabigaga kata ya Kamuli wilayani Kyerwa.
Alidai siku hiyo ya tukio, mwanamke huyo, Jane Leonard alijifungua salama mtoto wa kike, lakini baadaye akamwambia mama mkwe wake, kuwa mtoto amepotea katika mazingira ya kutatanisha.
Nestory alisema kutokana na taarifa hizo, juhudi za kumsaka mtoto zilianza na ilipofika asubuhi wamlikuta mtoto huyo kwenye shimo, akiwa amefunikwa kwa maganda ya maharage na tayari siafu na wadudu wengine, walikuwa wameanza kumshambulia.
Alisema jitihada za kumuokoa mtoto huyo zilifanyika, ambapo baada ya kumuosha alipelekwa katika Kituo cha Afya Kamuli na kupatiwa huduma. Kwa sasa anaendelea vizuri na tayari amekabidhiwa kwa mama yake mzazi.
Kwa upande wake, mama mzazi wa mtoto huyo alisema alifanya hivyo, kutokana na hofu ya kuvunjika kwa ndoa yake changa, kwani imepita miezi miwili tu tangu aolewe.
Ingawa hakutaka kuingia kwa undani, imeelezwa hofu yake imetokana na ukweli kwamba, ameingia katika ndoa mpya akiwa mjamzito, ilhali mumewe wa sasa si mhusika.
Hata hivyo, Nestory aliwataka wananchi kuwa na hofu ya Mungu na kuacha  vitendo vya unyanyasaji na ukatili kwa watoto, kwani mtoto ni tegemeo la taifa kwa ujamla.
Kamanda wa Polisi mkoani Kagera, Henry Mwaibambe alisema tukio hilo hajalipata;na alisema ameagiza polisi wilayani Kyerwa, kufuatilia zaidi na kumpa taarifa juu hilo.

No comments: