ARUMERU WATAKA SERIKALI IWALIPE SHILINGI BILIONI 3.7

Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Arusha wilayani Arumeru, limemwagiza Mbunge wa Arumeru Magharibi, kufuatilia malipo yao ya Sh bilioni 3.7 kutoka serikali kuu baada ya serikali kuchukua viwanja katika halmashauri hiyo.
Limemtaka Mbunge huyo, Goodluck ole Medeye kuhakikisha anafuatilia fedha hizo kwa ukaribu zaidi na kuwa na majibu ya uhakika katika kikao kijacho cha baraza la madiwani.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Saimoni Saning’o  alisema halmashauri ina changamoto nyingi zinazohitaji fedha.
Alisema baraza liliamua kuuza viwanja hivyo kwa watu binafsi ili waweze kutumia fedha hizo katika miradi mbalimbali ya maendeleo.
Alisema kutokana na ucheleweshwaji huo, unaofanywa na serikali kuu wa malipo hayo ya Sh  bilioni 3.7,  inakuwa vigumu halmashauri kujiendesha kikamilifu.
"Halmashauri ina matatizo mengi kama vile barabara mbovu, maji, zahanati hazina dawa na baadhi ya shule madawati ni shida sasa nakuagiza Mbunge fuatilia hili, kwani wewe ndio uko karibu na wahusika  na kikao kijacho uje na hundi,’’ alisema.
Mbunge wa Jimbo hilo alikubali kubeba jukumu hilo. Alisema hata yeye suala hilo halimpi usingizi kwa kuwa fedha hizo zikipatikana, zitatatua changamoto nyingi za maendeleo zilizoko katika jimbo lake, ikiwa ni pamoja na ahadi alizoahidi katika kampeni ya mwaka 2010.
"Ninakwenda katika Bunge la Katiba na wahusika wote watakuwa huko na nitakuja na majibu mazuri, ama nitakuja na hundi ya kiasi kilichobaki," alisema.
Hata hivyo, aliwataka madiwani kuamini serikali yao juu ya deni hilo. Alisema Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia aliahidi  kulipa deni hilo haraka, lakini majukumu yamekuwa yakiingiliana. Inadaiwa kati ya Sh bilioni 5.7, serikali imeshalipa Sh bilioni mbili kwa halmashauri hiyo.

No comments: