AJIRA 200 ZA KONSTEBO, KOPLO ZAPIGWA 'STOP' UHAMIAJI

Ajira za washindi 200, walioitwa kufanya usaili wa nafasi za ajira za Konstebo na Koplo wa Uhamiaji, zimesitishwa kupisha uchunguzi wa utaratibu wa uteuzi wa washindi hao.
Hatua hiyo imekuja katika siku chache, tangu kulipoibuka utata, uliotokana na kuitwa kwa watu zaidi ya 10,000 wenye shahada za kwanza, kufanya usaili wa nafasi 70 tu za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji, zilizokuwa wazi katika Idara hiyo.
Taarifa ya Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Isaac Nantanga, kwa vyombo vya habari jana, ilieleza kuwa hatua hiyo ya kusitisha ajira hizo, imechukuliwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mbarak Abdulwakil.
Kwa mujibu wa Nantanga, hatua hiyo imechukuliwa baada ya kuibuka tuhuma kuwa kati ya washindi hao 200, ambao walishatangazwa na kutakiwa kuanza kazi Jumatano ya wiki ijayo, sehemu kubwa ni ndugu na jamaa za wafanyakazi wa Uhamiaji.
“Kutokana na kusitishwa kwa ajira hizi, waombaji wote walioitwa na kutakiwa kuripoti Makao Makuu ya Idara ya Uhamiaji tarehe 6, Agosti 2014, sasa wanatakiwa kusubiri hadi hapo watakapotangaziwa tena baada ya uchunguzi huu kukamilika na uamuzi kufanyika,” alieleza Nantanga katika taarifa yake.
Tayari Katibu Mkuu, Abdulwakil, ameshaunda Kamati Ndogo ya Uchunguzi wa suala hilo. Taarifa zilizofikia gazeti hili jana, zilieleza kuwa kuna uwezekano muda wa uchunguzi huo na hadidu za rejea, vitajulikana leo.
Sifa za wasailiwa 100 katika nafasi ya Koplo wa Uhamiaji, zilikuwa awe amehitimu Kidato cha Sita na kufaulu, bila kutaja kiwango cha ufaulu ; na ya pili ni umri usiozidi miaka 30.
Kwa nafasi 100 za Konstebo wa Uhamiaji, sifa zilikuwa awe amehitimu Kidato cha Nne na kufaulu, bila kutaja kiwango cha ufaulu, na awe na umri usiozidi miaka 25.
Majukumu na kazi zao, zilikuwa kufungua, kupanga na kutunza majalada ya huduma mbalimbali za Uhamiaji, kuandika hati mbalimbali za Uhamiaji, kufanya doria sehemu za mipakani, bandarini, vituo vya mabasi, treni na sehemu zenye vipenyo vya kuingia na kutoka nchini, vikiwemo vya majini.
Nyingine ni kusindikiza watuhumiwa wa kesi za Uhamiaji mahakamani pamoja na wageni wanaofukuzwa nchini, kufanya ukaguzi kwenye mahoteli, nyumba za kulala wageni na sehemu za biashara, kuchapa au kuandika kwa kompyuta barua au nyaraka mbalimbali zinazohusu kazi za kila siku za Uhamiaji, kufanya matengenezo/ukarabati wa mitambo na vitendea kazi vya Uhamiaji na kuandaa na kutunza takwimu za huduma mbalimbali za uhamiaji.
Tuhuma hizo zilizosambaa katika mitandao ya jamii, zilidai kuwa matokeo ya usaili wa nafasi za kazi Uhamiaji, yaliyotolewa katika magazeti, yameonesha kuwa katika Idara hiyo Watanzania wengine, mbali ya watoto au ndugu wa wafanyakazi wa Idara hiyo, hawawezi kupata ajira ndani ya Idara hiyo ya Serikali kirahisi. 
“Majina ya wengi walioitwa kazini ni watoto au ndugu wa wafanyakazi wa idara hiyo,” ilieleza taarifa hiyo, iliyosambazwa katika mitandao na kutaja majina ya wanaodaiwa kuwa ni washindi wa usaili huo na uhusiano wao na maofisa wa Uhamiaji.
“Hii ni sampuli tu, ila zaidi ya asilimia tisini ni watoto na ndugu wa maofisa Uhamiaji. Nadhani ingekuwa vyema wasingekuwa wanatangaza nafasi hizi, bali wawe wanagawiana ndani kwa ndani. Alamsiki,” ilieleza taarifa hiyo.
Hivi karibuni Idara ya Uhamiaji ilipotangaza majina ya wasailiwa zaidi ya 10,000, waliotakiwa kushindania nafasi 70 za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji. Hatua hiyo ilisababisha utata, kutokana na uchache wa nafasi, ikilinganishwa na wasailiwa walioitwa.
Utata huo ulisababisha kuibuka kwa hisia za usaili huo, kugubikwa na rushwa, kiasi kwamba Nantanga alilazimika kutoa taarifa, kukanusha kuwepo kwa tuhuma hizo.
“Tuhuma za rushwa zinazoambatanishwa na kazi hii, ni hisia tu za wahusika, kwani kwanza hazina ushahidi, na pia usaili ulifanywa kufuatana na kanuni na sheria zinazosimamia ajira za watumishi wa umma,” ilieleza taarifa hiyo ya Nantanga, kuhusu usaili wa watu zaidi ya 10,000.
Nantanga alifafanua kuwa nafasi za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji, zilitangazwa katika magazeti na Tovuti ya Wizara na Idara ya Uhamiaji, kufuatana na taratibu za Serikali, zinazosimamia ujazaji wa nafasi za kazi katika utumishi wa umma, kwa lengo la kuiweka wazi kwa umma wa Watanzania na matokeo yake wahitimu zaidi ya 20,000, walitumia haki yao ya msingi kuomba nafasi hizo.   
Kufuatana na wingi wa waombaji, Wizara ilifanya zoezi la mchujo wa awali, ambao hatimaye ulibakiza kiasi cha maombi 10,000 yenye waombaji wenye sifa zinazohitajika.
Aidha, kutokana na wingi huo, na haki ya kila mwombaji ya kupatiwa nafasi ya kushindania nafasi hizo, ilibidi Wizara ifanye utaratibu wa kutafuta eneo lenye nafasi ya kutosha ya kuweza kuwapokea wasailiwa, ambalo hatimaye ilionekana iwe Uwanja mpya wa Taifa.
Tayari katika usaili huo wa wasailiwa zaidi ya 10,000, walishinda wasailiwa 1,281  ambao walikuwa wakiwania nafasi hizo 70.
Nantanga alitangaza kuwa washindi hao, walitarajiwa kuingia katika kinyang’anyiro cha mwisho cha usaili uliofanyika Juni 30 hadi Julai 3 mwaka huu katika Bwalo la Maofisa wa Magereza, Ukonga.
Mwandishi alielezwa jana kuwa usaili wa watahiniwa wa nafasi hizo 70 za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji pamoja na Uhamiaji kuita katika usaili watu zaidi ya 10,000, haukuleta matatizo na washindi wameshapatikana. 
Wasailiwa walitakiwa kuwa na Shahada au Stashahada ya Juu kutoka vyuo vinavyotambuliwa na Serikali katika fani za Sheria, Uchumi, Biashara, Utawala, Uandishi wa Habari, Ualimu, Usafirishaji, Rasilimali Watu, Sayansi ya Kompyuta, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Takwimu, Uchapaji, Uhandisi Majengo na Uhandisi Mitambo.

1 comment:

Anonymous said...

Hi, ɑll the time i use to check welog posts Һere in the еarly
hours іn tthe dawn, fߋr the reason that i
enjoy to find out moгe and moгe.

Аlso visit my website - design your own