Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Silaa na
Diwani wa Kata ya Kipawa, Bonnah Kaluwa jana waliwaongoza mamia ya wakazi wa
Jiji la Dar es Salaam katika kampeni ya kutoa damu ili kuchangia Benki ya Damu
inayokabiliwa na upungufu wa damu.
Tukio hilo kubwa, lilifanyika katika Viwanja
vya Sitaki Shari Majumbasita, ambapo viongozi hao walisema wamechukua hatua
hiyo kama ishara ya kuonesha kuguswa na vifo, vinavyotokana na ukosefu wa damu
vikiwemo vya uzazi.
Akizungumza wakati akitolewa damu, Silaa
alisema takwimu zinaonesha kuwa Manispaa ya Ilala, inakusanya asilimia 33 tu ya
mahitaji ya damu kila mwaka, kiasi ambacho hakitoshelezi mahitaji ya wagonjwa
wanaohitaji kuongezewa damu.
“Upungufu huu wa damu unasababisha wakazi wa
Manispaa ya Ilala na wakazi wengine wa Jiji la Dar es Salaam kushindwa kupata
damu inayotosheleza mahitaji hatua ambayo inasababisha vifo kuongezeka.
“Ni lazima sasa kila kiongozi kwa nafasi yake
akawahamasisha wakazi wa Dar es Salaam na Watanzania kwa ujumla kujitokeza
kutoa damu ili kutunisha benki yetu ya damu iweze kukidhi mahitaji
yanayohitajika.
Ni jambo la kupongeza kuona Diwani wa Kipawa
(Bonna) ameweza kuandaa hafla kama hii ya leo ambapo idadi kubwa sana ya wakazi
wa Dar es Salaam wamefika hapa ili kutoa damu,” alisema Silaa.
Kwa upande wake, Kaluwa alisema; “ Mimi kama mama, kama
kiongozi na kama mzalendo nimeona umuhimu wa kuandaa kampeni hii ili kuwezesha
wakazi wa Dar es Salaam kutoka maeneo yote wajitokeze kutoa damu.
“Ni jambo la kutia faraja kuona muitikio
umekuwa mkubwa kiasi hiki na ni imani yangu kwamba kiwango cha damu
kitakachokusanywa leo kitasaidia sana kuokoa maisha ya Watanzania wenzetu ambao
leo wapo mahospitalini wakiteseka kutokana na kukosa damu,” alisema Diwani
huyo.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Ilala, Dk Willy
Sangu alisema Serikali itaendelea kuwaunga mkono viongozi wanaowahamasisha
Watanzania kujitolea damu kwa vile hatua hiyo itasaidia katika kupunguza vifo
vya wananchi vinavyotokana na kukosa damu.
Kampeni
hiyo ilizinduliwa rasmi jijini Dar es Salaam Juni 12, mwaka huu na Diwani huyo
na iliweza kudumu kwa muda wa siku 10, kabla ya jana kufikia tamati kwa
mafanikio makubwa, kutokana na idadi kubwa ya watu kujitokeza kuchangia damu.
No comments:
Post a Comment