TMAA YAOKOA BILIONI 1.6/- VITA YA UTOROSHAJI MADINI



Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) umefanikiwa kudhibiti utoroshaji wa madini yenye thamani takribani Sh bilioni 15.72 katika viwanja vitatu vya ndege hapa nchini tangu mwezi Julai 2012 hadi Machi 2014 na imeahidi kuongeza kasi ya udhibiti.
Mafanikio hayo ni baada ya Wakala ulipoanza kukagua wasafiri na mizigo katika viwanja vya ndege katika kipindi hicho ambapo  jumla  ya matukio 43 ya utoroshaji wa madini yenye thamani hiyo yaliripotiwa  kwenye viwanja hivyo.
Hayo yalisemwa na Mwezeshaji  wa Wakala, Julius Moshi wakati alipowasilisha  mada  ya shughuli za Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania kwa washiriki wa semina elekezi kuhusu ukaguzi na udhibiti wa uzalishaji na mauzo ya madini ya ujenzi na viwandani  yaliyofanyika  mjini Morogoro.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera alikuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa semina hiyo elekezi ambayo iliwashirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wachimbaji, wawakilishi na wasafirishaji wa madini wanaotumia malori, viongozi wa Serikali ya Mkoa na wilaya, madiwani, wenyeviti na watendaji wa vijiji vilivyopo kwenye maeneo yenye shughuli za uchimbaji wa madini.
Kwa mujibu wa mwezeshaji huyo, kupitia kaguzi mbalimbali, Serikali imepata mrabaha na takwimu sahihi za madini yanayozalishwa na migodi mikubwa hapa nchini.
Hata hivyo alisema, Serikali imeendelea kupata mafanikio mbalimbali ambapo katika kipindi cha kuanzia mwaka 1998 hadi 2013, jumla ya Dola za Marekani milioni 437 zilikusanywa  kama mrabaha kwa kipindi hicho.
Mafanikio mengine yaliyopatikana kwa kipindi cha Juni 2011 hadi machi 2014, Wakala umewezesha Serikali kukusanya mrabaha wa jumla ya Sh bilioni 3.6 kutokana na ukaguzi wa madini ya ujenzi na viwandani.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera akifungua  semina  hiyo elekezi alisema, sekta ya madini kukabiliwa na changamoto nyingi hususani mchango mdogo katika taifa usioendana na kasi ya ukuaji wake.
Awali, Kaimu Mtendaji Mkuu TMAA, Mhandisi  Dominic Rwekaza alisema Wakala utaendelea kuweka vipaumbele vya ukaguzi wa shughuli za usimamizi na utunzaji wa mazingira, ukaguzi na uhakiki wa gharama za uwekezaji na uendeshaji wa migodi.

No comments: