SUA YAKWANZA DUNIANI KUGUNDUA CHANJO YA KUKU



Wafugaji wa kuku nchini wataanza kupata neema ya kupata dawa ya mifugo yao kwa bei rahisi, baada ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kugundua chanjo ya kwanza ya kuku  duniani dhidi ya ugonjwa wa ndui.
Chanjo hiyo ambayo imegunduliwa na mtafiti, Profesa Philemon Wambura wa SUA, itazalishwa na kusambazwa na Kampuni ya MCI Sante Animale ya Morocco katika nchi za Afrika ikiwemo Tanzania. Inatarajiwa kuanza kusambazwa hivi karibuni ikiuzwa kwa bei rahisi. 
Jana SUA ilitiliana saini makubaliano na kampuni hiyo ya kimaitaifa inayotengeneza dawa na chanjo mbalimbali za mifugo kutumia matokeo ya utafiti  wa chanjo kuku dhidi ya ugonjwa wa ndui.
Makubaliano hayo yalifanyika katika ofisi za makao makuu ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (Costech); iliyofadhili utafiti huo ambao umefanywa kwa miaka 10.
Mkurugenzi Mkuu wa Costech Dk Hassan Mshindo alisema kwa mara ya kwanza kazi za watafiti wa  nchini zimeanza kuonekana kwa kampuni za nje badala ya kukaa kwenye makabati.
Alisema utafiti huo wa Profesa Warioba utawasaidia wafugaji wa hapa nchini kuweza kuwakinga kuku wao dhidi ya magonjwa hatarishi ukiwemo ugonjwa wa ndui.
Mwakilishi  wa Kampuni ya MCI Dk Baptiste Dungu, alisema kampuni yake inatengeneza dawa kwa viwango vya kimataifa na akaeleza kufurahishwa na utafiti wa Profesa Wambura kuwa utakuwa na manufaa makubwa kwa wakulima wa Afrika na Tanzania.
Kwa upande wake Profesa Wambura, alisema ni ngumu watafiti wa hapa nchini kupata fedha za kufanyia tafiti kutoka nje ya nchi hivyo akaeleza kitendo cha Costech kutoa fedha kwa watafiti wa hapa nchini kutasaidia kazi za watafiti ziweze kuonekana.

No comments: