PROFESA MWANDOSYA AONYA WASOMI KUTEGEMEA VYETI



Wasomi wengi nchini wameshindwa kujiajiri kutokana na kutojua kuwa  elimu waliyonayo imewafungua akili ili waweze kufanya mambo yao wakiwa na uelewa mzuri hali inayowafanya kutegemea vyeti walivyonavyo.
 Kauli hiyo ilitolewa hivi karibuni na Waziri Ofisi ya Rais asiyekuwa na Wizara Maalumu Profesa  Mark Mwandosya alipokuwa kwenye mahafali ya wanafunzi
 ambao ni wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa vyuo vikuu vilivyopo mkoani Dodoma.
 Mwandosya alisema wengi wamejikuta wamekwama kujiajiri kutokana na  kusubiri ajira bila kujua kuwa elimu waliyopata imelenga kuwasaidia kufanya mambo ya kimaisha kutokana na uelewa walioupata vyuoni na  vinginevyo.
 Alisema hivi sasa ushindani katika soko la ajira ni mkubwa kutokana na  wasomi kuwa wengi hivyo ni afadhali wakaweka  malengo ya kujiajiri pindi wanapomaliza masomo yao.
 ‘’Vijana wangu …  hakikisheni mnajiwekea malengo ya kujiajiri pindi muondokapo vyuoni maana  kukosa malengo kutawafanya kutojituma na kujikuta kila siku mkiuza vyeti ambavyo kila mtu anavyo  badala ya ubora wa elimu  mlioupata vyuoni’’, alisema.
 Awali chama cha CCM kilipokea jumla ya wanachama wapya 230 na kuwakabidhi kadi wanachuo wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) na wengine sita waliokabidhi kadi wakitokea Chadema akiwemo kiongozi  wao Belina Maingu maarufu kwa jina la Balozi.
 Jumla ya wanafunzi 1,500 wa vyuo 10 vilivyopo mkoani hapa ambao ni wanachama wa Chama Cha Mapinduzi walikutana kwenye mahafali ya kwanza yaliyowakutanisha kwa pamoja mwaka huu tofauti na miaka mingine ambayo kila chuo hufanya chenyewe.

No comments: