Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Li
Yuanchao alitembelea Hifadhi ya Ngorongoro na kuisifia Tanzania kwa jinsi
inavyosimamia masuala ya uhifadhi wa wanyamapori.
Kiongozi huyo wa China alitua nchini kupitia Uwanja Mdogo wa
Arusha juzi jioni katika zira yake ya
siku sita nchini, akitokea Zambia.
Akiwa amefuatana na ujumbe wa China, Yuanchao
alipokelewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na viongozi mbali wa Serikali ya
Tanzania akiwemo Waziri wa Nchi, Utawara Bora, George Mkuchika na Mkuu wa Mkoa
wa Arusha, Magesa Mulongo.
Makamu huyo wa Rais wa China alipata fursa ya kutembelea kreta akiwa
katika hifadhi hiyo, ambayo ni kivutio muhimu nchini.
Bonde la Ngorongoro ambalo ni maarufu duniani
ndiyo sehemu pekee katika Afrika na duniani kote, ambako wanyama pori na
binadamu wanaishi pamoja kwa amani bila shida yoyote.
Eneo la Kreta ya Ngorongoro au Bonde la
Ngorongoro, ndilo eneo maarufu na kivutio kikuu cha maelfu ya watalii
wanaotembelea Mamlaka ya Hifadhi ya
Ngorongoro (NCAA) kila mwaka kutoka kote duniani kwa ajili ya kujifunza na kujifurahisha kwa
kuona wanyama wa aina mbalimbali.
Kiongozi huyo wa China alishuka kwenye Kreta
ya Ngorongoro na kujionea juu ya umbaji
wa Mungu na utajiri wa wanyamapori. Aliitaka Tanzania kuendeleza shughuli za uhifadhi kwa matumizi ya sasa na vizazi
vijavyo.
Alisema
nchi yake inatambua juhudi ya Tanzania katika shughuli za uhifadhi na mapambano
yake juu ya tatizo la ujangili ambalo linatishia uwepo wa wanyamapori. China ni
mdau mkubwa wa maendeleo nchini Tanzania
na katika miaka ya hivi karibuni idadi ya watalii kutoka China imekuwa
ikiongezeka kila mwaka.
No comments:
Post a Comment