JARIBIO CHANJO YA MALARIA LAONYESHA MAFANIKIO



Tanzania ni nchi ya kwanza katika bara la Afrika kufanya jaribio la chanjo ya ugonjwa wa malaria ambapo watu watatu waliofanyiwa majaribio ya chanjo hiyo imeonesha mafanikio makubwa.
Chanjo hiyo ijulikanayo kama PfSPZ Vaccine ilifanyika mwezi uliopita katika Taasisi ya Utafiti wa Afya ya Ifakara iliyoko Bagamoyo, matokeo ya awali yamethibitisha kwamba chanjo hiyo ni rahisi na ina uwezo mkubwa wa kuzuia malaria.
Taarifa hiyo ya majaribio ya chanjo hiyo ilitolewa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo, Dk Salim Abdullah pamoja na watafiti wakuu wa malaria Profesa Stephen Hoffman wa Taasisi ya Sanaria huko Marekani na Mkurugenzi wa taasisi ya utafiti ya magonjwa ya kitropiki ya Uswisi, Profesa Marcel Tanner.
"Idadi ya wasomi 73 walikubali kujitolea katika utafiti huo ambapo mafanikio yake yatasaidia kutokomeza malaria katika nchi za Afrika, ugonjwa huu unaua zaidi ya watu 600,000 kwa mwaka kwa Afrika," alisema.
Alisema ilibidi kuchagua wasomi kwa sababu ni rahisi kwao kuelewa umuhinu wa utafiti huu na kwa kutumia Kituo cha Utafiti cha Bagamoyo maisha ya watu wakiwemo watoto na watu wazima wataepuka vifo vinavyosababishwa na malaria.
Dk Abdullah alisema licha ya kwamba chanjo ya malaria kama hiyo imejaribiwa huko Marekani, utafiti kwa Afrika ni muhimu kwa jamii katika nchi za joto kwa sababu aina ya malaria huwa ni tofauti.
Profesa Hoffman alisema vimelea wanaojulikana kama plasmodium falciparum husababisha malaria kali kwa mgonjwa na utafiti huu umelenga kueneza chanjo kutokomeza aina hiyo kali ya malaria.
"Tuko katika hatua za awali za utafiti lakini kutokana na mafanikio hayo mazuri tunaamini chanjo hii itasaidia kutokoneza malaria kama Polio ilivyotoweshwa duniani," alisema Profesa Huffman.
Alisema katika kipindi kati ya miaka mitatu na mitano ijayo, uzalishaji wa chanjo hiyo utakua mkubwa na utasambazwa katika maeneo mbalimbali duniani ambapo itaokoa watu ambao wangepoteza maisha kutokana na malaria.
Profesa Tanner alisema pamoja na chanjo hiyo kusambazwa kwa wananchi bado matumizi ya vyandarua na aina nyingine ya kujikinga na mbu waambukizao malaria zitaendelea kutumika.
Akitoa shukrani zake kwa watafiti hao, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dk Hassan Mshinda aliwapongeza watafiti hao kwa ushirikiano wao ambao matokeo yake yatatatua changamoto kubwa ya malaria kwa Tanzania na bara la Afrika.

No comments: