EAC KUREKEBISHA SHERIA YA SOKO LA PAMOJA



Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kwa kushirikiana na nchi wanachama inazifanyia kazi sheria ambazo ni vikwazo kwa utekelezaji wa Itifaki ya Soko la Pamoja iliyosainiwa mwaka 2010.
Katibu Mkuu wa EAC, Dk Richard Sezibera alisema mjini Nairobi, Kenya juzi kwamba uhuru wa kufanyakazi, uhamishaji wa mitaji na bidhaa ndani ya nchi wanachama utawezesha raia ndani ya kanda kunufaika na itifaki hiyo ipasavyo.
“Sheria zote za kitaifa hazina budi kuoanishwa ili kuhakikisha kwamba EAC ambayo imebahatika kuwa na rasilimali nyingi inakuwa mgodi wa kuleta maendeleo,” Sezibera alisema wakati wa mkutano wa kwanza wa Jukwaa la Biashara la EAC na Ujerumani.
Sekretarieti ya EAC imebainisha sheria ndogo zaidi ya 6,000 katika nchi wanachama ambazo zinatakiwa kufanyiwa marekebisho ili kuruhusu utekelezaji wa mtangamano kamili wa EAC.
Vikwazo vya kiuchumi ikiwa ni pamoja na vizuizi vya barabarani katika njia kuu ya Kaskazini na kati pia limepewa umuhimu wake.
Katibu Mkuu huyo wa EAC alifafanua pia kwamba Tanzania imekubali kupunguza idadi ya vizuizi vya barabarani kati ya Dar es Salaam na Rwanda na Burundi kutoka 15 vya sasa hadi vitatu ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Matumizi ya vitendea kazi vya kielektroniki pia vitapunguza ucheleweshaji wa kupitisha mizigo mpakani, hususan   mizigo inayosafirishwa kwenda nchi zisizo na bahari kama Rwanda na Burundi.
Rais wa zamani wa Ujerumani, Horst Koher alisema Ulaya iliwachukua muda wa miaka zaidi ya 40 kulegeza masharti ya udhibiti wa mipaka.
“Hata hivyo EAC hainabudi kuyakwepa makosa yaliyofanywa na Umoja wa Ulaya (EU),” alihadharisha wajumbe wa mkutano huo.

No comments: