Mkuu wa Wilaya Kibondo, Venance
Mwamotto ametoa agizo kukamatwa kwa waganga wa kienyeji wanaowapa wajawazito
dawa za kuwasaidia kujifungua.
Mkuu huyo wa Wilaya amesema kwamba
vitendo hivyo vinasababisha kuendelea kwa vifo vya mama wajawazito na watoto
wachanga kwa kushindwa kuhudhuria kliniki na kujifungulia kwenye vituo vya
afya.
Mwamotto alisema hayo mjini Kibondo
wakati wa kampeni ya uhamasishaji jamii kujitolea damu kwa hiari iliyokuwa
ikiendeshwa na Taasisi ya Evidence for Action kupitia kampeni yake
inayojulikana kama Mama Ye.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema kuwa kwa
muda mrefu sasa licha ya uhamasishaji unaofanywa kwa jamii ili kuwapeleka
akinamama wajawazito kujifungua hospitali na vituo vya afya bado jamii imekuwa
ikiendelea kuwatumia waganga wa jadi hali ambayo imechangia vifo vya akinamama
hao.
“Tumehamasisha kwa maneno kwa jamii
kuwahimiza mama wajawazito kujifungulia katika vituo rasmi vya kutoa huduma
lakini bado wengi wanaenda kwa waganga wa kienyeji, agizo kuanzia sasa waganga
wa kienyeji watakaoendelea kuwahudumia na kutoa dawa kwa mama wajawazito badala
ya kuwapeleka hospitali tutawakamata na kuwachukulia hatua,” alisema Mwamotto.
Awali Mganga Mkuu wa Wilaya ya
Kibondo, Emanuel Mwasulama alisema kuwa licha ya maboresho makubwa ya miundo
mbinu ya utoaji huduma yaliyofanywa na Shirika la World Lung Foundation katika
vituo vya utoaji huduma wilayani humo bado vifo vya akinamama wajawazito na
watoto wachanga vimeendelea kutokana na wajawazito kujifungulia nyumbani
na kuchelewa kuhudhuria kwenye vituo vya afya na zahanati.
Wakati huo huo viongozi wa Serikali
ya Kijiji, wahudumu wa afya na wananchi wa Tarafa ya Nguruka katika Wilaya ya
Uvinza mkoani Kigoma wamelalamikia kutokuwepo kwa friji maalumu la kuhifadhia
damu kwenye kituo cha afya Nguruka hali inayofanya wananchi kukatishwa tamaa na
uchangiaji damu kwa hiari.
Walisema hayo wakizungumza na timu
ya waandishi wa habari iliyofanya ziara katika kituo hicho kuona hali ya
udhibiti wa vifo vya akinamama wajawazito na watoto kufuatia uboreshaji wa
miundombinu ya utoaji huduma na ujenzi wa chumba cha upasuaji uliofanywa na
shirika la World Lung Foundation.
Akizungumza jambo hilo Kaimu Mganga
Mfawidhi wa kituo hicho, Beatrice Mtesigwa alisema kuwa kuboreshwa kwa kituo
hicho na kujengwa kwa chumba kidogo cha upasuaji kumechangia kuwafanya akina
mama wajawazito kuongezeka maradufu katika kufuata huduma na kujifungua kwenye
kituo hicho.
Hata hivyo Mwenyekiti wa Kijiji cha
Nguruka, Yakubu Mussa Nzigamiye amesema kuwa licha ya kuboreshwa kwa kituo
hicho cha afya na kujengwa kwa chumba cha upasuaji wanachangamoto kubwa ya
kutokuwepo kwa chumba cha kuhifadhia damu hali ambayo inalazimu kutokuwepo kwa
damu ya akiba.
No comments:
Post a Comment