WAZEE WA CHADEMA WATAKA UKAWA WAREJEE BUNGENI



Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wameomba kuwepo na maridhiano ya madai ya `waumini’ wa kinachoitwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ili warejee katika Bunge la Katiba ili kukamilisha kazi ya kutengeneza Katiba mpya.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa wazee hao, Erasto Singila alisema pamoja na wao kuunga mkono hatua ya Ukawa kutoka bungeni, lakini wanaona ni vyema madai yao, yakasikilizwa ili kuwepo na maridhiano.
“Tunaunga hatua ya Ukawa kutoka, kwa kile tulichokuwa tukiona kikiendelea ndani ya ukumbi wa Bunge, lakini Katiba mpya  tunaitaka, ila madai yao yasikilizwe kuwe na maridhiano ili warejee”, alisema Singila.
Alisema kwa mwenendo wa sasa, ni vigumu Katiba mpya kupatikana na kwamba hata ikipatikana, itakuwa sio yenye maridhiano ya pande zote, wala sio ya wananchi, bali itakuwa imeegemea upande mmoja, hivyo ni vyema maridhiano yakapewa nafasi.
Katika hatua nyingine, Singila alisema leo wameandaa kongamano la wazee, linalofanyika katika ukumbi wa Kituo cha Msimbazi jijini Dar es Salaam, lenye lengo la kuwakutanisha  wazee wa maeneo tofauti ya Kanda ya Pwani  wa chama hicho, kujadili masuala mbalimbali.
Kongamano hilo, litakalofunguliwa na Profesa Abdallah Safari, litazungumzia mada nne, ikiwemo suala la Ukawa na yaliyojiri bungeni, Ushiriki wa wazee katika Chama, huduma za wazee na maendeleo na rasilimali za nchi.
Singila aliongeza kongamano hilo, pia litazungumza kwa urefu juu na mtazamo kuhusu wazee na kwamba sio kweli kuwa wazee ni waoga, bali wapo imara kuangalia mambo yanayojiri nchini.
Alisema katika mada hizo, suala la wazee litapewa kipaumbele, ambapo watazungumza mambo wanayotaka yawepo, ikiwemo sera bora kuhusu wazee, kwani wamelitumikia taifa kwa muda mrefu na sasa wanapaswa kuthaminiwa na kutunzwa.

No comments: