Rais
Jakaya Kikwete, anatarajiwa kuongoza mkutano wa mashauriano ya uwekezaji wa
awamu ya kwanza ya Mradi wa Mabasi ya Haraka (DART), utakaowakutanisha
wawekezaji mbalimbali wa ndani na nje kwenye kituo cha mikutano Mlimani City
jijini Dar es Salaam.
Mtendaji
Mkuu wa DART, Asteria Mlambo aliwaambia waandishi hivi karibuni kuwa mkutano
huo wa mashaurino, utakaofanyika kati ya Juni 3 na 4, mwaka huu, utatoa nafasi
kwa wawekezaji kuzijua fursa mbalimbali za uwekezaji zitakazopatika kwenye
mradi huo unaojengwa kwa mabilioni ya fedha.
“Washiriki
wote kwenye mkutano wa majadiliano, watapata fursa ya kutembelea eneo la mradi
na watapata nafasi ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi wake kuhusu mradi,”
alisema Mlambo na kuongeza kuwa mkutano huo ni muhimu.
Akifafanua
zaidi, Mtendaji huyo Mkuu alisema benki na taasisi mbalimbali za kifedha,
kampuni za kutengeneza mabasi, kampuni za mawasiliano, mifuko ya kijamii
na nyinginezo nyingi zimealikwa kwenye mkutano huo.
“Mada
mbalimbali kuhusu mradi zitatolewa ambapo Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu
,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Jumanne Sagini atawasilisha
mada kuhusu mradi wa DART,” alisisitiza.
Mlambo
alisema kabla ya mkutano huo wa mashauriano mwezi ujao, Wakala ameandaa mkutano
utakaowakutanisha wamiliki wote wa daladala jijini Dar es Salaam pamoja na
Kampuni ya Usafirishaji Dar es Salaam (UDA) na wadau wengine, ili kuwafahamisha
kuhusu mkutano na kushauriana na ni jinsi gani watanufaika na mfumo.
“Tutawaelezea faida na fursa zitakazopatikana
kwenye mfumo mpya wa usafirishaji jijini na jinsi watakavyokuwa sehemu ya
mradi,” alisema Mtendaji Mkuu huyo, na kuongeza kuwa taarifa na ratiba za
mkutano zinapatikana kwenye tovuti ya wakala www.dart.go.tz.
Mwezi
uliopita, DART ilikamilisha usajili wa mabasi ya daladala yanayopita katika
barabara ya Morogoro au kukatiza katika njia hiyo.
Hatua
hiyo ya kuandikisha mabasi hayo ilikuwa moja ya matayarisho ya kupisha mradi
huo wa mabasi yaendayo haraka.
Kwa
sasa wakala huo uko kwenye mchakato wa kuwezesha upatikanaji wa watoa huduma
kwenye mfumo mpya wa mabasi yaendayo haraka awamu ya kwanza ambayo inajumuisha
barabara ya Morogoro, Kawawa na mtaa wa Msimbazi kwa njia kuu na nyingine za
kiungo.
Kulingana
na mpango wa uendeshaji wa mfumo wa DART, barabara zinazohusika, zitapaswa
kutumiwa na mabasi ya mfumo huo pekee.
Jumla
ya ruti 64 jijini Dar es Salaam, zitakoma kutumika kutokana na kuanza kwa
mradi huo.
No comments:
Post a Comment