Wizara ya Ujenzi imesema inaendelea na
maandalizi ya ujenzi wa barabara mbadala kati ya Dar es Salaam na Chalinze kwa
kiwango cha Expressway na itakuwa ya kulipia yenye njia sita.
Waziri Dk John Magufuli alibainisha
hayo juzi usiku wakati alipowasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi
ya wizara yake kwa mwaka wa fedha 2014/15. Aliliomba Bunge liidhinishe bajeti
ya Sh 1,219,717,592,000.
Dk Magufuli alisema barabara hiyo yenye
urefu wa kilometa 100, itajengwa kwa utaratibu wa kushirikisha Serikali na
Sekta Binafsi (PPP).
“Barabara hiyo mbadala ambayo itakuwa
ni ya kulipia, itajengwa kwa njia sita (6 lanes). Barabara iliyopo sasa
itaendelea kutoa huduma kwa wale ambao hawako tayari kutumia barabara ya
kulipia,” alisema Dk Magufuli na kuongeza:
“Wizara imefanya maandalizi ya ujenzi
wa mradi huu ikiwa ni pamoja na kufanya upembuzi yakinifu wa awali
(pre-feasibility study), kutoa tangazo la kualika kampuni kuonesha nia
(Expression of Interest) ya kushiriki katika ujenzi wa barabara hii kwa
utaratibu wa PPP ambapo kampuni 12 zimeonesha kuwa na uwezo wa kujenga barabara
hiyo.”
Alisema Wizara inaendelea na taratibu
za kumpata Mtaalamu Mwelekezi wa mradi ambaye ataisaidia Serikali katika
kufanya upembuzi yakinifu na usanifu, kuandaa nyaraka za zabuni kwa ajili ya
kumpata mbia pamoja na kushauri masuala ya kifedha na kisheria.
Akizungumzia Barabara ya Nelson
Mandela, alisema mwaka ujao wa fedha imetengewa Sh bilioni 1.5 kwa ajili ya
kulipa malipo ya mwisho ya mkandarasi, kwa ajili ya kuimarisha njia hiyo ili
kurahisisha usafiri wa magari ya mizigo yanayotoka Bandari ya Dar es Salaam,
hivyo kupunguza msongamano jijini.
Aidha, alisema katika Mpango wa Matokeo
Makubwa Sasa, maandalizi ya upanuzi wa Barabara ya Nelson Mandela sehemu ya Dar
Port – Tazara ya kilometa sita, yataanza katika mwaka 2014/15 kwa njia sita.
Zimetengwa Sh bilioni 150 kwa ajili ya maandalizi ya upanuzi kwenda Uwanja wa
Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).
Kuhusu njia za juu “flyovers”, Dk
Magufuli alisema Sh bilioni moja za ndani na Sh bilioni 15 fedha za nje,
zimetengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa “flyover” ya Tazara.
Aidha, alisema zimetengwa Sh milioni
100 kwa ajili ya kulipa fidia kwa mali na kuhamisha miundombinu ya huduma za
kijamii zitakazoathirika na ujenzi wa “flyover” hiyo eneo la Tazara.
Kuhusu ukarabati na kupanua barabara ya
lami ya sehemu ya Gerezani (Kamata – Bendera Tatu) kutoka njia mbili za sasa
hadi njia nne chini ya msaada kutoka Serikali ya Japan na Serikali ya Tanzania,
usanifu wa kina na utayarishaji wa zabuni umekamilika.
“Kazi ya kuhamisha miundombinu iliyoko
eneo la ujenzi zinaendelea. Aidha, taratibu za kutafuta mkandarasi zinaendelea.
Katika mwaka wa fedha 2014/15, mradi huu umetengewa Sh milioni 2,000 fedha za
ndani na Sh milioni 6,000 fedha za nje kwa ajili ya kukamilisha ulipaji fidia
na kuanza ujenzi wa sehemu ya Kamata – Bendera Tatu (kilometa 1.5),” alisema Dk
Magufuli.
No comments:
Post a Comment