Kundi la watoto nchini Tanzania wenye
kinga asilia ya malaria, wanawasaidia wanasayansi kutengeneza kinga mpya ya
ugonjwa huo.
Watafiti wa Marekani wamebaini miili ya
watoto hao, hutoa viini vya kinga ambavyo hushambulia wadudu wanaosababisha
malaria.
Watafiti hao walisema mtu akidungwa
sindano yenye viini hivyo vya kinga asilia vya binadamu, vinaweza kumkinga na
ugonjwa huo.
Ripoti ya watafiti hao imechapishwa
katika jarida la kisayansi nchini humo,
na kusema majaribio ya utafiti huo, yalifanywa kwa sokwe na binadamu na kwamba
hivi sasa yanahitaji kutathminiwa kikamilifu ili kupata matumaini halisi ya
chanjo ya malaria.
Mkurugenzi wa Kituo cha Utafiti wa Afya
cha Kimataifa katika Hospitali ya Kisiwa cha Rhode cha Chuo Kikuu cha Tiba cha
Brown, Profesa Jake Kurtis, alisema
anaamini upo ushindi wa kuaminika na matokeo hayo ni ishara ya upatikanaji wa
chanjo dhidi ya ugonjwa huo.
"Hata hivyo wadudu wa malaria ni
vigumu kuwashambulia, ni maadui wakubwa wa fya ya binadamu", alisema
Kurtis.
Utafiti huo ulianza kwa kundi la watoto 1,000 nchini Tanzania, ambao sampuli za damu
yao zilichunguzwa mara kwa mara katika miaka ya mwanzo ya maisha yao .
Kati ya sampuli hizo, asilimia sita ya
watoto hao waliochukuliwa sampuli walikuwa na kinga asilia dhidi ya malaria,
licha ya wao kuishi katika eneo ambalo ugonjwa huo umekithiri.
Taarifa za Shirika la Afya Duniani
(WHO) za mwaka 2012, zinasema ugonjwa wa malaria umeua watu zaidi ya 600,000,
huku asilimia 90 ya vifo hivyo ni vya wagonjwa kutoka Kusini mwa Jangwa la
Sahara, ikiwemo Tanzania.
No comments:
Post a Comment