Serikali imewataka Watanzania kuwa
mashujaa wa kuomba vitalu vya uwekezaji katika mashamba ya mifugo
vinapotangazwa badala ya kuwaachia watu kutoka nje.
Aidha, Wizara ya Fedha imesema itatoa
Sh bilioni 10.5 kati ya takribani Sh bilioni 20 zilizosalia ambazo zilitengwa
katika bajeti ya mwaka wa fedha 2013/14 ya Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na
Uvuvi, ili kukamilisha baadhi ya miradi ya maendeleo.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi,
Dk Titus Kamani alisema hayo juzi jioni wakati akihitimisha mjadala wa bajeti
ya wizara hiyo kwa mwaka 2014/15 bungeni mjini hapa.
Dk Kamani alisema: “Watanzania tuwe
mashujaa katika kuomba vitalu vya uwekezaji. Watanzania wengi wanaogopa. Vitalu
hivi si kwa ajili ya watu wa nje pekee. Ni muhimu kuwatambua wazawa.”
Waziri alisema hadi sasa kuna vitalu
105 vya mashamba ya uwekezaji ambavyo vimebinafsishwa kwa wawekezaji, na
kurejea kauli yake kwamba vile ambavyo havifanyi vizuri, Serikali itavichukua
na kuvigawa upya.
Akizungumzia ruzuku kwa wavuvi, alisema
katika mwaka ujao wa fedha zimetengwa Sh bilioni 2.2 kwa ajili ya wavuvi
wadogo, tofauti na madai ya Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), kwamba
hakukuwa na fedha hizo katika bajeti ya waziri.
Aidha, alikubaliana na michango ya
wabunge wengi kuwa sekta ya mifugo na uvuvi, ikitumiwa fedha, itasaidia sana
kuleta tija na ufanisi na kukuza uchumi wa Taifa.
Kuhusu fedha za bajeti inayomalizika,
Waziri huyo pamoja na Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima, walitangaza kwamba
Hazina itatoa Sh bilioni 10.5 ili zikamilishe baadhi ya miradi iliyopangwa
kufanyika katika mwaka huo wa fedha unaoishia Juni 30, 2014.
Wakati Bunge lilipokaa kama Kamati
kupitisha bajeti hiyo, Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa (Chadema),
alizungumzia suala la migogoro ya wafugaji na wakulima na kutaka kufahamu hatua
ambazo waziri huyo pamoja na Naibu wake,
Kaika Telele ni wapya katika wizara, watachukua kukomesha kadhia hiyo.
Hoja yake iliibua mjadala mkali, lakini
mwishoni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William
Lukuvi alisema Kamati iliyoundwa na Bunge chini ya Mwenyekiti wa Kamati ya
Kudumu ya Kilimo, Mifugo na Maji, Profesa Peter Msolla imekamilisha kazi yake
na ripoti iko kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda.
Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu
aliyekuwa akiendesha kikao cha juzi, alilieleza Bunge kuwa atamshauri Spika
kuiwasilisha haraka bungeni ripoti hiyo ili ijadiliwe; hoja ambayo ilikubaliwa
na Msigwa ambaye alitangaza kuondoa Shilingi katika mshahara wa Waziri.
No comments:
Post a Comment