WASOMI WA SAUT WAMWALIKA SUMAYE KAGERA



Wasomi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (Saut), wamemualika aliyekuwa Waziri Mkuu, Fredrick Sumaye mkoani Kagera, kwenda kutoa mihadhara kwa wasomi  na  watu wa kada mbali mbali katika mkoa huo.
Mwaliko huo umetokana na mihadhara aliyotoa katika vyuo vikuu mbali mbali nchini Marekani hivi, ambayo iliwagusa kiasi cha kuamua kufanya Kongamano kuchambua mada mbalimbali  alizotoa kiongozi huyo.
Taarifa ya wasomi hao iliyotumwa jana kwa vyombo vya habari, ilieleza kuwa wasomi hao wameamua kuendelea kuchambua hotuba hizo kwa kuoanisha na mazingira ya sasa ya Tanzania na Bara la Afrika.
Pia walikubaliana watumie wigo na wasomi wenzao wa vyuo mbalimbali hapa nchini, ili kupata mawazo zaidi  kwa faida ya Watanzania.
Wasomi hao wapatao 189 wanatoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (Saut), Kampasi ya Bukoba,  Tumaini University na shule za sekondari za Ihungo, Rugambwa, Nyakato na Kahororo.
Sumaye alikuwa nchini  Marekani kwa karibu mwezi mmoja na alirejea  nchini Aprili mwaka huu. Akiwa huko alipata nafasi ya kutoka mihadhara katika Chuo Kikuu cha  Wellesley  Boston, Morehouse College Atlanta George (USA), Elizabeth State University North Caroline (USA),  na Havard University katika 20th Annual International Conference  Day.
Mada iliyokuwa na mjadala mkali ilikua ni kuhusu viongozi wengi wa Afrika kutokuwa na moyo wa uzalendo na hasa kujitumbukiza katika  rushwa kubwa kubwa, kujilimbikizia  mali na kuficha fedha  katika mabenki ya Ulaya huku bara la Afrika likiendelea kuwa masikini.
Pia wasomi hao walijadili kuhusu hali ya elimu duni isiyoendana na dunia ya leo, vifo vya watoto na wajawazito, miundombinu hafifu, vita ya wenyewe kwa wenyewe na matatizo mengi yanayoikabili bara la Afrika.
Kuhusu suala la haki za binadamu wasomi walikubaliana kuwa umefika wakati sasa wa nchi za kiafrika kuchukua hatua za haraka kuhakikisha kuwa watu wote wanapata haki zao za msingi bila kubaguliwa hasa katika masuala ya elimu, chakula, afya, haki za kupata habari.
Kuhusu Afrika kushiriki katika uchumi wa dunia walikubaliana na  Sumaye kuwa umefika wakati bara la Afrika lisiangaliwe kama chimbuko la rasilimali tu bali kama mbia na mshirika mkubwa katika uchumi wa dunia kwa kuwa  lina rasilimali kubwa ya ardhi yenye rutuba, madini, maji na hata rasilimali watu. Pia suala la  waafrika  kujitambua  ni jambo lililojitokeza kwenye mada za wasomi hao.

No comments: