WANYAMAPORI WAUNDIWA RASMI MAMLAKA YAO


Katika kuhakikisha kunakuwa na uhifadhi endelevu wa wanyamapori nchini, serikali imetangaza kuanzisha Mamlaka ya Hifadhi ya Wanyamapori inayotarajiwa kuanza kazi mwishoni mwa mwezi huu huku makao yake makuu yakiwa mkoani Morogoro.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alisema sambamba na uanzishwaji wa mamlaka hiyo, pia itaundwa bodi maalumu itakayokuwa na wajumbe wasomi na waadilifu ambao wataleta ushindani katika sekta hiyo umuhimu.
Nyalandu alisema hayo jana wakati akihutubia Mkutano wa Kimataifa wa Kuzuia Uhalifu wa Wanyamapori na kuendeleza Uhifadhi wa Wanyamapori uliokutanisha wadau mbalimbali wakiwemo viongozi wa serikali, jumuiya za kimataifa, wafanyabiashara na wadau wengine katika sekta ya utalii na maliasili.
Aidha, Nyalandu alisema pia wanatarajia kuanzisha Bodi ya Nidhamu itakayosimamia kanuni za maadili wakati askari wanyamapori wakitekeleza majukumu yao ili kudhibiti yasitokee kama yale yaliyotokea wakati wa Operesheni Tokomeza.
Nyalandu alisema matarajio ya mkutano huo wa siku mbili ni serikali kujadili na wadau mbalimbali kuona njia bora zaidi ya kukabiliana na ujangili na kulinda tembo wa Tanzania.
Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal akifungua mkutano huo alisema Sekta ya Maliasili na Utalii imekuwa ikichangia kwa kiasi kikubwa Pato la Taifa pamoja na kukabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ujangili, ongezeko la uhitaji wa bidhaa za wanyamapori na uharibifu unaofanywa na wakazi.
Aidha Dk Bilal alisema ukosefu wa fedha za kutosha, vifaa, teknolojia na mafunzo ni changamoto kubwa na kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kusaidia katika maeneo hayo ili askari hao waweze kukabilianana wahalifu hao.
“Tafadhali Jumuiya ya Kimataifa na marafiki tunaomba mtuunge mkono na kutusaidia kuchukua hatua za kiusalama kuhakikisha tunalinda tembo wetu wasiendelee kuteketezwa na majangili,” alisema.
Makamu Mwenyekiti wa Taasisi ya Kimataifa inayosimamia Hifadhi (ICCF-Group), Dk Kaush Arha alisema Urithi wa Asili umevamiwa na kwamba wadau wamekutana pamoja kujadiliana na kutoka na hatua maalumu na namna ya kuziendeleza au kuziboresha.

No comments: