WANAOUZA WASICHANA WADOGO KUFANYA UKAHABA CHINA WANASWA


Baada ya kuwepo malalamiko ya wasichana wadogo wa nchini kusafirishwa kwenda China  kutumikishwa katika biashara ya ngono pamoja na dawa za kulevya, sasa serikali imenasa mtandao huo.Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe alitoa taarifa hiyo  juzi bungeni wakati akihitimisha michango  kuhusu bajeti  yake kwa mwaka wa fedha 2014/15 iliyopitishwa. 
Chikawe ambaye hata hivyo hakufafanua kwa undani wa mtandao huo ulivyokamatwa, alieleza Bunge namna watoto hao wanavyopatikana kabla ya kufikishwa nchi hiyo ya nje. 
Kwa mujibu wa Waziri, watu hao wamekuwa wakichukua watoto wadogo na kuwaambia kwamba wanawapeleka China hususani mji wa Guanzhou kuwaajiri kwenye saluni na maduka. 
Alisema kinara wa usafirishaji amekuwa akitambuliwa kwa jina la ‘Mama’ ambaye baada ya kufika nchini humo, huwanyang’anya watoto hao hati zao za kusafiria. Imebainika zipo hata wakala zinazojihusisha na biashara hiyo haramu ya binadamu. 
“Wakifika, Mama anawanyang’anya pasipoti zao. Anawaambia ili kuwarudishia, lazima watimize masharti ya kumpa kati ya dola 8,000 na 10,000 baada ya kutumika katika vitendo vya ngono,” alisema Waziri Chikawe. 
Aliendelea kueleza kuwa wanaposhindwa kutimiza masharti hayo, hukutana na Wanigeria ambao huwapa hati bandia za kusafiria na kisha kuwaingiza katika biashara ya kusafirisha dawa za kulevya kwenda nchi mbalimbali. 
“Tumenasa mtandao huu…polisi imenasa mtandao,” alisema Waziri na kutoa mfano kwamba hivi karibuni, alikamatwa mtu akiwa na hati ya kusafiria akimpelekea binti mmoja. Alisema binti huyo alipoulizwa juu ya hati hiyo, alikuwa hafahamu anakokwenda. 
Awali, taarifa juu ya kuwepo usafirishaji wa wasichana wadogo kwenda China kwa ajili ya kutumikishwa katika ngono, ilitolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe baada ya kutoka ziarani nchini humo. 
Membe alisema serikali inashirikiana na ubalozi wa China katika kubaini wahusika wa biashara hiyo sanjari na mkakati wa kuhakikisha wasichana hao wanarudishwa nchini. 
Akielezea mikakati ya serikali katika kukabili biashara haramu ya usafirishaji wa binadamu, Waziri Chikawe alisema katika mwaka wa fedha 2013/2014 Sekretarieti ya kupambana na biashara hiyo imeratibu vikao vinne vya Kamati ya kupambana nayo. 
Aidha imeandaa kitabu cha anuani na majina ya watoa huduma kwa waathirika wa biashara haramu ya usafirishaji binadamu na vilevile kutengeneza rasimu ya kanuni za sheria ya kupambana na biashara hiyo nchini. 
Katika mwaka wa fedha 2014/2015 sekretarieti itakamilisha kutengeneza kanuni za Sheria ya kupambana na biashara hiyo ya mwaka 2008. Pia itatoa elimu na kuimarisha mikakati ya kupambana na biashara hiyo ya kusafirisha binadamu. 
Watanzania zaidi ya 100 wakiwemo wasichana 20 wamedaiwa wapo gerezani nchini China wakijihusisha na biashara ya dawa za kulevya na miongoni mwa matukio ya hivi karibuni ni la mwanamitindo, Jackie Clief (28) aliyekamatwa na kilo 1.1 za heroini huko Macao, China. Dawa hizo 66 zenye thamani ya dola za Marekani 137, 720 alikuwa amezimeza na akizipeleka katika mji wa Guanzhou.

No comments: