Jeshi la Polisi nchini limewatimua jumla ya wanafunzi wa uaskari 237 wa Chuo cha Taalumu ya Polisi Moshi, kutokana na makosa mbalimbali yakiwemo ya kughushi vyeti, matatizo ya kiafya pamoja na makosa ya kinidhamu.
Akitoa taarifa hizo jana katika ukumbi wa chuo cha
Taaluma ya Polisi Moshi, Kamishna wa Utawala na Utumishi ndani ya Jeshi la
Polisi, Thobias Andengenye alisema wanafunzi wa uaskari waliofukuzwa kwa
kughushi vyeti ni 212 na wengine 25 ni kwa makosa ya kinidhamu na matatizo ya
kiafya.
Andengenye alisema katika kuhakikisha jeshi la polisi
linaendelea kuwa na askari wenye weledi na uaminifu kwa raia na taifa,
lilianzisha uhakiki wa vyeti kwa kushirikiano na Baraza la Mitihani Taifa,
ambapo wanafunzi wa uaskari 212 walionekana vyeti vyao ni vya kughushi.
"Kutokana na maboresho ya jeshi la polisi la
kutaka askari wenye weledi na kulitumikia taifa, tumeona tuanze uhakiki wa
vyeti, kwa kushirikiana na baraza la mitihani, ambapo vyeti vya wanafunzi wa
uaskari 212 kati ya walioripoti vimeonekana ni vya kughushi, hivyo tumeona
tuwaachishe masomo," alisema CP Andengenye.
Alisema tatizo kama hilo linaweza kusababisha taifa
kupata madhara makubwa kwa kuwa na watu ambao sio wataalamu husika, hivyo jeshi
la polisi litaendelea kufanya uchunguzi kwa kushirikiana na taasisi nyingine
kwa lengo la kuzuia mianya hiyo.
Alibainisha wanafunzi waliofukuzwa wamefunguliwa
mafaili yao, kwa ajili ya kuwafuatilia mienendo yao wakiwa uraiani na kutokana
na mafunzo ambayo wamekwisha yapata, ili wasije kujihusisha na masuala ya
uhalifu.
Andengenye alisema wanafunzi wote walibainika kughushi
vyeti watachukuliwa hatua mara baada ya upelelezi kukamilika kwa kushirikiana
na taasisi nyingine, ikiwemo Baraza la Mitihani la Taifa.
Alisema jeshi la polisi lina mkakati wa kubadilisha
mfumo wa ajira, ambapo watakuwa wanapokea wanafunzi kutoka vyuoni na mashuleni,
ambapo wataachana na njia ya kupokea maombi kwa njia ya barua hali
itakayosaidia kupata watu wanaopenda kazi za uaskari.
Pia jeshi hilo linaenda kwenye maboresho ya alama za
vidole nchi nzima, ambapo patakuwepo na data za watu wote waliofanya makosa,
hivyo endapo mtu yeyote atakapofanya kosa na kukimbilia sehemu nyingine,
atakapokamatwa kosa lingine taarifa zake zitasoma makosa yake yote.
Andengenye alisema kitendo chochote cha kughushi ni
kosa la jinai, ambapo aliwataka wananchi wote kuacha tabia kama hizo na badala
yake wafuate taratibu na sheria zilizopo kwa ustawi wa taifa.
No comments:
Post a Comment