Mgomo wa wafanyakazi wa
Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia umesababisha hasara ya Sh bilioni 2.65
ambazo sasa Serikali imesema wafanyakazi watakatwa kwenye mishahara yao
kufidia.
Wafanyakazi hao ambao
jana wametangaza kusitisha mgomo huo baada ya Mahakama kuubatilisha juzi,
imeelezwa kwamba mishahara yao itakatwa kwa utaratibu utakaowekwa na
Menejimenti.
Akizungumza na waandishi
wa habari kwenye viwanja vya Bunge mjini hapa, Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison
Mwakyembe, alisema mgomo huo ulioanza Mei 12 mwaka huu,
umesababisha hasara ya dola za kimarekani milioni 1.6 sawa na Sh bilioni
2.65.
Awali, Dk Mwakyembe
alitaka wafanyakazi hao kutii amri ya Mahakama kwa kurejea kazini na kusema
atakayekaidi atakuwa amejifukuzisha.
Aidha alisema Serikali
itachukua hatua kali za kinidhamu kwa wafanyakazi na viongozi wa chama cha wafanyakazi
watakaochochea migomo kinyume cha sheria ili kurejesha ufanisi katika mamlaka
hiyo.
Kwa mujibu wa Dk
Mwakyembe, Mahakama Kuu Kitengo cha Kazi juzi ilitoa uamuzi kuwa mgomo huo ni
batili na ikataka wafanyakazi kurejea kazini baada ya Menejimenti
kupeleka suala hilo kwenye Mahakama hiyo kupata ufumbuzi.
Alisema wafanyakazi hao
kwa upande wa Tanzania waligoma kinyume cha sheria kwa madai ya kutolipwa
mishahara ya Februari kwa baadhi ya wafanyakazi pamoja na mishahara ya Machi na
Aprili mwaka huu.
Alisema Zambia
wanaendelea na kazi licha ya kutolipwa kwa kutambua kuwa mapato ya mamlaka hiyo
ni madogo ya dola milioni moja huku matumizi ikiwa dola milioni 2.5.
Mwakyembe alisema Mei 21
mwaka huu, Wizara iliagiza Menejimenti kuzungumza
na wafanyakazi hao lakini waligoma kurejea kazini.
Baadaye Wizara
ilizungumza na uongozi wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli nchini (Trawu) na
kukubaliana iwapo Serikali ingelipa mishahara ya Februari na Aprili wangerejea
kazini kuanzia Mei 19 mwaka huu.
“Serikali ya Tanzania
ilitimiza ahadi ya kulipa malimbikizo ya mishahara ya miezi hiyo kwa kuingiza
fedha hizo katika akaunti ya Tazara Mkoa wa
Tanzania na baadhi ya wafanyakazi kuthibitisha kupokea fedha hizo,”
alisema Dk Mwakyembe.
Hata hivyo alisema,
cha kushangaza baada ya kupokea fedha hizo wafanyakazi hao walianzisha madai
mapya ya kutaka madaraka ya Mamlaka yarejeshwe kwenye mikoa yaani ya
Tanzania na Zambia na kutoa msimamo wa kutorejea kazini hadi
yatakapotekelezwa.
Waziri alisema kutokana
na madai hayo, Menejimenti ya Tazara ilizungumza na uongozi wa Trawu na
kuwaeleza kuwa suala hilo linahitaji uamuzi wa bodi kwa kuwa linahusu wanahisa
wote wawili jambo ambalo Trawu hawakukubaliana na ushauri huo.
Menejimenti baada ya
kuona kungetokea mgogoro wa kikazi, iliamua kupeleka suala hilo Mahakama Kuu
Kitengo cha Kazi ambayo imetoa uamuzi kwamba mgomo huo ni batili.
Akizungumza jana
Mwenyekiti wa Trawu, Kanda ya Dar es Salaam, Yusuph Mandai alisema wafanyakazi
wamekubali kutii amri ya Mahakama na kurejea kazini kuanzia jana ingawaje
hawajajua hatma yao.
Alisema wamekubali
kurudi kazini bila kujua hatma ya mishahara yao, ingawaje baadaye wataangalia
ni kitu gani cha kufanya.
Kuhusu mgomo kusababisha
hasara na kutakiwa kukatwa katika mishahara yao, alisema taarifa hiyo
hawajaipata rasmi.
Hata
hivyo kiongozi huyo wa
wafanyakazi, alihoji, “Kama fedha hizo zinaweza kupatikana kwa kipindi cha
mgomo pekee, kumbe wafanyakazi wangeweza kulipwa mishahara yao wanayoidai.”
Alisisitiza, “Tatizo letu
kubwa ilikuwa ni kulipwa mishahara ambayo tulikuwa tunaidai…unajua hatulipwi
kabisa na hata hatujui baada ya kukubali kutii amri ya Mahakama hatma yetu
itakuwaje”, alisema Mandai.
No comments:
Post a Comment