Serikali
inatarajia kuweka utaratibu maalumu wa ajira kwa walimu wenye ufaulu wa juu
katika elimu ya sekondari, watakaojiunga kusomea Stashahada ya Ualimu wa
Sayansi na Hisabati chini ya utaratibu wa kupewa ruzuku na mikopo.
Waziri
wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, alisema hayo mwishoni mwa
wiki wakati akiwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara yake kwa mwaka 2014/2015
aliyosoma bungeni mjini hapa.
Dk
Kawambwa alisisitiza azma ya Serikali kuimarisha vigezo na utaratibu wa
kupata walimu wa elimu ya msingi na sekondari kwa kutumia kigezo cha ufaulu wa
daraja la tatu katika elimu ya sekondari. Alisema hiyo ndiyo sifa ya chini ya
kujiunga na kozi ya ualimu katika ngazi yoyote ya ualimu.
Alisema
katika kuhakikisha elimu bora inatolewa, wameweka utaratibu wa kuanza
kutoa ruzuku na mikopo kwa wanachuo wenye sifa watakaojiunga na mafunzo ya
Stashahada ya Ualimu wa Sayansi na Hisabati ili kuvutia wenye ufaulu wa juu na
wenye sifa linganishi, kujiunga na ualimu katika maeneo hayo.
Alisema
Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na
Serikali za Mitaa (Tamisemi) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma,
itaweka utaratibu maalumu kuhusu ajira ya walimu watakaopatikana kupitia
utaratibu huo ili watumishi hao watumikie jamii kama
inavyotarajiwa.
Alisema
wamerejesha utaratibu wa kujiunga na mafunzo ya ualimu kwa walimu wa sekondari
kwa masomo ya sayansi kwa miaka mitatu kwa wahitimu wa kidato cha nne.
Utaratibu huu unaanza kutekelezwa rasmi Julai mwaka huu.
Hata
hivyo, Waziri Kawambwa alisema pamoja na mikakati mbalimbali kufanyika, bado
mwendo ni mrefu wa kufikia lengo la kumwandaa mwalimu mahiri na mwenye weledi
wa kutosha.
“Hili
linahitaji wadau wote tuendelee kushirikiana…wizara yangu itaendelea kutimiza
wajibu wake katika upatikanaji wa walimu bora nchini,” alisema
Kawambwa.
Kwa
mujibu wa taarifa ya Waziri Kawambwa, kwa sasa taifa lina upungufu wa walimu
30,949 wa shule ya msingi na walimu 24,596 wa sekondari hususani Sayansi na
Hisabati.
Hata
hivyo, upungufu ulikuwa mkubwa zaidi kabla ya Serikali kuajiri walimu wapya
36,338 mwaka huu. Kati ya idadi hiyo ya walioajiriwa, walimu wa
masomo ya Sayansi na Hisabati ni 2,364, ngazi ya cheti 17,928, Stashahada 5,416
na Shahada ni walimu 12,994.
Kawambwa
alisema Wizara na wadau wake, itaendelea kuwaandaa kulingana na mikakati na
kadri rasilimali zinazohitajika zinavyoendelea kupatikana.
No comments:
Post a Comment