Wafanyabiashara wa Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo
(DRC), wameelezea na matumaini yao kwa hatua ya Tanzania kufungua ofisi ndogo
ya mawasiliano ya Mamlaka ya Bandari (TPA) mjini Lubumbashi, Katanga nchini
humo.
Wakizungumza kwa niaba ya wenzao baada ya
kuzinduliwa kwa ofisi hiyo hivi karibuni, wafanyabiashara hao wanaopitisha
mizigo yao katika Bandari ya Dar es Salaam, wamesema kuanzishwa kwa ofisi hiyo
kumekuja wakati muafaka na kuwa itawarahisishia biashara yao.
Mmoja wa wafanyabiashara hao, Mubanzo Fils anayeendesha kampuni ya ETS
Mubanzo, alisema jumuiya ya wafanyabiashara Lubumbashi imefurahia kupata ofisi
hiyo wanayotarajia kurahisisha kazi zao na kukuza biashara baina ya nchi hizo
mbili.
“Tuna furaha kubwa kwa hatua hii muhimu,” alisema.
Inatarajiwa tatizo lililokuwa likiwakabili
wafanyabiashara hao la kukabiliana na wakala wa kupakia na kupakua mizigo wasio
waaminifu, sasa itakuwa historia kwa kuwa ofisi ya Lubumbashi itakuwa na orodha
ya wakala wanaokubalika na waaminifu.
Pia mienendo ya taarifa za mizigo itafanyika mjini
humo na kuharakisha taratibu za mizigo
bandarini hapo.
Kwa upande wake, Lumbu Useni wa kampuni ya Luwang
SPRL alitoa mwito kwa wafanyakazi kwenye ofisi hiyo kutimiza lengo
lilikusudiwa. “Wafanye kazi kwa bidii na akili zao zote ili lengo
lililokusudiwa na nchi hizi lifikiwe na sisi tuweze kufaidika.”
Mfanyabiashara mwingine, Mohamed Hassan Hammy, Mkurugenzi Mtendaji wa
kampuni ya Drill Tek ya mjini humo alisema Kongo ni soko kubwa hivyo Tanzania
imefanya busara kubwa kufungua ofisi hiyo.
Mizigo ya DRC inayopita katika Bandari ya Dar es
Salaam imekuwa ikiongezeka kwa asilimia takribani 24 kwa mwaka tangu mwaka
2004, kutoka tani 155,611 hadi tani 1,117,249 mwaka 2013.
No comments:
Post a Comment