WAJAWAZITO 100,000 WANUFAIKA NA MRADI WA NHIF

Mradi wa huduma za afya kwa akinamama wajawazito wasio na uwezo na watoto, unaotekelezwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na Benki ya Maendeleo ya Watu wa Ujerumani (KfW), umevuka lengo kwa asilimia 155 kwa kuwanufaisha wajawazito 109,184 hadi sasa.
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Hamis Mdee, alisema jana kuwa  mradi huo unaotekelezwa katika mikoa ya Tanga na Mbeya, hadi Machi 31, mwaka huu umewanufaisha wajawazito 109,184, ikiwa ni sawa na asilimia 155 ya lengo la kuwafikia wajawazito 70,000 ifikapo Desemba mwaka huu.
Lengo la mradi huo ulioanzishwa Januari 2012 ni kuhakikisha wajawazito 700,000 wasio na uwezo katika mikoa hiyo, wanapata uhakika wa huduma bora za uzazi na salama kupitia mfuko huo wa bima ya afya  na kuchangia upatikanaji wa vifaa bora vya kisasa vya kuwahudumia na pia kuzikinga familia za akinamama hao kwa kuwapatia kadi za matibabu katika kipindi hicho.
Mdee alitaja mafanikio mengine ya mradi huo, uliogharimu Euro milioni 13, ambapo Euro milioni 6.6 zimetolewa na NIHF, ni akinamama zaidi ya asilimia 60 sasa wanajifungulia katika vituo vya matibabu, ikiwa ni kiwango cha juu cha wastani wa kitaifa ambacho ni asilimia 50.
Alisema vifo vya watoto wachanga, vimepungua kutoka vifo tisa kwa vizazi hai 1,000 hadi kufikia vifo sita kwa kila vizazi hai 1,000.
“Haya ni mafanikio makubwa kwa sababu jinsi unavyokaribia kumaliza tatizo, ndio unakuwa na changamoto ngumu zaidi,” alieleza Mdee.
Pia alisema kasi ya vifo vya wajawazito imepungua kutoka 170/100,000 mwaka 2011 hadi 139/100,000 mwaka 2013.
 Alitaja changamoto za mradi kuwa ni upatikanaji wa dawa usioridhisha katika vituo vya matibabu, licha ya kuwa vituo vya matibabu vina vyanzo vya uhakika wa fedha.

No comments: