Mamlaka ya Reli la Tanzania na Zambia
(Tazara) imewapeleka mahakamani wafanyakazi wake waliokuwa wamegoma,
wakishinikiza kulipwa fedha zao za mishahara.
Wafanyakazi hao wameendelea kugoma licha ya
Serikali kutoa Sh bilioni 1.6 kulipia
mishahara hiyo wiki iliyopita.
Wamegoma kutoa huduma, kwa madai kuwa
fedha hiyo iliyotolewa na serikali ni ya
miezi miwili tu na kwamba umebakia
mshahara wa mwezi mmoja.
Akizungumza na mwandishi jana Dar es Salaam,
Mwenyekiti wa Kanda ya Dar es Salaam wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli nchini
(Trawu), Yusuph Mandai alisema
menejimenti iliwapeleka Mahakama
Kuu Divisheni ya Kazi, kwa madai
wafanyakazi hao kufanya mgomo kinyume na sheria.
“Ni ukweli kuwa tumeshtakiwa katika mahakama
hiyo iliyopo Kinondoni, ambapo Ijumaa
tulipofika shauri hilo liliahirishwa kutokana na maelezo kuwa lilitakiwa
kufanyiwa marekebisho,” alisema Mandai. Alisema kuwa hata jana, waliitwa tena
mahakamani.
Alisema menejimenti inadai kuwa mgomo huo
siyo wa kisheria. Alisema menejimenti hiyo inataka mahakama kutoa amri ya
wafanyakazi hao, kurudi kazini.
Alisema walikwenda tena jana mahakamani
kusikiliza shauri hilo.
Katika hatua nyingine, mwandishi alimtafuta
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, kwa
ajili ya kuzungumzia suala hilo, ambapo alipokea simu na kudai yuko mkutanoni,
huku Msemaji wa Tazara akidai kutokuwapo kazini.
Mgomo wa wafanyakazi hao, ulianza wiki mbili zilizopita, ambapo
walikataa kurudi kazini hadi hapo watakapolipwa fedha yote.
Serikali imeshatoa Sh bilioni 1.6 kwa ajili
ya mishahara hiyo, lakini wafanyakazi hao wanadi kuwa ni ya miezi miwili tu,
ambapo umebakia mwezi mmoja, ambao fedha yake haijaingizwa katika akaunti ya
Tazara, hivyo hawawezi kurudi kazini.
“Fedha inayodaiwa kutolewa bado wafanyakazi
hawajaiweka mifukoni, lakini pia bado mwezi mmoja ambao fedha yake
hazikuwekwa,” alisema Mandai.
Alisema kuwa ili kuendesha Tazara kwa ufanisi mkubwa, wafanyakzi hao
warudishiwe madaraka.
No comments:
Post a Comment