WABUNGE WATAKA UWEKEZAJI ZAIDI KATIKA MIFUGO, UVUVI



Wabunge wameitaka Serikali kuongeza uwekezaji katika sekta ya mifugo na uvuvi ili itoe mchango mkubwa katika Pato la Taifa, huku wakisisitiza kuwa matumizi bora ya ardhi yataepusha migogoro inayoota mizizi ya wakulima na wafugaji nchini.
Aidha, kwa upande wake, Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), amesema atatema ubunge wake pamoja na kutoa fedha Sh milioni 50 endapo Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi itamuonesha fedha za ruzuku zilizotengwa kwa ajili ya wavuvi.
Wabunge hao walikuwa wakichangia bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi iliyowasilishwa bungeni juzi na Waziri Dk Titus Kamani ambaye anaomba Bunge liidhinishe makadirio ya matumizi ya Sh 66,142,627,000.
Takriban wabunge zaidi ya 15 waliochangia kwa kuzungumza bungeni jana, walisema sekta ya mifugo na uvuvi inaweza kuisaidia kukuza uchumi wa Taifa na kusaidia sekta nyingine zisizo za uzalishaji mali kama vile elimu na afya, endapo bajeti yake itaongezwa zaidi.
Lugola katika mchango wake, mbali ya mambo mengine, alisema, "Waziri amesema atatoa ruzuku kwa wavuvi, lakini nimetazama katika vitabu vyote sijaona fedha. Ikifika jioni, kama Waziri atanionesha fungu hilo, nitatema ubunge wangu na nitatoa cheki ya shilingi milioni hamsini. Maana tumekuwa tunapiga porojo tu."
Mbunge wa Kiteto na Naibu Waziri wa zamani wa wizara hiyo, Benedict ole Nangoro, alisema kama sekta hizo mbili zitaongezwa fedha, zitaleta manufaa makubwa, huku akisisitiza Serikali kusimamia bila upendeleo masuala ya migogoro ya wakulima na wafugaji.
Kwa upande wake, Mbunge wa Kibaha Vijijini, Hamoud Jumaa (CCM), mbali ya bajeti, aligusia kusuasua kwa ujenzi wa machinjio ya Ruvu, Mlandizi mkoani Pwani; hoja ambayo pia ilichangiwa na Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete (CCM).
Ridhiwani pia alisisitiza matumizi bora ya ardhi na kutaka kuwekwa kwa sheria ambayo itawalazimisha wafugaji kufuga kisasa na pia akaomba ujenzi wa majosho ya mifugo.
Mbunge wa Viti Maalumu, Mamelok Sokoine (CCM), alikuwa na ushauri kwa Serikali kwamba iongeze uwekezaji katika sekta hizo, itenge matumizi bora ya ardhi, iweke doria katika bahari kuu na kuanzisha bandari ya uvuvi.
Naye Mbunge wa Kishapu, Suleiman Nchambi (CCM), alisema mifugo ni dhahabu inayotembea, hivyo akasisitiza uwekezaji pamoja na elimu kwa wafugaji na wakulima ili kuepusha migogoro kati ya makundi hayo mawili.
Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP), pia alisisitiza suala la elimu kwa makundi hayo mawili, lakini pia akaiomba Serikali ihalalishe wafugaji watumie maeneo ya ranchi kulisha mifugo yao badala ya sasa kufanya hivyo kinyemela.
"Wafugaji si masikini kama baadhi ya watu wanavyotaka jamii iamini hivyo. Tunachohitaji ni kuwaelimisha," alisema Cheyo huku akibainisha kuwa Operesheni Tokomeza ilikuwa mbaya na kuwa suala la kuua mifugo ni lazima likomeshwe.
Kwa upande wake, Mbunge wa Kigoma Mjini, Peter Serukamba (CCM), alisema hivi sasa kila mtu anazungumzia masuala la gesi, lakini akabainisha kuwa hata kama gesi itaanza kuzalishwa nchini, haitakuwa muarobaini wa matatizo bali kinachotakiwa ni kubadili namna ya kufikiri kuhusu rasilimali zetu.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu, Stephen Wassira, alisema uwekezaji kupitia Benki ya Kilimo inayoanza karibuni, utakuwa mkombozi kwa sekta hiyo, huku akisisitiza kupima ardhi, kukopa na kuwezesha kama njia ya kuzisaidia sekta hizo.
Mbunge wa Mji Mkongwe, Muhammad Sanya (CUF), licha ya kulia na bajeti ndogo kwa sekta hizo, aliitaka Serikali kwenda kusaka masoko ya kondoo Saudi Arabia na Falme za Kiarabu, huku akiahidi kugharamia tiketi na malazi kwa Waziri kama atashindwa kupata fedha za kwenda huko.
"Nendeni Saudi Arabia, kuna soko kubwa la kondoo. Wakati wa hija wanachinja kondoo wengi. Tulitumie hili kiuchumi. Kondoo wao wanatoa Brazil, mbali kabisa, wakati sisi tuko nao karibu na pia tunao uhusiano mzuri. Niko tayari kutoa tiketi ya ndege na malazi kwa Waziri kwenda huko," alisema.
Wabunge wengine, Michael Laizer (Longido - CCM), Rose Kamili (Viti Maalum - Chadema), Innocent Kalogeries (Morogoro Vijijini - CCM) na Aeshi Hilary (Sumbawanga Mjini - CCM), pia walisisitiza uwekezaji, kutengewa kwa maeneo ya wakulima na wafugaji na elimu.
Bunge lilitarajiwa kupitisha makadirio hayo jana jioni na leo itakuwa zamu ya Wizara ya Kazi na Ajira, kabla ya Bunge hili la Bajeti kuendelea tena Jumatatu.

No comments: