Wabunge wanaodaiwa kumkashifu Baba wa
Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere wakati wa Bunge Maalumu la Katiba,
wamempigia simu Mama Maria Nyerere kumuomba msamaha, kutokana na maneno ya
kashfa ndani ya bunge hilo.
Hayo yamethibitishwa jana na Mama Maria
Nyerere wakati akizungumza na Jumuiya ya
Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) na wazalendo wa Tanzania,
waliojitokeza kwa wingi kwenda nyumbani kwa mjane huyo wa Baba wa Taifa,
Msasani jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, Mama Maria alisema kuwa
hakuweza kumtambua mmoja wa wabunge hao, waliopiga simu, kutokana na yeye
kutojua nani aliyemkashifu Baba wa Taifa, kwa kuwa hakuwa akifuatilia mjadala
wa bunge hilo.
"Siku moja nilipigiwa simu naombwa
msamaha, lakini mimi nikasema ngoja niwaulize wenzangu, waliokuwa wakifuatilia
kujua ni nani alimkashifu," alisema Mama maria.
Alisema kwa sasa tayari nchi imeshakuwa
na matabaka na ikiwa hakutakuwa na umakini, nchi inaweza ikaingia katika vita
ya wenyewe kwa wenyewe, jambo ambalo ni hatari sana.
Alisema kuwa ikiwa wataendelea
kuwakashifu wazee wa taifa hili, nchi haitaweza kufika mbali kutokana na kauli
wanazozungumza kuwa ni zenye chuki.
"Nawaambia hata mkizunguka nchi
nzima, endeleeni tu, lakini tukirudi nyuma hali ya nchi siyo nzuri na
tunapokwenda siyo kuzuri, kiroho nchi imetawaliwa na ibilisi," alisema.
Alisema kinachoonekana kwa sasa nchi ina
maadui ndani na nje ya nchi na kwamba silaha pekee ya kupambana nao ni sala,
hivyo watu wote kwa ujumla waiombee mema Tanzania.
"Vita inaweza kutokea kwa sababu
kila mtu amejiandaa kwa lolote, tukikalia haya tutaumia," alisema.
Akisoma ujumbe wa vijana wenzake,
Mwenyekiti wa Vijana Mkoa wa Pwani, Mohammed Nyundo alisema kumekuwepo na
kampeni yenye nia ovu, iliyoasisiwa hivi karibuni, yenye kuharibu taswira na
heshima ya Baba wa Taifa katika jamii na kimataifa.
"Kampeni hiyo inaendeshwa na
vibaraka wa nchi za Magharibi na Ulaya, wazandiki na maadui wa amani ya
Tanzania, imeendelea kusambazwa kwa kasi na gharama kubwa," alisema
Nyundo.
Alisema kutokana na kuwepo kwa kampeni
hiyo chafu, jumuiko hilo la vijana wa UVCCM na wazalendo, wameamua kutoa tamko
la kulaani na kupinga kwa nguvu zote vitendo vya baadhi ya watu kumtuhumu,
kumkebehi na kumtukana Mwalimu Nyerere.
Aidha, alisema kwa masikitiko makubwa,
wameshitushwa na kufadhaishwa kwa kuona chombo kikubwa na taasisi muhimu,
ambayo ni mhimili wa serikali kama Bunge, linakuwa uwanja wa matusi ya
kumtukana mwasisi wa taifa.
"Imefikia wakati sasa kwa Bunge
tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kudhibiti na kuondoa kinga yake kwa
wale wote, ambao kwa ujinga na kutumika, wameamua kuanzisha na kuendesha
kampeni kabambe ya kutia doa taswira na heshima ya Baba wa Taifa,"
alisema.
Vijana hao zaidi ya 100 walikwenda
kumuona Mama Maria ili kufikisha ujumbe wao wa kutaka amani na umoja wa Taifa,
viendelee kulindwa. Vijana hao ni kutoka mikoa ya Dar es Salaam, Katavi, Unguja
Kusini, Unguja Kaskazini na Mwanga mkoani Kilimanjaro.
Vijana hao walisema baada ya kumuona
Mama Maria, watakwenda Tanzania Visiwani kwa ajili ya kwenda kumuona Mama Fatma
Karume, ambaye ni Mke wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Hayati Sheikh Abeid Amaan
Karume.
Wakati wa Bunge Maalumu la Katiba
likiendelea kati ya Februari 18 na Aprili 25 mwaka huu lilipoahirishwa hadi
Agosti 5, mwaka huu ili kupisha Bunge la Bajeti, vyombo mbalimbali viliandika
kwa kudai kuwa miongoni mwa wabunge hao ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu
Lissu alimtukana Baba wa Taifa.
Lissu, jana hakupatikana kuzungumzia
hilo, kwani kila alipopigiwa kupitia simu yake ya kiganjani, ilikutwa inakatwa
badala ya kupokelewa.
No comments:
Post a Comment