Kampuni
kinara ya mtandao wa huduma za mawasiliano ya simu za mkononi nchini Vodacom na
Benki ya Biashara Afrika (CBA), jana walizindua huduma mpya yenye kuleta
mapinduzi makubwa ya M-Pawa itakayowawezesha mamilioni ya watanzania kuhifadhi
fedha na kukopa kupitia simu zao za mkononi.
Uzinduzi
wa huduma hiyo ulifanyika jana Dar es Salaam, mgeni rasmi akiwa Rais Jakaya
Kikwete ambaye wakati anazindua, alisema; "Uzinduzi wa kihistoria wa
M-Pawa kwa kiasi kikubwa ni uthibitisho wa mafanikio yaliyotokana na mageuzi
yaliyofanyika kwenye sekta ya fedha nchini ambayo yamechangiwa pamoja na mambo
mengine uwekezaji mkubwa katika sekta ya mawasiliano na hivyo kuwawezesha
wananchi kumudu kuzifikia huduma za fedha."
Naye
Mkurugenzi Mkuu wa Vodacom Tanzania, Rene Meza alisema; "M-Pawa ni ubunifu
mpya katika sekta ya huduma za fedha ambao unaleta pamoja uzoefu wa zaidi ya
miaka 50 wa benki ya CBA katika Afrika Mashariki na mafanikio makubwa ya
mtandao mpana wa huduma ya M-Pesa wenye mawakala zaidi ya 65,000 nchi nzima.
“Huduma
hii itaimarisha zaidi uletaji pamoja wa huduma za kifedha kwa kuwezesha
wananchi kuweka akiba ya hadi Shilingi moja, na kukopa kadiri mteja anavyokidhi
vigezo."
Aliongeza
kuwa, "M-Pawa ni rahisi kutumia, mteja haitaji kutuma wala kujaza fomu za
maombi. Kila mmoja sasa anaweza kufungua akaunti ya benki kwenye benki ya CBA
kwa urahisi zaidi kiasi tu cha kuchagua M-Pawa kutoka simu yake ya mkononi
katika menu ya huduma ya M-Pesa. Zaidi, haina gharama zozote wala ukomo wa
kutoa ama kuhamisha fedha kutoka M-Pesa kwenda M-Pawa na kinyume chake."
Kwa
upande wa Mwenyekiti wa Bodi wa CBA Tanzania, Ndewirwa Kitomari, alisema:
"M-pesa ilikuwa ni mbia sahihi kwetu kuifikisha huduma hii Tanzania
tukiamini kuwa kupitia mtandao wake mpana na mfumo imara wa mawakala zaidi ya 65,000 waliosambaa nchi
kote, huduma hii itapokelewa na kukua kwa kasi hapa nchini."
Vodacom
na CBA wanalenga kuwafikia mamilioni zaidi ya watanzania walio nje ya mfumo
rasmi wa huduma za kibenki nchini mbali na wateja milioni 5 ambao tayari kwa
sasa wanatumia huduma ya M-pesa.
Mbali
na ubia na CBA, M-pesa pia ina ubia wa kibiashara na benki zaidi ya 21 nchini
inayowapa uwezo wateja wake kuweka ama kutoa fedha wakati wowote mahali popote
kwa urahisi zaidi katika akaunti walizonazo kwenye benki hizo.
No comments:
Post a Comment