Viongozi wa dini
kutoka mikoa ya Mtwara na Lindi, waliopata fursa ya ziara ya kujifunza sekta ya
gesi na mafanikio yake nchini Thailand, wamerudi na ushuhuda kwamba neema ya gesi inawezekana.
Wakizungumza
jana asubuhi walipowasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere
(JNIA) kutoka katika ziara hiyo ya masomo, viongozi hao walisema mafanikio ya
uchumi wa gesi, yatapatikana ikiwa
Watanzania watashirikiana na serikali, kuhakikisha wanafikia uchumi wa gesi
asilia.
Katika
kushirikiana huko, viongozi hao wamewataka wananchi kuepuka migogoro isiyo na
tija huku wakitumia wakati uliopo vizuri kujiandaa na uchumi huo.
Wameeleza kuwa licha ya kuwa gesi
itachukua muda mrefu kuanza uzalishaji, ni vema Watanzania wajipe muda bila
kuwa waoga kukopa, kujifunza pamoja na kuhamasisha wanafunzi kusoma masomo ya
sayansi pamoja na kujiunga na vyuo vya ufundi.
Makamu wa Askofu wa Kanisa la
Anglikana, ambaye ni Askofu wa Kanisa hilo Dayosisi ya Newala, Mtwara, Oscar
Mnung’a alisema ni lazima wananchi wakubali kupokea uchumi huo mpya kwa
kujifunza, na kujiandaa kukopa ili kuwekeza katika uchumi huo.
“Ili tufikie malengo, tujifunze
na tusikubali migogoro isiyo na tija huku tukishirikiana na Serikali kwa kila
mmoja kuwa na bidii na juhudi kwani katika nchi hiyo (Thailand), hawana
rasilimali kama zilivyo nchini lakini wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa,” alisema Askofu
Mnung’a.
Askofu Mnung’a alitaka wananchi
washirikiane na Serikali katika kutunga sera zitakazosaidia kuwezesha wageni
wakati wa maandalizi, ili washiriki
kusaidia nchi kufikia malengo hayo na baadaye uchumi ushikiliwe na
wazawa kama walivyofanya wananchi wa Thailand.
Mhadhiri Mkuu wa Chuo Kikuu cha
Stella Maris, Padri Dk Aidan Msafiri, alisema wakiwa nchini humo wamejifunza
kuwa kufikia uchumi wa gesi inachukua muda mrefu, na ni lazima gesi isafirishwe
kwa kutumia mabomba jambo lililosaidia nchi ya Thailand asilimia 98 kuwa na nishati ya umeme.
Shekhe wa Mkoa wa Mtwara, Nurdin
Mangochi, alisema wananchi wanatakiwa
kuelimishwa na kupata muda wa kujiandaa kwa kutumia vizuri rasilimali
watu na ardhi.
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya
Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), Mohamed Sinani, alisema jambo kuu
lililofanikisha Thailand kupata neema ya
gesi, ni kuwekeza zaidi katika amani pamoja na kupanga mipango ya maendeleo na
kuitekeleza.
Alisema baada ya kupata gesi,
hawakubweteka bali walipanga mikakati ya kuongeza viwanda na kuzalisha zaidi
pamoja na kuendelea na utafiti mbalimbali uliowasaidia kutumia upepo na vyanzo
vingine kuzalisha umeme.
Naye Kiongozi wa Serikali katika
msafara huo, Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi, Abdallah Ulega, alisema
wanatarajia viongozi wa dini kuwaeleza waumini wao kuwa gesi duniani kote husafirishwa kwa kutumia
mabomba, husaidia kukopa fedha na kushirikisha nchi nyingine katika kupata
utaalamu.
Alisema wamejifunza kuwa awali
Thailand walitumia wataalamu wa kigeni kutoka Ufilipino na baadaye sera yao
ililazimisha wenyeji washirikishwe, baada ya kujifunza utaalamu baada ya
kusisitiza kujifunza masomo ya sayansi pamoja na vijana wengi kujiunga na chuo
cha ufundi.
Ulega alisema ikiwa hayo
yatafanikiwa Tanzania, mafanikio yatapatikana mapema kuliko ilivyokuwa kwa Thailand, kwani walianza kuona mafanikio
baada ya miaka 40 tangu wagundue gesi, wakati Tanzania ugunduzi wa gesi ulikuwa
2006, lakini mafanikio tayari yameanza kuonekana, ikiwemo matumizi ya magari
kwa gesi na mengineyo.
No comments:
Post a Comment