Serikali inatarajia kutumia Sh bilioni 1.2 kwa ajili ya utekelezaji
wa mradi wa umeme katika vijiji 12
vilivyopo mkoani Mbeya.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini,
Charles Kitwanga aliliambia bunge jana wakati akijibu swali la Mbunge wa Mbeya
Mjini, Joseph Mbilinyi (Chadema).
Mbunge huyo alitaka kujua ni lini serikali itapeleka umeme katika Kata
za Iduda, Isyesye, Itende, Tembela, Mwansanga, Mwansekwa na Iziwa vilivyopo
Jijini Mbeya, ambapo wananchi walishaweka waya kwenye nyumba zao kwa zaidi ya
miaka minane.
Akijibu swali hilo, Kitwanga alisema
miradi ya kupeleka umeme kata ya Iduda, Mwansekwa na Iziwa imejumuishwa katika
miradi ya Shirika la Umeme nchini (Tanesco) ya kupeleka umeme katika maeneo ya
Iduda, Igawilo, Itagha, Hasanga, Iwambala, Itanji, Utukuyu, Mwasenga, Itengano
na Iziwa.
Alisema miradi hiyo itajumuisha ujenzi
wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 16.5, ujenzi
wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 11 yenye urefu wa kilomita 13, ujenzi wa
njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 26.
Pia, alisema fedha hizo zitatumika kwa
ajili ya kufunga transfoma tano na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,335.
No comments:
Post a Comment