Shirika
la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), limetenga dola za Marekani milioni 22
kwa ajili ya kuunga mkono utoaji elimu kwenye uchaguzi mkuu ujao nchini.
Kiongozi
wa shirika hilo, Helen Clark aliuambia Umoja wa Wanawake Wabunge jana mjini
hapa kwamba fedha hizo zitatolewa chini ya Mradi wa Uchaguzi unaoendeshwa na
shirika lake.
Alisema
shirika lake limepokea maombi kutoka vyama vya siasa kuomba kuungwa mkono
hususani kwenye suala la elimu, kujenga uwezo na uhamasishaji katika shughuli
za uchaguzi mkuu ujao.
Alisema
fedha hizo zitajikita katika kuelimisha na kuhamasisha wanawake na vijana
kujihusisha kwenye mchakato wa uchaguzi huo hususani kugombea nafasi za
uongozi.
Kiongozi
huyo wa UNDP alipongeza Tanzania kwa hatua iliyofikia katika kutekeleza malengo
ya maendeleo ya millennia; hasa malengo namba moja, sita na saba.
Alisema
pia Tanzania imekuwa ikifanya vizuri katika juhudi za kutokomeza umasikini,
kuimarisha afya kwa watoto na kuwezesha watoto kuendelea na masomo hadi
sekondari.
Juhudi
nyingine ambazo kiongozi huyo amepongeza Tanzania, ni kupunguza vifo kwa
wajawazito na mapambano dhidi ya Ukimwi.
Kiongozi
huyo ambaye anashika nafasi ya tatu kicheo katika Umoja wa Mataifa, baada ya
Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu, aliendelea kupongeza juhudi zinazofanywa na
serikali katika kuwezesha wanawake kisiasa na kwenye utawala.
Alisema
uwepo wa viti maalumu umewezesha idadi kubwa ya wanawake kuingia kwenye bunge
ambalo ni chombo muhimu cha kutunga sheria.
Wakati
huo huo, akiwa ameongozana na Mwakilishi wa UNDP nchini, Philippe Poinsot,
kiongozi huyo mkuu wa shirika pia alisifu juhudi za serikali katika kukabili
ujangili.
Kwa
upande wake, Mwenyekiti wa Umoja wa Wabunge Wanawake, Anna Abdallah aliambia
ujumbe huo kwamba wakiungwa mkono na wadau wengine, wamekuwa wakifanya
uhamasishaji wa wanawake kuingia kwenye
siasa.
“Tunahamasisha
wanawake na kuwajengea uwezo wa kushiriki katika mchakato wa uchaguzi kwa
kugombea nafasi mbalimbali,” alisema.
Aidha,
Clark ambaye amewahi kuwa Waziri Mkuu wa New Zealand kwa muda mrefu kabla
ya kuingia UNDP, alifanya mazungumzo na Spika Anne Makinda kabla ya kurejea
jijini Dar es Salaam jana.
No comments:
Post a Comment