BAJETI YA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA


HOTUBA YA WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA
MHE. Dkt. HUSSEIN ALI MWINYI (MB) AKIWASILISHA BUNGENI
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI
YA FEDHA KWA MWAKA  2014/15

UTANGULIZI

1.    Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Ulinzi na Usalama, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kujadili na kupitisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2014/15.

2.    Mheshimiwa Spika, kabla ya kuwasilisha hoja yangu, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, aliyenijalia kuwa na uzima na afya njema na kuniwezesha kuwasilisha hotuba yangu ya bajeti kwa mwaka 2014/15. Aidha, namshukuru kwa dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, wa majeshi shupavu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa kuniteua kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mara ya pili. Ahadi yangu kwake  Mheshimiwa Rais, kwenu Waheshimiwa Wabunge na kwa Watanzania wenzangu, hususan wenye mapenzi mema na nchi yetu, yenye amani, utulivu, upendo na mshikamano ni  kwamba, nitatumia uwezo na nguvu zangu zote kutekeleza majukumu mazito na nyeti mliyonikabidhi kwa umakini mkubwa, uaminifu na uadilifu wa hali ya juu.

3.    Mheshimiwa Spika, napenda pia kuwashukuru Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal na Waziri Mkuu Mhe. Mizengo Peter Kayanza Pinda (Mb) kwa miongozo, ushauri na ushirikiano mkubwa wanaonipatia katika kutekeleza majukumu ya Wizara yangu.  Vilevile, nakushukuru wewe Mheshimiwa Spika na Kamati yako Tukufu ya Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Ulinzi na Usalama chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Anna Margareth Abdallah (Mb), kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kutoa ushauri, maelekezo na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za   Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

4.    Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nachukua fursa hii kuwashukuru wajumbe wa Kamati yako ya Ulinzi na Usalama kwa kutenga muda wao adhimu kwenda kuwatembelea wanajeshi wetu wanaotekeleza jukumu zito la kimataifa la Ulinzi wa Amani huko Darfur nchini Sudan. Naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa ziara yao hiyo ilileta hamasa na kuongeza ari kubwa kwa wapiganaji  wetu katika utendaji wao wa kazi.  Ni matumaini yangu kuwa Kamati itaendelea kufanya ziara kama hiyo katika vikosi vyetu vingine vilivyopo nje ya nchi ikiwemo Force Intervention Brigade (FIB) iliyopo  huko Mashariki mwa Kongo. Aidha, namshukuru mtangulizi wangu, Mhe. Shamsi Vuai Nahodha (Mb), kwa kazi nzuri aliyoifanya katika kipindi chake cha uongozi wa Wizara.

5.    Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/14 Wabunge wenzetu waliaga dunia. Wabunge hao ni Mheshimiwa Dkt. William Augustao Mgimwa aliyekuwa Mbunge wa Kalenga na Waziri wa Fedha na Mheshimiwa Said Ramadhan Bwanamdogo aliyekuwa Mbunge wa Chalinze. Napenda kuungana na wenzangu walionitangulia kutoa pole za dhati kwako Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, ndugu, marafiki na Watanzania wote kwa ujumla kwa kuondokewa na wapendwa hao. Namuomba Mwenyezi Mungu azilaze roho za Marehemu Peponi. Amina.

DIRA, DHIMA, MALENGO NA MAJUKUMU YA WIZARA YA ULINZI NA JKT

6.    Mheshimiwa Spika, Dira ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa inaendelea kuwa ile ile ya kuwa Taasisi iliyotukuka ya kudumisha amani na usalama wa Taifa. Vivyo hivyo, Dhima ya Wizara hii bado ni kulinda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhidi ya adui wa aina yoyote kutoka ndani au nje ya nchi na kuhakikisha kuwa mamlaka ya nchi (national sovereignty)  na maslahi ya Taifa letu (national interests) yako salama.

7.    Mheshimiwa Spika, ili kufikia Dhima yake, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ina malengo yafuatayo: -

                      i.           Kuwa na Jeshi dogo la Ulinzi wa nchi lenye taaluma, zana na vifaa vya kisasa.  

                    ii.           Kujenga na kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi na makazi.

                   iii.           Kuendeleza utafiti na uhawilishaji wa teknolojia ya kijeshi katika mashirika ya Mzinga na Nyumbu.

                   iv.           Kujenga uzalendo, ukakamavu, maadili mema na utaifa kwa vijana wa kitanzania.

                     v.           Kuimarisha jeshi la akiba.

                   vi.           Kuimarisha mawasiliano salama jeshini.

                  vii.           Kuimarisha umiliki wa ardhi kwa ajili ya matumizi ya jeshi.

                 viii.           Kudumisha amani na usalama kwa kushirikiana na nchi nyingine duniani.

8.    Mheshimiwa Spika, ili kufikiwa kwa malengo yaliyoainishwa, Wizara imekusudia kutekeleza majukumu yafuatayo:-

                      i.        Kuandikisha wanajeshi wa kutosha wenye sifa zinazohitajika kwa ajili ya ulinzi wa Taifa na kuwapatia mafunzo na mazoezi ya kinadharia na kivitendo.
                    ii.        Kuwapatia wanajeshi makazi, zana, vifaa na vitendea kazi bora na vya kisasa.
                   iii.        Kusimamia matunzo na matumizi mazuri ya zana, vifaa na vitendea kazi.
                   iv.        Kuimarisha mafunzo na mazoezi ya kijeshi na kuendesha mafunzo ya ulinzi wa mgambo.
                     v.        Kuendeleza mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa Sheria na ya kujitolea ili kuwaandaa kwa ukamilifu vijana wa Kitanzania na kuwajengea moyo wa uzalendo na mshikamano wa kitaifa katika kutekeleza shughuli za kujitegemea.
                   vi.        Kuendeleza utafiti na  uhawilishaji wa teknolojia za kijeshi na kuzalisha mali kupitia mashirika ya Mzinga na Nyumbu.
                  vii.        Kuliwezesha Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) liweze kuzalisha kwa tija na faida itakayochangia katika uendeshaji wa shughuli za Jeshi la Kujenga Taifa.
                 viii.        Kushirikiana na Mamlaka za kiraia katika kukabiliana na majanga ili kuwapatia wahanga misaada ya kibinadamu.
                   ix.        Kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi na
                     x.        Kuimarisha ushirikiano na nchi nyingine duniani katika masuala ya kijeshi

UTEKELEZAJI WA MAONI NA USHAURI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA YA ULINZI NA USALAMA

9.     Mheshimiwa Spika, wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na Usalama ilipokaa na kujadili Makadirio ya Mapato, Mpango na Bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka 2013/14 ilitoa maoni, ushauri na maelekezo kadhaa kwa Wizara hii yaliyolenga kuboresha utendaji wa majukumu yake. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa maoni, ushauri na maelekezo yaliyotolewa yamefanyiwa kazi na majibu yake yameainishwa katika Kiambatanisho Namba 1. Aidha, hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wa mjadala huo pia zimezingatiwa katika mpango na bajeti ya mwaka 2014/15 ninayowasilisha leo hapa Bungeni.


HALI YA USALAMA WA MIPAKA MWAKA 2013/14


10.       Mheshimiwa Spika, hali ya usalama wa mipaka ya nchi yetu (nchi kavu, maji na anga) kwa mwaka 2013/14 ilikuwa shwari kwa ujumla. Licha ya kuwepo kwa matishio na mashambulizi ya kigaidi katika eneo la Afrika Mashariki, hakukujitokeza tukio lolote la uharamia kwa upande wa bahari yetu. Hata hivyo, vitendo vya usafirishaji wa madawa ya kulevya na biashara haramu ya usafirishaji binadamu vilijitokeza. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na vyombo vingine vya Usalama  vimeendelea kushirikiana katika kukabiliana na hali hiyo. Kwa upande wa mipaka, matukio ya uharibifu wa alama za mipaka na ujenzi holela unaofanywa na wananchi wanaoishi maeneo ya mipakani hususan maeneo ya Namanga, Jasini, Tunduma na Mtukula yameendelea kujitokeza. Hata hivyo, vikao vya wataalamu kutoka Serikali za Tanzania na nchi jirani za Kenya, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Zambia vyenye lengo la kutatua matatizo hayo vimeanza.  Kufuatia vikao hivyo, alama nane za mpaka (umbali wa km 14.8) zilizokuwa zimeharibiwa katika Wilaya za Tarime (Tanzania) na Kurya (Kenya) zimeimarishwa, ambapo alama saba zimejengwa upya na moja imekarabatiwa. Aidha, alama mpya sabini zimejengwa katikati ya beacons za zamani ili kufanya mpaka huo uonekane kwa urahisi. Mazungumzo kuhusiana na utata wa mpaka wa Tanzania na Malawi katika  ziwa Nyasa yanaendelea chini ya uratibu wa Wizara ya Mambo ya  Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Pamoja na hali hiyo, hakuna uhasama wowote wa kijeshi uliojitokeza baina ya nchi zetu.


MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA MWAKA 2013/14

11.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/14 Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ilikadiria kukusanya mapato ya jumla ya shilingi 68,206,000.00 kutoka katika Mafungu yake matatu ya 38-NGOME, 39-JKT na 57-Wizara. Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Mafungu hayo yalikusanya mapato ya jumla ya shilingi 43,317,624.00 sawa na asilimia 63.5 ya makadirio.

12.       Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2013/14, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iliidhinishiwa jumla ya shilingi 1,102,999,529,000.00 kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Maendeleo katika Mafungu yake matatu. Kati ya fedha hizo, shilingi 857,417,502,000.00 zilitengwa kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi 245,582,027,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo. Hadi kufikia mwezi Machi 2014, Wizara ilikuwa imepokea jumla ya shilingi 768,496,687,343.00 (sawa na asilimia 69.7) ya bajeti yake. Kati ya fedha hizo shilingi 719,118,556,008.00 zilikuwa ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida (sawa na asilimia 83.8) ya fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya matumizi hayo. Kwa upande wa Matumizi ya Maendeleo, fedha zilizopokelewa ni shilingi 49,378,131,335.00 (sawa na asilimia 20.1) ya fedha zote zilizoidhinishwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo. Mchanganuo wa Matumizi ya Kawaida na Maendeleo kwa Mafungu yote matatu ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa hadi mwezi Machi, 2014 umeonyeshwa katika Kiambatanisho Namba 2.

13.       Mheshimiwa Spika, tathmini ya fedha zilizopokelewa inaonesha kwamba mwenendo wa upatikanaji wa fedha kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida katika kipindi hicho kiujumla ulikuwa ni wa kuridhisha.  Fedha kwa ajili ya mishahara na marupurupu zilipokelewa kulingana na makisio ya bajeti. Hata hivyo, fedha zilizotolewa kwa ajili ya shughuli  za Maendeleo hadi kufikia mwezi Machi, 2014 zilikuwa kidogo ukilinganisha na mahitaji. Hali hii imeathiri utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo. 

Shughuli za Matumizi ya Kawaida

14.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/14 Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ilipanga kutekeleza shughuli mbalimbali ili kufikia malengo niliyoyaeleza hapo awali. Shughuli hizo ni pamoja na za:- kulipa stahili mbalimbali za wanajeshi, watumishi wa Umma na vijana walioko katika mafunzo ya JKT; kusafirisha wastaafu; na kutoa huduma muhimu za chakula, tiba na sare. Wizara pia ilipanga kulipia huduma za umeme, maji, simu na mafuta kwa ajili ya uendeshaji wa majukumu ya ulinzi zikiwemo za mafunzo ya kijeshi, mafunzo ya ulinzi wa mgambo na kutengeneza vifaa na zana za kijeshi.



Mafunzo na Mazoezi ya Kijeshi

15.       Mheshimiwa Spika, uimara wa jeshi lolote duniani unategemea mafunzo pamoja na mazoezi ya mara kwa mara. Katika mwaka 2013/14 jeshi letu lilipata fursa ya kushiriki mazoezi mbalimbali ya pamoja na nchi marafiki. Miongoni mwa mazoezi hayo ni zoezi la Kituo cha Uamrishaji (Command Post Exercise - CPX). Zoezi hilo la uamrishaji lilikuwa ni sehemu ya maandalizi ya zoezi la medani  litakalohusisha Majeshi ya Nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Zoezi hilo lijulikanalo kwa jina la USHIRIKIANO IMARA 14 (Field Tactical Exercise - FTX), litafanyika katika jimbo la Mwaro nchini Burundi tarehe 13 – 26 Oktoba, 2014.  Aidha, kupitia Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), Jeshi letu limeshiriki katika mazoezi ya:- “EX WILWETSCHIA” lililofanyika mwezi Septemba, 2013 nchini Namibia; “EX BLUE ZAMBEZI” lililofanyika nchini Angola mwezi Oktoba, 2013; na “EX CUTLASS EXPRESS” lililofanyika mwezi Novemba, 2013 nchini Seychelles.  Jeshi  linategemea pia kushiriki katika zoezi linaloandaliwa na Umoja wa Afrika (AU). Zoezi hilo lijulikanalo kwa jina la Amani Afrika II FTX litafanyika nchini Lesotho mwezi Oktoba/Novemba 2014. Mazoezi ya namna hii siyo tu yameimarisha jeshi letu kimedani, bali pia yamekuwa chachu kubwa ya kuboresha mahusiano na majeshi mengine.

(i)            Mafunzo ya Ulinzi wa Mgambo

16.       Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea kuweka umuhimu katika mafunzo ya mgambo. Katika kipindi hiki Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa kushirikiana na vyombo vya Usalama limeendesha mafunzo katika ngazi mbalimbali kwa wananchi 13,484 (Wanaume 12,337 na wanawake 1,147) ikiwa ni ongezeko la asilimia 14.8 ikilinganishwa na mwaka 2013. Natoa wito kwa Viongozi wa Wilaya na Mikoa kuongeza kasi ya usimamizi na ushiriki wa mafunzo hayo na kutoa huduma stahiki za usafiri kwa wakufunzi wetu, hifadhi ya silaha na maeneo ya mafunzo. Matarajio ya baadaye ya Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania ni kuanzisha rasmi Kamandi ya Jeshi la Akiba.

(ii)  Huduma za Afya na Tiba

17.       Mheshimiwa Spika, pamoja na majukumu ya kiulinzi, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea kutoa huduma za tiba kwa maafisa, askari, watumishi wa Umma, familia za wanajeshi na wananchi kwa ujumla. Huduma hizo zimezidi kuimarika baada ya kuboresha hospitali za JWTZ zilizoko Mwanza, Mbeya, Bububu (Unguja), Tabora, Nyumbu (Pwani) na Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli (Arusha).  Lengo letu ni kuboresha huduma hiyo pia katika ngazi ya vituo vya afya vikosini. Ningependa Bunge lako Tukufu litambue kwamba asilimia 80 ya wagonjwa wanaohudumiwa na hospitali na vituo vyetu ni wananchi wanaoishi maeneo jirani.

(iii)         Ushirikiano wa Kiulinzi na Kijeshi na Nchi Nyingine

18.       Mheshimiwa Spika, ushirikiano kati ya nchi yetu na nchi nyingine katika nyanja za kijeshi ni suala muhimu katika mustakabali wa ulinzi na usalama duniani. Hivyo basi, nchi yetu inaendelea kuimarisha ushirikiano wa kijeshi na kiulinzi (Bilateral Cooperation) na nchi mbalimbali zikiwemo: - China, Ujerumani, Marekani, Afrika ya Kusini, India, Umoja wa Falme za Kiarabu, Uingereza, Canada na Urusi. Kupitia ushirikiano huo, Jeshi letu, pamoja na mambo mengine limenufaika katika maeneo yakiwemo ya nyanja za mafunzo ya kijeshi na kitaaluma, zana na vifaa, mazoezi na michezo. Kwa ujumla ushirikiano huu umekuwa ni wa manufaa makubwa.

19.       Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/14, Serikali imeendelea kudumisha ushirikiano katika Jumuiya za kikanda (Regional Cooperation) hususan za Afrika Mashariki (EAC) na Kusini mwa Afrika (SADC). Ushirikiano huo ulijikita katika nyanja za mafunzo, mazoezi na michezo baina ya majeshi ya nchi zetu. Na kama nitakavyoeleza hapo baadaye, Tanzania, tukiwa wanachama wa nchi za SADC tumepeleka nchini DRC kikosi cha ulinzi wa amani kuungana na majeshi ya Umoja wa Mataifa. Aidha, kupitia vyuo vyetu, Jeshi letu limeendelea kutoa nafasi za mafunzo ya kijeshi kwa Majeshi ya nchi za Botswana, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Malawi, Zambia, Namibia, Seychelles, Swaziland na Zimbabwe kupitia:- Chuo cha Taifa cha Ulinzi (National Defence College- NDC); Chuo cha Ukamanda na Unadhimu (Command and Staff College-CSC); na Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (Tanzania Military Academy-TMA).  Vivyo hivyo, Maafisa wetu nao walipata mafunzo katika baadhi ya nchi hizo.

20.       Mheshimiwa Spika, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania limeendelea kushiriki katika Operesheni za Ulinzi wa Amani katika nchi mbalimbali. Hadi sasa, ushiriki wa wanajeshi wetu katika Operesheni hizo ni kama ifuatavyo;

                      i.        Kikosi kimoja (TANZBATT – 8) kipo Darfur nchini Sudan.
                    ii.        Kikosi kimoja (TANZBATT – 1) kipo Mashariki mwa DRC ikiwa ni sehemu ya MONUSCO Force Intervention Brigade.
                   iii.        Kombania mbili za Polisi Jeshi zipo nchini Lebanon.
                   iv.        Waangalizi wa amani (military observers)  na maafisa wanadhimu (staff officers) wapo katika baadhi ya nchi ikiwemo Sudani Kusini. 

(iv)         Mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa Vijana


21.       Mheshimiwa Spika, Jeshi la Kujenga Taifa limeendelea kutoa mafunzo kwa vijana wa kujitolea na wa Mujibu wa Sheria. Malengo ya mafunzo hayo ni pamoja na kujenga uzalendo, ukakamavu, maadili mema, utaifa na kuwapa stadi za maisha vijana wa kitanzania. Katika mwaka 2013/14 JKT linaendesha operesheni moja ya mafunzo ya vijana wa kujitolea ijulikanayo kama Operesheni Miaka Hamsini ya Muungano. Katika operesheni hii idadi ya vijana 8,439 (wavulana 6,610 na wasichana 1,829) wanaendelea na mafunzo yaliyoanza mwezi Machi 2014. Nafurahi kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba hivi sasa vyombo vya Ulinzi na Usalama vimeanza kutekeleza utaratibu wa kuajiri vijana waliopitia mafunzo ya JKT. Idadi ya vijana  7,062 walichukuliwa  na vyombo hivyo kwa mwaka huu. Aidha, vijana 155 walichukuliwa na taasisi na makampuni binafsi (Benki Kuu ya Tanzania-BOT, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania-TAA, Barrick  Gold Mine na Geita Gold Mines).

22.       Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mafunzo ya Mujibu wa Sheria,  na kama ilivyoelezwa mwaka jana, mafunzo hayo yalirejeshwa kwa wahitimu wa kidato cha sita kuanzia mwezi Machi 2013. Mafunzo haya yaliendelea kutolewa ambapo jumla ya vijana 10,505 wameweza kuhitimu mafunzo hayo kipindi hiki. Kati yao, vijana 9,510 walihitimu mafunzo awamu ya pili iliyomalizika mwezi Oktoba, 2013. Ingawa mategemeo yalikuwa kuchukua idadi ya vijana 15,000 wajiunge na mafunzo awamu ya tatu, ni vijana 1,002 waliweza kujiunga na mafunzo hayo yaliyoanza mwezi Oktoba, 2013 hadi Januari 2014, ambapo vijana 995 ndio waliohitimu. Kupatikana kwa idadi ndogo ya vijana wa awamu ya tatu na kutopatikana kabisa kwa vijana awamu ya nne kulitokana na vijana wengi kujiunga na vyuo vya elimu ya juu ambapo muhula wa masomo huanza mwezi Oktoba.

23.       Mheshimiwa Spika, utaratibu wa vijana waliomaliza kidato cha sita kujiunga na JKT kwa mujibu wa sheria si wa hiari. Hivyo kwa mwaka huu Jeshi la Kujenga Taifa litachukua vijana wasiopungua 45,000 watakaomaliza kidato cha sita hivi karibuni.  Awamu ya kwanza kwa mwaka 2014/15 itaanza mwezi Juni hadi Septemba, 2014 na itahusisha vijana 20,000.  Awamu ya pili itakayochukua vijana 14,450  itaanza mwezi Oktoba 2014 hadi Januari 2015.  Na awamu ya tatu itakayochukua vijana 10,550 itaanza mwezi Januari hadi Aprili 2015. Naomba vijana wote wanaotakiwa kujiunga na mafunzo ya JKT watambue kuwa ni kosa kisheria kukaidi wito wa kujiunga na mafunzo hayo.

(v)           Mapambano dhidi ya UKIMWI

24.       Mheshimiwa Spika, UKIMWI umeendelea kuwa janga la kitaifa na kuleta athari kubwa kijamii, kiuchumi na kuathiri nguvu kazi inayotegemewa. Hivyo, jitihada za kupambana na maambukizi ya UKIMWI ni suala endelevu. Kwa msingi huo Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea kutoa elimu ya jinsi ya kujikinga ili kuzuia maambukizi mapya. Aidha, wizara imekuwa ikihimiza upimaji wa hiari kwa maafisa, askari na watumishi wa umma na vijana wa JKT kwa kutumia waelimishaji rika. Kwa wale ambao tayari wameshaambukizwa virusi vya UKIMWI, Wizara imeendelea kutoa huduma ya  lishe na dawa za kupunguza makali ya virusi (ARVs).

Shughuli za Matumizi ya Maendeleo

25.       Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa shughuli za maendeleo hadi kufikia robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2013/14 kwa ujumla haukuwa mzuri. Mafungu yote matatu yalipokea wastani wa asilimia 20.1 ya bajeti iliyoidhinishwa. Kwa mapokezi hayo, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeweza kutekeleza miradi ifuatayo; mradi wa ujenzi wa nyumba 10,000 za makazi ya wanajeshi, kulipia madeni ya kimikataba, kukarabati majengo pamoja na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi na makazi katika makambi na viteule vya JKT, ulipiaji fidia kwa maeneo yaliyotwaliwa na Jeshi, kuboresha mawasiliano jeshini, ujenzi wa Shule ya Mafunzo ya Awali ya Kijeshi Kihangaiko, kulipia ujenzi wa viporo vya miradi ya maji Msangani na Ngerengere na ukarabati wa viteule vya Kasanga, Kalando na Hospitali ya Jeshi Lugalo, kuboresha miundombinu ya Shirika la Nyumbu na ununuzi wa malighafi kwa Shirika la Mzinga.
(i)            Ujenzi wa Nyumba na Makazi ya Wanajeshi

26.       Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2013/14, Wizara yangu ililiarifu Bunge lako Tukufu kwamba, maandalizi ya ujenzi wa nyumba 10,000  kwa ajili ya makazi ya askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania yamekamilika ambapo ujenzi wa nyumba 6,064 za awamu ya kwanza ungeanza. Nafurahi kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa ujenzi wa nyumba hizo unaotekelezwa na Kampuni ya Shanghai Construction (Group) General Company ulianza rasmi tarehe 17 Julai, 2013. Ujenzi huo utakaofanyika katika vikosi 37 vya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na Jeshi la Kujenga Taifa utakuwa katika mikoa tisa kwa mgawanyo ufuatao; Arusha (792), Dar es Salaam (2,288), Dodoma (592), Kagera (144), Morogoro (616), Pemba (320), Pwani (840), Kigoma (160) na Tanga (312). Ujenzi huu utachukua muda wa miezi hamsini (50). Hadi sasa, ujenzi tayari umeanza kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani ambapo hatua ya ujenzi huo imefikia asilimia 80. Maandalizi ya ujenzi katika mikoa ya Arusha, Morogoro, Pemba na Tanga unaotarajiwa kuanza mwezi Juni 2014 yamekamilika.

(ii)          Ununuzi wa Zana na Vifaa vya Kijeshi

27.       Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea na azma yake ya kuimarisha Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa kulipatia zana na vifaa vya kisasa. Katika mwaka 2013/14 Jeshi lilipokea zana na vifaa vya kisasa ambavyo vimeendelea kutumika katika shughuli za ulinzi na mafunzo. Nisingependa kuwachosha Waheshimiwa Wabunge katika eneo hili kwani mwenye macho alijionea mwenyewe yaliyojiri siku ya kilele cha maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2014.  Kwa yule ambaye hakubahatika kuyaona, ni imani yangu kuwa alisimuliwa.  Mpango wa ununuzi wa zana za kisasa na bora ni endelevu, hivyo natarajia Bunge lako Tukufu litaendelea kuidhinisha fedha za kutekeleza mpango huu.

 (iii)     Shirika la Uzalishaji Mali la SUMAJKT


28.       Mheshimiwa Spika, Jeshi la Kujenga Taifa kupitia Shirika lake la Uzalishaji Mali (SUMAJKT) linaendelea kutekeleza majukumu yake kupitia idara zake za uhandisi na ujenzi, viwanda na kilimo, biashara na utalii.  Utekelezaji wa shughuli hizi unalenga katika kuhakikisha kuwa SUMAJKT inafanikisha malengo iliyojiwekea kwa tija na ufanisi mkubwa. Katika kutekeleza azma  ya kujitosheleza kwa chakula, mwaka 2013/14 SUMAJKT lilifanikiwa kulima ekari 4,390 za mazao mbalimbali ya chakula na ekari 1,913 za mbegu bora.  Tatizo linaloendelea kulikabili SUMAJKT katika eneo hili ni kutokulipwa madeni. Hadi sasa jumla ya shilingi 495,792,000.00 hazijalipwa na makampuni yaliyouziwa mbegu hizo. Makampuni hayo ni Agricultural Seed Agency (ASA), Tropical Seed Co. Ltd na Southern Highland Seed Growers Ltd.

29.       Mheshimiwa Spika, SUMAJKT kupitia “National Service Construction Department” inatekeleza miradi  ya ujenzi wa majengo na barabara. Katika kipindi cha mwaka 2013/14 Jeshi la Kujenga Taifa limefanya mageuzi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuboresha ujuzi wa wataalam, kuongeza matumizi ya zana na mitambo pamoja na kuimarisha uwezo wa Idara zake ili kujikita kwenye utekelezaji wa miradi mikubwa ya ujenzi wa majengo na barabara. Miongoni  mwa miradi inayotekelezwa ni ya ujenzi wa Shule ya  Mafunzo ya Awali  (Recruits Training School - RTS) Kihangaiko, ujenzi wa barabara kiwango cha lami wilayani Chato, ujenzi wa barabara za ndani katika mgodi wa Tulawaka na ukarabati wa jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa.

30.       Mheshimiwa Spika, katika eneo la ulinzi wa mali za wananchi, SUMAJKT limejizatiti katika shughuli za ulinzi kupitia kampuni tanzu ya SUMAJKT Guard Ltd. Vijana wanaotoa huduma hii ni wale waliohitimu mafunzo ya JKT ambao sasa wanafikia idadi ya 1,668. Hadi sasa SUMAJKT Guard Ltd wameweza kupata zabuni ya kutoa huduma hiyo ya ulinzi kwa taasisi za Serikali, mashirika ya Umma na binafsi, viwanda na migodi. Katika  mwaka 2014/15 Kampuni hii inatarajia kuajiri vijana 2,000 kuongeza idadi ya nguvu kazi iliyopo na hivyo kupanua utoaji huduma hiyo katika taasisi mbalimbali za umma na binafsi.

31.       Mheshimiwa Spika, kama ilivyoelezwa katika hotuba ya mwaka 2013/14 kuhusiana na mradi wa matrekta, matrekta 1,558 na zana za kilimo zenye thamani ya shilingi 53,675,837,001.00 ziliuzwa kwa mkopo kwa wadau mbalimbali zikiwemo Halmashauri za Wilaya, vikundi vya uzalishaji mali, SACCOS na watu binafsi wakiwemo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge.  Marejesho ya mikopo hii  hadi kufikia Machi, 2014 ni kiasi cha Shilingi 26,162,374,328.96. Baada ya mauzo ya awamu ya kwanza kukamilika, SUMAJKT bado limeendelea kutekeleza mradi wa uagizaji wa matrekta mengine pamoja na zana za kilimo. Hivi sasa yapo matrekta 197 aina ya New Holland na Farmtrac kwenye kituo cha Mwenge. Waheshimiwa Wabunge, Halmashauri za Wilaya, vikundi vya uzalishaji mali, SACCOS na watu binafsi  wenye mkopo mnakumbushwa kurejesha mikopo yenu na mnahamasishwa kuja  kununua matrekta mapya.

(i)            Shughuli za Shirika la Mzinga


32.       Mheshimiwa Spika, shughuli za msingi za Shirika la Mzinga na kampuni yake tanzu ya Mzinga Holdings zimeendelea kwa mafanikio. Uzalishaji wa mazao ya risasi na milipuko umeongezeka ikiwa ni pamoja na kupata masoko mapya ya mazao hayo nje ya nchi. Aidha, katika ukanda wetu wa Afrika Mashariki, Shirika la Mzinga limeteuliwa kuwa Centre of Excellence. Kwa upande wa Mzinga Holdings shughuli zake zimejikita katika ujenzi na ukarabati wa majengo na uendeshaji wa maduka ya kuuza bidhaa zisizolipiwa kodi (Duty Free Shops) kwenye vikosi na makambi ya Jeshi.

(ii)           Shughuli za Shirika la Nyumbu

33.       Mheshimiwa Spika, shughuli za utafiti katika Shirika la Nyumbu hazikuwa na mafanikio makubwa kutokana na kutopatikana kwa fedha za maendeleo. Hivyo tafiti zinazohusiana na mitambo ya kuchuna mkonge, “engine” na “gear box” za matrekta madogo na uzalishaji wa vipuri vya mashine (prototype) na pampu ya umwagiliaji hazikukamilika. Hata hivyo, shughuli za uzalishaji vipuri mbalimbali ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa vipuri vya Shirika la Reli (TRL) hususan “brake blocks” zimeendelea. Aidha, Shirika limeendelea kutoa huduma ya kutengeneza pampu za maji za DAWASCO na pia kuhusika katika ufungaji na ukarabati wa vifaa vinavyotumiwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa ajili ya Ulinzi wa Amani huko Darfur - Sudan, Lebanon na Mashariki mwa DRC. Miongoni mwa vifaa vilivyofanyiwa ukarabati na Nyumbu ni magari ya kubebea mizigo, maji, mafuta na askari. Aidha, uzalishaji na upatikanaji wa “Powered Brick making machine”, mashine za kusaga na kukoboa nafaka unaendelea.

(iii)          Mtandao wa Mawasiliano Jeshini

34.       Mheshimiwa Spika, kazi ya ukarabati na uboreshaji wa mawasiliano jeshini imeendelea kutekelezwa. Awamu ya kwanza ya mradi wa uboreshaji wa mawasiliano ndani ya vikosi imekamilika katika mkoa wa Dar es Salaam. Kazi ya uboreshaji wa mawasilianao ndani ya vikosi vilivyo nje ya Mkoa wa Dar es Salaam haijafanyika kutokana na kutokupatikana kwa fedha za maendeleo. Hivyo utekelezaji wa kazi hiyo pamoja na awamu ya pili ya kuunganisha mfumo wa Satellite utategemeana na upatikanaji wa fedha. Zoezi la kusimika minara ya mawasiliano huru na salama nchi nzima linaendelea.

(iv)          Uvamizi wa Maeneo ya Jeshi, Upimaji na Ulipaji Fidia


35.          Mheshimiwa Spika, tatizo la uvamizi wa maeneo ya Jeshi bado linaendelea kujitokeza. Katika kipindi hiki maeneo yaliyoathirika na tatizo hilo ni pamoja na Tondoroni – Pwani, Tanganyika Packers na Monduli –Arusha, Kimbiji – Dar es Salaam, Chita – Morogoro, Itaka na Uyole – Mbeya, Uwanja wa Ndege na Ilemela – Mwanza na Kisakasaka - Unguja.  Pamoja na hatua zinazochukuliwa zikiwemo za kisheria, nawasihi wananchi wasivamie maeneo ya Jeshi wala kuendesha shughuli za kibinadamu katika maeneo hayo.

36.       Mheshimiwa Spika, kuhusu fidia, katika mwaka 2013/14 Wizara imekamilisha kulipa fidia katika maeneo yafuatayo; Mwakidila (Tanga), Cheyo (Tabora), Mwantini (Shinyanga) na Mataya Kiromo (Pwani).  Mipango yetu ya kulipa fidia katika maeneo mengine yaliyochukuliwa kwa matumizi ya Jeshi inaendelea. Aidha, maeneo tunayoyalenga kulipa fidia katika mwaka 2014/15 ni ya Makambako (Njombe), Ilemela na Kigongo Ferry (Mwanza). Zoezi la kupima na kuweka alama za mipaka, mabango na “buffer zones” linaendelea.

CHANGAMOTO ZA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA MWAKA 2013/14

37.       Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa katika utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2013/14 ni ya Wizara kuidhinishiwa kiwango kidogo cha bajeti ikilinganishwa na mahitaji halisi. Kwa mfano katika mwaka wa fedha 2013/14 wakati mahitaji halisi kwa kuzingatia vipaumbele vya Wizara yalikuwa ni shilingi 1,741,888,249,500.00, bajeti iliyoidhinishwa ilikuwa shilingi 1,102,999,529,000.00 sawa na asilimia 63.3 ya mahitaji. Hali hiyo imepelekea utekelezaji wa shughuli za Wizara hususan shughuli za maendeleo kutofikia malengo yaliyokusudiwa. Baadhi ya shughuli zilizoathirika ni za uboreshaji wa viwanda, utafiti na uzalishaji wa bidhaa za kijeshi, kulipia huduma na mahitaji muhimu kama vile mafuta, maji na umeme. Hali hiyo imesababisha Wizara kulimbikiza madeni makubwa ya kimkataba. Kwa upande wa matumizi ya kawaida, changamoto hii imesababisha ongezeko kubwa la madeni yakiwemo ya wazabuni na ya taasisi zinazotoa huduma muhimu za maji, umeme na simu.

38.       Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine inayoikabili Wizara ni mtiririko wa fedha kutoka Hazina kutozingatia mpango kazi wa Wizara, ambapo fedha zinapoidhinishwa, hutolewa zikiwa pungufu na bila kuzingatia ratiba ya mikataba.  Hali hii imesababisha shughuli za Wizara hususan za maendeleo kutotekelezwa kama ilivyopangwa. Matokeo yake ni kuwa  Wizara imeshindwa kukamilisha ujenzi wa majengo na miundombinu katika makambi, kushindwa kulipa mikopo mbalimbali ukiwemo wa NSSF na kushindwa kulipa malipo ya kimikataba.

MPANGO WA MWAKA 2014/2015
 
39.       Mheshimiwa Spika, mpango wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka 2014/15 umekusudia kuimarisha utendaji kazi na ufanisi wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika kutekeleza majukumu ya Ulinzi wa Taifa kulingana na Dira, Dhima na Malengo ya Wizara. Vilevile, mpango umelenga kuimarisha mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa vijana wa Mujibu wa Sheria na wale wa kujitolea. Aidha, Wizara inakusudia kukamilisha miradi inayoendelea na kulipa madeni ya kimikataba. Hivyo, Wizara  imepanga kutekeleza shughuli zifuatazo:-

i.        Kununua vifaa na zana za kijeshi ikiwemo vifaa vya uhandisi wa medani na ndege vita.
ii.            Kuanza ujenzi wa gati katika Kamandi ya Jeshi la Wanamaji.
iii.           Kuboresha mifumo ya mawasiliano ya ndani na nje ya vikosi na makambi ya Jeshi.
iv.           Kuendelea na ujenzi wa nyumba 6,064 kwa ajili ya makazi ya wanajeshi.
v.             Kukamilisha ujenzi wa Shule ya Mafunzo ya Awali ya Kijeshi (RTS) – Kihangaiko Pwani na Chuo cha Ukamanda na Unadhimu (CSC) – Tengeru Arusha.
vi.           Kuboresha viwanda vya  Mashirika ya Mzinga na Nyumbu.
vii.          Kulipa mkopo wa NSSF wa ujenzi wa nyumba za makazi ya wanajeshi.
viii.         Upimaji na ulipaji wa fidia ya ardhi katika maeneo ya wananchi yaliyochukuliwa kwa ajili ya matumizi ya Jeshi.
ix.           Kuanza ujenzi wa Hospitali Kuu ya Jeshi huko Mataya - Kiromo Pwani.
x.             Ujenzi na umaliziaji wa viporo vya nyumba, bwalo na bweni huko Pemba.
xi.           Ujenzi wa maghala ya kuhifadhia silaha na zana pamoja na kuboresha mawasiliano.
xii.          Kulipia gharama za matumizi ya mahitaji muhimu ya umeme, maji, simu na huduma za uendeshaji wa majukumu ya kimsingi.
xiii.         Kulipia stahili mbalimbali za wanajeshi, vijana wa Jeshi la Kujenga Taifa na Watumishi wa Umma.
xiv.         Kuimarisha ushirikiano na nchi nyingine duniani katika nyanja za kijeshi na ulinzi.
xv.          Kulipa madeni ya  kimkataba.
xvi.         Kuongeza uwezo wa makambi ya JKT kuweza kuchukua idadi kubwa ya vijana kwa wakati mmoja.
xvii.        Kupanua wigo wa makundi ya vijana wa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa Sheria.

SHUKRANI

40.       Mheshimiwa Spika, kabla sijahitimisha hotuba yangu napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru  wafuatao kwa michango yao katika maandalizi ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu:- Katibu Mkuu Bw. Job D. Masima; Naibu Katibu Mkuu Bi. Mwintango Rose Shelukindo; Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Davis A Mwamunyange; Mnadhimu Mkuu Luteni Jenerali Samuel A Ndomba; Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa Meja Jenerali Raphael M Muhuga; Wakuu wa Kamandi za Jeshi la Nchi Kavu Meja Jenerali Salum M Kijuu; Jeshi la Anga Meja Jenerali Joseph F Kapwani na Jeshi la Wanamaji Brigedia Jenerali Rogastian S Laswai; Meneja Mkuu wa Shirika la Mzinga Meja Jenerali Dkt Charles N Muzanila na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumbu Kanali John K Nchimbi.

41.       Mheshimiwa Spika, pia napenda kuwashukuru Wakuu wa Idara na Vitengo (Makao Makuu ya Wizara), Wakuu wa Matawi (NGOME), Wakuu wa Idara (Makao Makuu ya Jeshi la Kujenga Taifa), Maafisa na Askari na Watumishi wa Umma wa Wizara kwa kunipokea na kunipa ushirikiano katika kufanikisha majukumu ya Wizara.  Vile vile, naomba kuwashukuru wapiga kura wangu wa jimbo la Kwahani kwa ushirikiano wao walionipa katika mwaka 2013/14. Ni matumaini yangu kuwa tutaendelea kushirikiana zaidi kwa manufaa ya jimbo letu na Taifa kwa ujumla. Aidha, namshukuru Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na watumishi walio chini yake kwa kuchapisha Hotuba hii kwa wakati.

42.          Mheshimiwa Spika, kwa umuhimu wa pekee na kwa kupitia Bunge lako Tukufu naomba kuwasilisha salamu za pongezi maalum za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa wanajeshi wote kwa kufanikisha maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanzania. Kazi waliyoifanya ni kubwa na waliifanikisha kwa weledi, utii, uhodari, ujasiri na kwa kishindo cha hali ya juu. Ushiriki wao huo umeudhihirishia umma wa Watanzania na ulimwengu kwa ujumla kuwa jeshi letu ni imara, shupavu na lipo tayari kulinda, kutetea na kudumisha Muungano wetu. Nami nikiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa natamka kuwa ‘I am proud of our gallant men and women in uniform’.

43.       Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia na kwa niaba ya wanajeshi wote namshukuru sana Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete. Hiba (legacy) yake ya  uongozi, ushupavu, uvumilivu na maridhiano itakumbukwa na kuenziwa vizazi na vizazi hususan kwetu sisi wanajeshi.   Ahadi yetu kwake ni kuwa tutaendelea kusimama imara, kupokea na kutii amri na maelekezo yake bila hila yoyote na kutoyumbishwa na kauli potovu za kisiasa.

MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA BAJETI YA MWAKA 2014/15

i.              Makadirio ya Mapato

44.          Mheshimiwa Spika, vyanzo vya mapato ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Taasisi zake bado ni vidogo.  Chanzo kikuu  cha mapato kwa Wizara ya Ulinzi na JKT na taasisi zake kimeendelea  kutegemea uuzaji wa nyaraka za zabuni. Hivyo, makadirio ya  Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2014/15 ni kukusanya mapato yenye jumla ya shilingi 60,506,000.00 kwa mchanganuo ufuatao:

Fungu38 – NGOME                     =            2,001,000.00
Fungu 39 – JKT              =          48,503,000.00
Fungu 57 – Wizara                     =          10,002,000.00
Jumla  shilingi           =          60,506,000.00

ii.            Bajeti ya Matumizi ya Kawaida na Maendeleo

45.       Mheshimiwa Spika, ili Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iweze kutekeleza majukumu yake katika mwaka 2014/15 inaomba kuidhinishiwa jumla ya shilingi 1,269,076,056,000.00 ambazo kati yake shilingi 1,020,076,056,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi 249,000,000,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo. Mchanganuo wa bajeti hiyo kwa kuzingatia mafungu ya Wizara ni ufuatao:-





FUNGU 38 NGOME




Matumizi ya Kawaida shilingi
803,542,549,000.00
Matumizi ya Maendeleo shilingi
  12,000,000,000.00
Jumla ya Makadirio kwa Fungu 38 shilingi

815,542,549,000.00


FUNGU 39 JKT

Matumizi ya Kawaida shilingi
196,822,661,000.00
Matumizi ya Maendeleo shilingi    
7,000,000,000.00
Jumla ya Makadirio kwa Fungu 39 shilingi

203,822,661,000.00


FUNGU 57 WIZARA YA ULINZI

Matumizi ya Kawaida  shilingi
19,710,846,000.00
Matumizi ya Maendeleo shilingi
230,000,000,000.00
Jumla ya Makadirio kwa Fungu 57 shilingi

249,710,846,000.00




MWISHO


46.          Mheshimiwa Spika, hotuba hii inapatikana pia katika tovuti ya Wizara (www.modans.go.tz).  Naomba kutoa Hoja.



No comments: