HOTUBA YA WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA
MHE. Dkt. HUSSEIN ALI MWINYI (MB) AKIWASILISHA
BUNGENI
MAKADIRIO
YA MAPATO NA MATUMIZI
YA
FEDHA KWA MWAKA 2014/15
UTANGULIZI
1. Mheshimiwa
Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na Mwenyekiti wa
Kamati ya Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Ulinzi na
Usalama, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kujadili na
kupitisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na
Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2014/15.
2. Mheshimiwa
Spika, kabla
ya kuwasilisha hoja yangu, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu,
mwingi wa rehema, aliyenijalia kuwa na uzima na afya njema na kuniwezesha
kuwasilisha hotuba yangu ya bajeti kwa mwaka 2014/15. Aidha, namshukuru kwa
dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, wa majeshi
shupavu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa
kuniteua kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mara ya pili. Ahadi
yangu kwake Mheshimiwa Rais, kwenu Waheshimiwa
Wabunge na kwa Watanzania wenzangu, hususan wenye mapenzi mema na nchi yetu,
yenye amani, utulivu, upendo na mshikamano ni kwamba, nitatumia uwezo na nguvu zangu zote kutekeleza
majukumu mazito na nyeti mliyonikabidhi kwa umakini mkubwa, uaminifu na
uadilifu wa hali ya juu.
3. Mheshimiwa
Spika, napenda pia kuwashukuru
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal na Waziri Mkuu Mhe. Mizengo Peter Kayanza Pinda (Mb) kwa miongozo, ushauri na
ushirikiano mkubwa wanaonipatia katika kutekeleza majukumu ya Wizara yangu. Vilevile, nakushukuru wewe Mheshimiwa Spika na
Kamati yako Tukufu ya Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania ya Ulinzi na Usalama chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Anna Margareth
Abdallah (Mb), kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kutoa ushauri, maelekezo na
kufuatilia utekelezaji wa shughuli za Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
4.
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nachukua fursa
hii kuwashukuru wajumbe wa Kamati yako ya Ulinzi na Usalama kwa kutenga muda
wao adhimu kwenda kuwatembelea wanajeshi wetu wanaotekeleza jukumu zito la
kimataifa la Ulinzi wa Amani huko Darfur nchini Sudan. Naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa ziara yao
hiyo ilileta hamasa na kuongeza ari kubwa kwa wapiganaji wetu katika utendaji wao wa kazi. Ni matumaini yangu kuwa Kamati itaendelea
kufanya ziara kama hiyo katika vikosi vyetu vingine vilivyopo nje ya nchi
ikiwemo Force Intervention Brigade (FIB) iliyopo huko Mashariki mwa Kongo. Aidha, namshukuru
mtangulizi wangu, Mhe. Shamsi Vuai Nahodha (Mb), kwa kazi nzuri aliyoifanya
katika kipindi chake cha uongozi wa Wizara.
5. Mheshimiwa
Spika, katika
kipindi cha mwaka 2013/14 Wabunge wenzetu waliaga dunia. Wabunge hao ni
Mheshimiwa Dkt. William Augustao Mgimwa aliyekuwa Mbunge wa Kalenga na Waziri
wa Fedha na Mheshimiwa Said Ramadhan Bwanamdogo aliyekuwa Mbunge wa
Chalinze. Napenda kuungana na
wenzangu walionitangulia kutoa pole za dhati kwako Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa
Wabunge, ndugu, marafiki na Watanzania wote kwa ujumla kwa kuondokewa na
wapendwa hao. Namuomba Mwenyezi Mungu azilaze roho za Marehemu Peponi. Amina.
DIRA,
DHIMA, MALENGO NA MAJUKUMU YA WIZARA YA ULINZI NA JKT
6. Mheshimiwa
Spika, Dira ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga
Taifa inaendelea kuwa ile ile ya kuwa Taasisi iliyotukuka ya kudumisha amani na
usalama wa Taifa. Vivyo hivyo, Dhima
ya Wizara hii bado ni kulinda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhidi ya adui wa
aina yoyote kutoka ndani au nje ya nchi na kuhakikisha kuwa mamlaka ya nchi (national
sovereignty) na maslahi ya Taifa letu (national
interests) yako salama.
7.
Mheshimiwa Spika, ili kufikia Dhima yake, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa ina malengo yafuatayo: -
i.
Kuwa
na Jeshi dogo la Ulinzi wa nchi lenye taaluma, zana na vifaa vya kisasa.
ii.
Kujenga
na kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi na makazi.
iii.
Kuendeleza utafiti na uhawilishaji wa teknolojia
ya kijeshi katika mashirika ya Mzinga na Nyumbu.
iv.
Kujenga
uzalendo, ukakamavu, maadili mema na utaifa kwa vijana wa kitanzania.
v.
Kuimarisha
jeshi la akiba.
vi.
Kuimarisha
mawasiliano salama jeshini.
vii.
Kuimarisha
umiliki wa ardhi kwa ajili ya matumizi ya jeshi.
viii.
Kudumisha
amani na usalama kwa kushirikiana na nchi nyingine duniani.
8.
Mheshimiwa Spika, ili kufikiwa
kwa malengo yaliyoainishwa, Wizara imekusudia kutekeleza majukumu yafuatayo:-
i.
Kuandikisha wanajeshi wa kutosha wenye sifa
zinazohitajika kwa ajili ya ulinzi wa Taifa na kuwapatia mafunzo na mazoezi ya
kinadharia na kivitendo.
ii.
Kuwapatia
wanajeshi makazi, zana, vifaa na vitendea kazi bora na vya kisasa.
iii.
Kusimamia matunzo
na matumizi mazuri ya zana, vifaa na vitendea kazi.
iv.
Kuimarisha
mafunzo na mazoezi ya kijeshi na kuendesha mafunzo ya ulinzi wa mgambo.
v.
Kuendeleza
mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa Sheria na ya kujitolea ili kuwaandaa kwa ukamilifu
vijana wa Kitanzania na kuwajengea moyo wa uzalendo na mshikamano wa kitaifa
katika kutekeleza shughuli za kujitegemea.
vi.
Kuendeleza
utafiti na uhawilishaji wa teknolojia za
kijeshi na kuzalisha mali kupitia mashirika ya Mzinga na Nyumbu.
vii.
Kuliwezesha
Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) liweze kuzalisha
kwa tija na faida itakayochangia katika uendeshaji wa shughuli za Jeshi la
Kujenga Taifa.
viii.
Kushirikiana
na Mamlaka za kiraia katika kukabiliana na majanga ili kuwapatia wahanga misaada
ya kibinadamu.
ix.
Kuimarisha
mazingira bora ya kufanyia kazi na
x.
Kuimarisha
ushirikiano na nchi nyingine duniani katika masuala ya kijeshi
UTEKELEZAJI
WA MAONI NA USHAURI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA
TANZANIA YA ULINZI NA USALAMA
9. Mheshimiwa Spika, wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ulinzi na
Usalama ilipokaa na kujadili Makadirio ya Mapato, Mpango na Bajeti ya Wizara ya
Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka 2013/14 ilitoa maoni, ushauri na
maelekezo kadhaa kwa Wizara hii yaliyolenga kuboresha utendaji wa majukumu
yake. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa maoni, ushauri na maelekezo
yaliyotolewa yamefanyiwa kazi na majibu yake yameainishwa katika Kiambatanisho Namba 1. Aidha, hoja
mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wa mjadala huo pia
zimezingatiwa katika mpango na bajeti ya mwaka 2014/15 ninayowasilisha leo hapa
Bungeni.
HALI YA USALAMA WA MIPAKA MWAKA 2013/14
10.
Mheshimiwa
Spika, hali ya usalama wa mipaka ya nchi yetu (nchi
kavu, maji na anga) kwa mwaka 2013/14 ilikuwa shwari kwa ujumla. Licha ya
kuwepo kwa matishio na mashambulizi ya kigaidi katika eneo la Afrika Mashariki,
hakukujitokeza tukio lolote la uharamia kwa upande wa bahari yetu. Hata hivyo, vitendo
vya usafirishaji wa madawa ya kulevya na biashara haramu ya usafirishaji
binadamu vilijitokeza. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na vyombo
vingine vya Usalama vimeendelea
kushirikiana katika kukabiliana na hali hiyo. Kwa upande wa mipaka, matukio ya
uharibifu wa alama za mipaka na ujenzi holela unaofanywa na wananchi wanaoishi
maeneo ya mipakani hususan maeneo ya Namanga, Jasini, Tunduma na Mtukula
yameendelea kujitokeza. Hata hivyo, vikao vya wataalamu kutoka Serikali za Tanzania
na nchi jirani za Kenya, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na
Zambia vyenye lengo la kutatua matatizo hayo vimeanza. Kufuatia vikao hivyo, alama nane za mpaka (umbali
wa km 14.8) zilizokuwa zimeharibiwa katika Wilaya za Tarime (Tanzania) na Kurya
(Kenya) zimeimarishwa, ambapo alama saba zimejengwa upya na moja imekarabatiwa.
Aidha, alama mpya sabini zimejengwa katikati ya beacons za zamani ili kufanya
mpaka huo uonekane kwa urahisi. Mazungumzo kuhusiana na utata wa mpaka wa
Tanzania na Malawi katika ziwa Nyasa
yanaendelea chini ya uratibu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa. Pamoja na
hali hiyo, hakuna uhasama wowote wa kijeshi uliojitokeza baina ya nchi zetu.
MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA MWAKA 2013/14
11.
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka 2013/14 Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ilikadiria
kukusanya mapato ya jumla ya shilingi
68,206,000.00 kutoka katika Mafungu yake matatu ya 38-NGOME, 39-JKT na 57-Wizara.
Hadi kufikia mwezi Machi, 2014 Mafungu hayo yalikusanya mapato ya jumla ya shilingi 43,317,624.00
sawa na asilimia 63.5 ya
makadirio.
12.
Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka wa Fedha 2013/14, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iliidhinishiwa
jumla ya shilingi 1,102,999,529,000.00 kwa
ajili ya Matumizi ya Kawaida na Maendeleo katika Mafungu yake matatu. Kati ya
fedha hizo, shilingi 857,417,502,000.00 zilitengwa
kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi
245,582,027,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Maendeleo. Hadi kufikia
mwezi Machi 2014, Wizara ilikuwa imepokea jumla ya shilingi 768,496,687,343.00 (sawa na asilimia 69.7) ya bajeti yake. Kati
ya fedha hizo shilingi 719,118,556,008.00 zilikuwa ni kwa ajili
ya Matumizi ya Kawaida (sawa na asilimia 83.8)
ya fedha zilizoidhinishwa kwa ajili ya matumizi hayo. Kwa upande wa Matumizi ya
Maendeleo, fedha zilizopokelewa ni shilingi
49,378,131,335.00 (sawa na asilimia 20.1) ya fedha zote zilizoidhinishwa
kwa ajili ya shughuli za maendeleo. Mchanganuo wa Matumizi ya Kawaida na
Maendeleo kwa Mafungu yote matatu ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
hadi mwezi Machi, 2014 umeonyeshwa katika Kiambatanisho
Namba 2.
13.
Mheshimiwa Spika, tathmini ya fedha zilizopokelewa inaonesha kwamba mwenendo wa upatikanaji wa fedha kwa
ajili ya Matumizi ya Kawaida katika kipindi hicho kiujumla ulikuwa ni wa
kuridhisha. Fedha kwa ajili ya mishahara
na marupurupu zilipokelewa kulingana na makisio ya bajeti. Hata hivyo, fedha
zilizotolewa kwa ajili ya shughuli za
Maendeleo hadi kufikia mwezi Machi, 2014 zilikuwa kidogo ukilinganisha na
mahitaji. Hali hii imeathiri utekelezaji wa miradi mbalimbali ya
maendeleo.
Shughuli za Matumizi ya Kawaida
14.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/14 Wizara ya Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa ilipanga kutekeleza shughuli mbalimbali ili kufikia malengo niliyoyaeleza
hapo awali. Shughuli hizo ni pamoja na za:- kulipa stahili mbalimbali za
wanajeshi, watumishi wa Umma na vijana walioko katika mafunzo ya JKT;
kusafirisha wastaafu; na kutoa huduma muhimu za chakula, tiba na sare. Wizara
pia ilipanga kulipia huduma za umeme, maji, simu na mafuta kwa ajili ya uendeshaji
wa majukumu ya ulinzi zikiwemo za mafunzo ya kijeshi, mafunzo ya ulinzi wa
mgambo na kutengeneza vifaa na zana za kijeshi.
Mafunzo
na Mazoezi ya Kijeshi
15.
Mheshimiwa Spika, uimara
wa jeshi lolote duniani unategemea mafunzo pamoja na mazoezi ya mara kwa mara. Katika
mwaka 2013/14 jeshi letu
lilipata fursa ya kushiriki mazoezi mbalimbali ya pamoja na nchi marafiki.
Miongoni mwa mazoezi hayo ni zoezi la Kituo cha Uamrishaji (Command Post Exercise - CPX). Zoezi hilo la uamrishaji lilikuwa ni
sehemu ya maandalizi ya zoezi la
medani litakalohusisha Majeshi ya Nchi wanachama
wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Zoezi hilo lijulikanalo kwa jina la USHIRIKIANO IMARA 14 (Field Tactical
Exercise - FTX), litafanyika
katika jimbo la Mwaro nchini Burundi tarehe 13 – 26 Oktoba, 2014. Aidha,
kupitia Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), Jeshi letu
limeshiriki katika mazoezi ya:- “EX WILWETSCHIA” lililofanyika mwezi Septemba, 2013 nchini Namibia;
“EX BLUE ZAMBEZI” lililofanyika
nchini Angola mwezi Oktoba, 2013; na “EX
CUTLASS EXPRESS” lililofanyika mwezi Novemba, 2013 nchini Seychelles. Jeshi linategemea pia kushiriki katika zoezi linaloandaliwa
na Umoja wa Afrika (AU). Zoezi hilo lijulikanalo kwa jina la Amani Afrika II FTX litafanyika nchini Lesotho mwezi Oktoba/Novemba 2014. Mazoezi
ya namna hii siyo tu yameimarisha jeshi letu kimedani, bali pia yamekuwa chachu
kubwa ya kuboresha mahusiano na majeshi mengine.
(i)
Mafunzo
ya Ulinzi wa Mgambo
16.
Mheshimiwa Spika, Wizara
ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea kuweka umuhimu katika mafunzo ya
mgambo. Katika kipindi hiki Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa kushirikiana
na vyombo vya Usalama limeendesha mafunzo katika ngazi mbalimbali kwa wananchi
13,484 (Wanaume 12,337 na wanawake 1,147) ikiwa ni ongezeko la asilimia 14.8 ikilinganishwa
na mwaka 2013. Natoa wito kwa Viongozi wa Wilaya na Mikoa kuongeza kasi ya
usimamizi na ushiriki wa mafunzo hayo na kutoa huduma stahiki za usafiri kwa
wakufunzi wetu, hifadhi ya silaha na maeneo ya mafunzo. Matarajio ya baadaye ya
Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania ni kuanzisha rasmi Kamandi ya Jeshi la
Akiba.
(ii) Huduma za Afya na Tiba
17.
Mheshimiwa Spika, pamoja
na majukumu ya kiulinzi, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea
kutoa huduma za tiba kwa maafisa, askari, watumishi wa Umma, familia za wanajeshi
na wananchi kwa ujumla. Huduma hizo zimezidi kuimarika baada ya kuboresha
hospitali za JWTZ zilizoko Mwanza, Mbeya, Bububu (Unguja), Tabora, Nyumbu (Pwani)
na Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli (Arusha). Lengo letu ni kuboresha huduma hiyo pia katika
ngazi ya vituo vya afya vikosini. Ningependa Bunge lako Tukufu litambue kwamba asilimia
80 ya wagonjwa wanaohudumiwa na hospitali na vituo vyetu ni wananchi wanaoishi maeneo
jirani.
(iii)
Ushirikiano
wa Kiulinzi na Kijeshi na Nchi Nyingine
18.
Mheshimiwa Spika, ushirikiano kati
ya nchi yetu na nchi nyingine katika nyanja za kijeshi ni suala muhimu katika mustakabali
wa ulinzi na usalama duniani. Hivyo basi, nchi yetu inaendelea kuimarisha
ushirikiano wa kijeshi na kiulinzi (Bilateral Cooperation) na nchi mbalimbali
zikiwemo: - China, Ujerumani, Marekani, Afrika ya Kusini, India, Umoja wa Falme
za Kiarabu, Uingereza, Canada na Urusi. Kupitia ushirikiano huo, Jeshi letu,
pamoja na mambo mengine limenufaika katika maeneo yakiwemo ya nyanja za mafunzo
ya kijeshi na kitaaluma, zana na vifaa, mazoezi na michezo. Kwa ujumla
ushirikiano huu umekuwa ni wa manufaa makubwa.
19.
Mheshimiwa Spika, katika
mwaka 2013/14, Serikali imeendelea kudumisha ushirikiano katika Jumuiya za
kikanda (Regional Cooperation) hususan
za Afrika Mashariki (EAC) na Kusini mwa Afrika (SADC). Ushirikiano huo
ulijikita katika nyanja za mafunzo, mazoezi na michezo baina ya majeshi ya nchi
zetu. Na kama nitakavyoeleza hapo baadaye, Tanzania, tukiwa wanachama wa nchi
za SADC tumepeleka nchini DRC kikosi cha ulinzi wa amani kuungana na majeshi ya
Umoja wa Mataifa. Aidha, kupitia vyuo vyetu, Jeshi letu limeendelea kutoa
nafasi za mafunzo ya kijeshi kwa Majeshi ya nchi za Botswana, Kenya, Uganda,
Rwanda, Burundi, Malawi, Zambia, Namibia, Seychelles, Swaziland na Zimbabwe
kupitia:- Chuo cha Taifa cha Ulinzi (National Defence College- NDC); Chuo cha Ukamanda
na Unadhimu (Command and Staff College-CSC); na Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi (Tanzania
Military Academy-TMA). Vivyo hivyo,
Maafisa wetu nao walipata mafunzo katika baadhi ya nchi hizo.
20.
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
limeendelea kushiriki katika Operesheni za Ulinzi wa Amani katika
nchi mbalimbali. Hadi sasa, ushiriki wa wanajeshi wetu katika Operesheni hizo
ni kama ifuatavyo;
i.
Kikosi
kimoja (TANZBATT – 8) kipo Darfur nchini Sudan.
ii.
Kikosi
kimoja (TANZBATT – 1) kipo Mashariki mwa DRC ikiwa ni sehemu ya MONUSCO Force
Intervention Brigade.
iii.
Kombania
mbili za Polisi Jeshi zipo nchini Lebanon.
iv.
Waangalizi
wa amani (military observers) na maafisa
wanadhimu (staff officers) wapo katika baadhi ya nchi ikiwemo Sudani
Kusini.
(iv) Mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa Vijana
21.
Mheshimiwa
Spika, Jeshi la Kujenga Taifa limeendelea kutoa
mafunzo kwa vijana wa kujitolea na wa Mujibu wa Sheria. Malengo ya mafunzo hayo
ni pamoja na kujenga uzalendo, ukakamavu, maadili mema, utaifa na kuwapa stadi
za maisha vijana wa kitanzania. Katika mwaka 2013/14 JKT linaendesha operesheni
moja ya mafunzo ya vijana wa kujitolea ijulikanayo kama Operesheni Miaka
Hamsini ya Muungano. Katika operesheni hii idadi ya vijana 8,439 (wavulana
6,610 na wasichana 1,829) wanaendelea na mafunzo yaliyoanza mwezi Machi 2014. Nafurahi
kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba hivi sasa vyombo vya Ulinzi na Usalama vimeanza
kutekeleza utaratibu wa kuajiri vijana waliopitia mafunzo ya JKT. Idadi ya
vijana 7,062 walichukuliwa na vyombo hivyo kwa mwaka huu. Aidha, vijana
155 walichukuliwa na taasisi na makampuni binafsi (Benki Kuu ya Tanzania-BOT,
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania-TAA, Barrick Gold Mine na Geita Gold Mines).
22.
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa mafunzo ya Mujibu wa Sheria,
na kama ilivyoelezwa mwaka jana, mafunzo
hayo yalirejeshwa kwa wahitimu wa kidato cha sita kuanzia mwezi Machi 2013. Mafunzo haya yaliendelea
kutolewa ambapo jumla ya vijana 10,505 wameweza kuhitimu mafunzo hayo kipindi
hiki. Kati yao, vijana 9,510 walihitimu mafunzo awamu ya pili iliyomalizika
mwezi Oktoba, 2013. Ingawa mategemeo yalikuwa kuchukua idadi ya vijana 15,000
wajiunge na mafunzo awamu ya tatu, ni vijana 1,002 waliweza kujiunga na mafunzo
hayo yaliyoanza mwezi Oktoba, 2013 hadi Januari 2014, ambapo vijana 995 ndio
waliohitimu. Kupatikana kwa idadi ndogo ya vijana wa awamu ya tatu na
kutopatikana kabisa kwa vijana awamu ya nne kulitokana na vijana wengi kujiunga
na vyuo vya elimu ya juu ambapo muhula wa masomo huanza mwezi Oktoba.
23. Mheshimiwa Spika, utaratibu wa vijana waliomaliza kidato cha
sita kujiunga na JKT kwa mujibu wa sheria si wa hiari. Hivyo kwa mwaka huu Jeshi
la Kujenga Taifa litachukua vijana wasiopungua 45,000 watakaomaliza kidato cha
sita hivi karibuni. Awamu ya kwanza kwa
mwaka 2014/15 itaanza mwezi Juni hadi Septemba, 2014 na itahusisha vijana
20,000. Awamu ya pili itakayochukua
vijana 14,450 itaanza mwezi Oktoba 2014
hadi Januari 2015. Na awamu ya tatu
itakayochukua vijana 10,550 itaanza mwezi Januari hadi Aprili 2015. Naomba
vijana wote wanaotakiwa kujiunga na mafunzo ya JKT watambue kuwa ni kosa
kisheria kukaidi wito wa kujiunga na mafunzo hayo.
(v)
Mapambano dhidi ya UKIMWI
24. Mheshimiwa Spika, UKIMWI umeendelea kuwa janga la kitaifa na
kuleta athari kubwa kijamii, kiuchumi na kuathiri nguvu kazi inayotegemewa. Hivyo,
jitihada za kupambana na maambukizi ya UKIMWI ni suala endelevu. Kwa msingi huo
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeendelea kutoa elimu ya jinsi ya
kujikinga ili kuzuia maambukizi mapya. Aidha, wizara imekuwa ikihimiza upimaji
wa hiari kwa maafisa, askari na watumishi wa umma na vijana wa JKT kwa kutumia
waelimishaji rika. Kwa wale ambao tayari wameshaambukizwa virusi vya UKIMWI, Wizara
imeendelea kutoa huduma ya lishe na dawa
za kupunguza makali ya virusi (ARVs).
Shughuli
za Matumizi ya Maendeleo
25.
Mheshimiwa
Spika, utekelezaji
wa shughuli za maendeleo hadi kufikia robo ya tatu ya Mwaka wa Fedha 2013/14
kwa ujumla haukuwa mzuri. Mafungu yote matatu yalipokea wastani
wa asilimia 20.1 ya bajeti iliyoidhinishwa. Kwa mapokezi hayo, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
imeweza kutekeleza miradi ifuatayo; mradi wa ujenzi wa nyumba 10,000 za makazi
ya wanajeshi, kulipia madeni ya kimikataba, kukarabati majengo pamoja na
kuboresha mazingira ya kufanyia kazi na makazi katika makambi na viteule vya
JKT,
ulipiaji fidia kwa maeneo yaliyotwaliwa na Jeshi, kuboresha
mawasiliano jeshini, ujenzi wa Shule ya Mafunzo
ya Awali ya Kijeshi
Kihangaiko, kulipia ujenzi wa viporo vya miradi ya maji Msangani na Ngerengere na ukarabati wa
viteule vya Kasanga, Kalando na Hospitali ya Jeshi Lugalo, kuboresha
miundombinu ya Shirika la Nyumbu na ununuzi
wa malighafi kwa Shirika la Mzinga.
(i)
Ujenzi
wa Nyumba na Makazi ya Wanajeshi
26.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2013/14, Wizara yangu ililiarifu Bunge lako Tukufu kwamba, maandalizi ya ujenzi wa nyumba 10,000 kwa ajili ya makazi ya askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi
wa Tanzania yamekamilika ambapo ujenzi wa nyumba 6,064 za awamu ya kwanza ungeanza.
Nafurahi kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa ujenzi
wa nyumba hizo unaotekelezwa na Kampuni ya
Shanghai Construction (Group) General Company ulianza
rasmi tarehe 17 Julai, 2013. Ujenzi huo utakaofanyika katika vikosi 37 vya Jeshi la Ulinzi la Wananchi
wa Tanzania na Jeshi la Kujenga Taifa utakuwa katika mikoa tisa kwa
mgawanyo ufuatao; Arusha (792), Dar
es Salaam (2,288), Dodoma (592), Kagera (144),
Morogoro (616), Pemba (320), Pwani (840),
Kigoma (160) na Tanga (312). Ujenzi huu utachukua
muda wa miezi hamsini (50). Hadi sasa, ujenzi tayari umeanza kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani ambapo
hatua ya ujenzi huo imefikia asilimia 80. Maandalizi ya ujenzi katika mikoa ya Arusha, Morogoro, Pemba na Tanga unaotarajiwa kuanza mwezi
Juni 2014 yamekamilika.
(ii)
Ununuzi wa
Zana na Vifaa vya Kijeshi
27.
Mheshimiwa Spika, Wizara
imeendelea na azma yake ya kuimarisha Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwa
kulipatia zana na vifaa vya kisasa. Katika mwaka 2013/14 Jeshi lilipokea zana
na vifaa vya kisasa ambavyo vimeendelea kutumika katika shughuli za ulinzi na
mafunzo. Nisingependa kuwachosha Waheshimiwa Wabunge katika eneo hili kwani
mwenye macho alijionea mwenyewe yaliyojiri siku ya kilele cha maadhimisho ya
miaka 50 ya Muungano tarehe 26 Aprili, 2014.
Kwa yule ambaye hakubahatika kuyaona, ni imani yangu kuwa alisimuliwa. Mpango wa ununuzi wa zana za kisasa na bora
ni endelevu, hivyo natarajia Bunge lako Tukufu litaendelea kuidhinisha fedha za
kutekeleza mpango huu.
(iii) Shirika la Uzalishaji Mali la SUMAJKT
28. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Kujenga Taifa kupitia Shirika
lake la Uzalishaji Mali (SUMAJKT) linaendelea kutekeleza majukumu yake kupitia idara
zake za uhandisi na ujenzi, viwanda na kilimo, biashara na utalii. Utekelezaji wa shughuli hizi unalenga katika
kuhakikisha kuwa SUMAJKT inafanikisha malengo iliyojiwekea kwa tija na ufanisi mkubwa.
Katika kutekeleza azma ya kujitosheleza kwa chakula, mwaka 2013/14 SUMAJKT
lilifanikiwa kulima ekari 4,390 za mazao mbalimbali ya chakula na ekari 1,913
za mbegu bora. Tatizo linaloendelea
kulikabili SUMAJKT katika eneo hili ni kutokulipwa madeni. Hadi sasa jumla ya
shilingi 495,792,000.00 hazijalipwa na makampuni yaliyouziwa mbegu hizo.
Makampuni hayo ni Agricultural Seed Agency (ASA), Tropical Seed Co. Ltd na
Southern Highland Seed Growers Ltd.
29. Mheshimiwa Spika, SUMAJKT kupitia “National Service Construction
Department” inatekeleza miradi ya ujenzi
wa majengo na barabara. Katika kipindi cha mwaka 2013/14 Jeshi la Kujenga Taifa
limefanya mageuzi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuboresha ujuzi wa wataalam,
kuongeza matumizi ya zana na mitambo pamoja na kuimarisha uwezo wa Idara zake
ili kujikita kwenye utekelezaji wa miradi mikubwa ya ujenzi wa majengo na barabara.
Miongoni mwa miradi inayotekelezwa ni ya
ujenzi wa Shule ya Mafunzo ya Awali (Recruits Training School - RTS) Kihangaiko, ujenzi
wa barabara kiwango cha lami wilayani Chato, ujenzi wa barabara za ndani katika
mgodi wa Tulawaka na ukarabati wa jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa.
30. Mheshimiwa Spika, katika eneo la ulinzi wa mali za wananchi,
SUMAJKT limejizatiti katika shughuli za ulinzi kupitia kampuni tanzu ya SUMAJKT
Guard Ltd. Vijana wanaotoa huduma hii ni wale waliohitimu mafunzo ya JKT ambao sasa
wanafikia idadi ya 1,668. Hadi sasa SUMAJKT Guard Ltd wameweza kupata zabuni ya
kutoa huduma hiyo ya ulinzi kwa taasisi za Serikali, mashirika ya Umma na
binafsi, viwanda na migodi. Katika mwaka
2014/15 Kampuni hii inatarajia kuajiri vijana 2,000 kuongeza idadi ya nguvu
kazi iliyopo na hivyo kupanua utoaji huduma hiyo katika taasisi mbalimbali za
umma na binafsi.
31.
Mheshimiwa
Spika, kama ilivyoelezwa katika hotuba ya mwaka
2013/14 kuhusiana na mradi wa matrekta, matrekta 1,558 na zana za kilimo zenye
thamani ya shilingi 53,675,837,001.00 ziliuzwa kwa mkopo kwa wadau mbalimbali
zikiwemo Halmashauri za Wilaya, vikundi vya uzalishaji mali, SACCOS na watu
binafsi wakiwemo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge. Marejesho ya mikopo hii hadi kufikia Machi, 2014 ni kiasi cha
Shilingi 26,162,374,328.96. Baada ya mauzo ya awamu ya kwanza kukamilika,
SUMAJKT bado limeendelea kutekeleza mradi wa uagizaji wa matrekta mengine
pamoja na zana za kilimo. Hivi sasa yapo matrekta 197 aina ya New Holland na
Farmtrac kwenye kituo cha Mwenge. Waheshimiwa Wabunge, Halmashauri za Wilaya,
vikundi vya uzalishaji mali, SACCOS na watu binafsi wenye mkopo mnakumbushwa kurejesha mikopo
yenu na mnahamasishwa kuja kununua
matrekta mapya.
(i) Shughuli za Shirika la Mzinga
32.
Mheshimiwa Spika, shughuli
za msingi za Shirika la Mzinga na kampuni yake tanzu ya Mzinga Holdings zimeendelea
kwa mafanikio. Uzalishaji wa mazao ya risasi na milipuko umeongezeka ikiwa ni
pamoja na kupata masoko mapya ya mazao hayo nje ya nchi. Aidha, katika ukanda
wetu wa Afrika Mashariki, Shirika la Mzinga limeteuliwa kuwa Centre of
Excellence. Kwa upande wa Mzinga Holdings shughuli zake zimejikita katika
ujenzi na ukarabati wa majengo na uendeshaji wa maduka ya kuuza bidhaa zisizolipiwa
kodi (Duty Free Shops) kwenye vikosi na makambi ya Jeshi.
(ii)
Shughuli
za Shirika la Nyumbu
33.
Mheshimiwa Spika, shughuli za utafiti
katika Shirika la Nyumbu hazikuwa na mafanikio makubwa kutokana na kutopatikana
kwa fedha za maendeleo. Hivyo tafiti zinazohusiana na mitambo ya kuchuna
mkonge, “engine” na “gear box” za matrekta madogo na uzalishaji wa vipuri vya
mashine (prototype) na pampu ya umwagiliaji hazikukamilika. Hata hivyo,
shughuli za uzalishaji vipuri mbalimbali ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa
vipuri vya Shirika la Reli (TRL) hususan “brake blocks” zimeendelea. Aidha,
Shirika limeendelea kutoa huduma ya kutengeneza pampu za maji za DAWASCO na pia
kuhusika katika ufungaji na ukarabati wa vifaa vinavyotumiwa na Jeshi la Ulinzi
la Wananchi wa Tanzania kwa ajili ya Ulinzi wa Amani huko Darfur - Sudan,
Lebanon na Mashariki mwa DRC. Miongoni mwa vifaa vilivyofanyiwa ukarabati na
Nyumbu ni magari ya kubebea mizigo, maji, mafuta na askari. Aidha, uzalishaji
na upatikanaji wa “Powered Brick making machine”, mashine za kusaga na kukoboa
nafaka unaendelea.
(iii)
Mtandao
wa Mawasiliano Jeshini
34.
Mheshimiwa Spika, kazi
ya ukarabati na uboreshaji wa mawasiliano jeshini imeendelea kutekelezwa. Awamu
ya kwanza ya mradi wa uboreshaji wa mawasiliano ndani ya vikosi imekamilika
katika mkoa wa Dar es Salaam. Kazi ya uboreshaji wa mawasilianao ndani ya
vikosi vilivyo nje ya Mkoa wa Dar es Salaam haijafanyika kutokana na
kutokupatikana kwa fedha za maendeleo. Hivyo utekelezaji wa kazi hiyo pamoja na
awamu ya pili ya kuunganisha mfumo wa Satellite utategemeana na upatikanaji wa
fedha. Zoezi la kusimika minara ya mawasiliano huru na salama nchi nzima linaendelea.
(iv) Uvamizi wa Maeneo ya Jeshi, Upimaji na Ulipaji Fidia
35.
Mheshimiwa Spika, tatizo la
uvamizi wa maeneo ya Jeshi bado linaendelea kujitokeza. Katika kipindi hiki
maeneo yaliyoathirika na tatizo hilo ni pamoja na Tondoroni – Pwani, Tanganyika
Packers na Monduli –Arusha, Kimbiji – Dar es Salaam, Chita – Morogoro, Itaka na
Uyole – Mbeya, Uwanja wa Ndege na Ilemela – Mwanza na Kisakasaka - Unguja. Pamoja na hatua zinazochukuliwa zikiwemo za
kisheria, nawasihi wananchi wasivamie maeneo ya Jeshi wala kuendesha shughuli
za kibinadamu katika maeneo hayo.
36.
Mheshimiwa Spika, kuhusu fidia,
katika mwaka 2013/14 Wizara imekamilisha kulipa fidia katika maeneo yafuatayo;
Mwakidila (Tanga), Cheyo (Tabora), Mwantini (Shinyanga) na Mataya Kiromo (Pwani). Mipango yetu ya kulipa fidia katika maeneo
mengine yaliyochukuliwa kwa matumizi ya Jeshi inaendelea. Aidha, maeneo
tunayoyalenga kulipa fidia katika mwaka 2014/15 ni ya Makambako (Njombe), Ilemela
na Kigongo Ferry (Mwanza). Zoezi la kupima na kuweka alama za mipaka, mabango
na “buffer zones” linaendelea.
CHANGAMOTO ZA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA
MWAKA 2013/14
37.
Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa katika
utekelezaji wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2013/14 ni ya Wizara kuidhinishiwa
kiwango kidogo cha bajeti ikilinganishwa na mahitaji halisi. Kwa mfano katika
mwaka wa fedha 2013/14 wakati mahitaji halisi kwa kuzingatia vipaumbele vya Wizara
yalikuwa ni shilingi 1,741,888,249,500.00, bajeti iliyoidhinishwa ilikuwa
shilingi 1,102,999,529,000.00 sawa na asilimia 63.3 ya mahitaji. Hali hiyo
imepelekea utekelezaji wa shughuli za Wizara hususan shughuli za maendeleo
kutofikia malengo yaliyokusudiwa. Baadhi ya shughuli zilizoathirika ni za
uboreshaji wa viwanda, utafiti na uzalishaji wa bidhaa za kijeshi, kulipia
huduma na mahitaji muhimu kama vile mafuta, maji na umeme. Hali hiyo imesababisha Wizara
kulimbikiza madeni makubwa ya kimkataba.
Kwa upande wa matumizi ya kawaida, changamoto hii imesababisha ongezeko kubwa la
madeni yakiwemo ya wazabuni na ya taasisi zinazotoa huduma muhimu za maji, umeme
na simu.
38.
Mheshimiwa Spika, changamoto
nyingine inayoikabili Wizara ni mtiririko wa fedha kutoka Hazina kutozingatia
mpango kazi wa Wizara, ambapo fedha zinapoidhinishwa, hutolewa zikiwa pungufu
na bila kuzingatia ratiba ya mikataba.
Hali hii imesababisha shughuli za Wizara hususan za maendeleo
kutotekelezwa kama ilivyopangwa. Matokeo yake ni kuwa Wizara imeshindwa kukamilisha ujenzi wa
majengo na miundombinu katika makambi, kushindwa kulipa mikopo mbalimbali ukiwemo
wa NSSF na kushindwa kulipa malipo ya kimikataba.
MPANGO WA MWAKA 2014/2015
39.
Mheshimiwa Spika, mpango wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga
Taifa kwa mwaka 2014/15 umekusudia kuimarisha utendaji kazi na ufanisi wa Jeshi
la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania katika kutekeleza majukumu ya Ulinzi wa Taifa
kulingana na Dira, Dhima na Malengo ya Wizara. Vilevile, mpango umelenga
kuimarisha mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa kwa vijana wa Mujibu wa Sheria na
wale wa kujitolea. Aidha, Wizara inakusudia kukamilisha miradi inayoendelea na
kulipa madeni ya kimikataba. Hivyo, Wizara imepanga kutekeleza shughuli zifuatazo:-
i. Kununua vifaa na zana za kijeshi ikiwemo
vifaa vya uhandisi wa medani na ndege vita.
ii.
Kuanza ujenzi
wa gati katika Kamandi ya Jeshi la Wanamaji.
iii.
Kuboresha
mifumo ya mawasiliano ya ndani na nje ya vikosi na makambi ya Jeshi.
iv.
Kuendelea na
ujenzi wa nyumba 6,064 kwa ajili ya makazi ya wanajeshi.
v.
Kukamilisha
ujenzi wa Shule ya Mafunzo ya Awali ya Kijeshi (RTS) – Kihangaiko Pwani na Chuo
cha Ukamanda na Unadhimu (CSC) – Tengeru Arusha.
vi.
Kuboresha viwanda
vya Mashirika ya Mzinga na Nyumbu.
vii.
Kulipa mkopo
wa NSSF wa ujenzi wa nyumba za makazi ya wanajeshi.
viii.
Upimaji na
ulipaji wa fidia ya ardhi katika maeneo ya wananchi yaliyochukuliwa kwa ajili
ya matumizi ya Jeshi.
ix.
Kuanza ujenzi
wa Hospitali Kuu ya Jeshi huko Mataya - Kiromo Pwani.
x.
Ujenzi na umaliziaji
wa viporo vya nyumba, bwalo na bweni huko Pemba.
xi.
Ujenzi wa
maghala ya kuhifadhia silaha na zana pamoja na kuboresha mawasiliano.
xii.
Kulipia
gharama za matumizi ya mahitaji muhimu ya umeme, maji, simu na huduma za uendeshaji
wa majukumu ya kimsingi.
xiii.
Kulipia
stahili mbalimbali za wanajeshi, vijana wa Jeshi la Kujenga
Taifa na Watumishi wa Umma.
xiv.
Kuimarisha
ushirikiano na nchi nyingine duniani katika nyanja za kijeshi na ulinzi.
xv.
Kulipa madeni
ya kimkataba.
xvi.
Kuongeza uwezo
wa makambi ya JKT kuweza kuchukua idadi kubwa ya vijana kwa wakati mmoja.
xvii.
Kupanua wigo
wa makundi ya vijana wa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa Sheria.
SHUKRANI
40. Mheshimiwa Spika, kabla
sijahitimisha hotuba yangu napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru wafuatao kwa michango yao katika maandalizi
ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yangu:- Katibu Mkuu Bw. Job D.
Masima; Naibu Katibu Mkuu Bi. Mwintango Rose Shelukindo; Mkuu wa Majeshi ya
Ulinzi Jenerali Davis A Mwamunyange; Mnadhimu Mkuu Luteni Jenerali Samuel A
Ndomba; Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa Meja Jenerali Raphael M Muhuga; Wakuu wa
Kamandi za Jeshi la Nchi Kavu Meja Jenerali Salum M Kijuu; Jeshi la Anga Meja
Jenerali Joseph F Kapwani na Jeshi la Wanamaji Brigedia Jenerali Rogastian S
Laswai; Meneja Mkuu wa Shirika la Mzinga Meja Jenerali Dkt Charles N Muzanila
na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumbu Kanali John K Nchimbi.
41. Mheshimiwa Spika, pia napenda
kuwashukuru Wakuu wa Idara na Vitengo (Makao Makuu ya Wizara), Wakuu wa Matawi
(NGOME), Wakuu wa Idara (Makao Makuu ya Jeshi la Kujenga Taifa), Maafisa na Askari
na Watumishi wa Umma wa Wizara kwa kunipokea na kunipa ushirikiano katika
kufanikisha majukumu ya Wizara. Vile
vile, naomba kuwashukuru wapiga kura wangu wa jimbo la Kwahani kwa ushirikiano
wao walionipa katika mwaka 2013/14. Ni matumaini yangu kuwa tutaendelea
kushirikiana zaidi kwa manufaa ya jimbo letu na Taifa kwa ujumla. Aidha,
namshukuru Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na watumishi walio chini yake kwa
kuchapisha Hotuba hii kwa wakati.
42.
Mheshimiwa
Spika, kwa umuhimu wa
pekee na kwa kupitia Bunge lako Tukufu naomba kuwasilisha salamu za pongezi maalum
za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt.
Jakaya Mrisho Kikwete kwa wanajeshi wote kwa kufanikisha maadhimisho ya miaka
50 ya Muungano wa Tanzania. Kazi waliyoifanya ni kubwa na waliifanikisha kwa
weledi, utii, uhodari, ujasiri na kwa kishindo cha hali ya juu. Ushiriki wao
huo umeudhihirishia umma wa Watanzania na ulimwengu kwa ujumla kuwa jeshi letu
ni imara, shupavu na lipo tayari kulinda, kutetea na kudumisha Muungano wetu. Nami
nikiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa natamka kuwa ‘I am proud of
our gallant men and women in uniform’.
43. Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia
na kwa niaba ya wanajeshi wote namshukuru sana Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe.
Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete. Hiba (legacy) yake ya uongozi, ushupavu, uvumilivu na maridhiano itakumbukwa
na kuenziwa vizazi na vizazi hususan kwetu sisi wanajeshi. Ahadi
yetu kwake ni kuwa tutaendelea kusimama imara, kupokea na kutii amri na
maelekezo yake bila hila yoyote na kutoyumbishwa na kauli potovu za kisiasa.
MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA
BAJETI YA MWAKA 2014/15
i.
Makadirio
ya Mapato
44.
Mheshimiwa Spika, vyanzo vya mapato ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa na Taasisi zake bado ni vidogo.
Chanzo kikuu cha mapato kwa Wizara
ya Ulinzi na JKT na taasisi zake kimeendelea
kutegemea uuzaji wa nyaraka za zabuni. Hivyo, makadirio ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2014/15 ni kukusanya
mapato yenye jumla ya shilingi 60,506,000.00
kwa mchanganuo ufuatao:
Fungu38
– NGOME = 2,001,000.00
Fungu
39 – JKT = 48,503,000.00
Fungu
57 – Wizara = 10,002,000.00
Jumla shilingi = 60,506,000.00
ii.
Bajeti
ya Matumizi ya Kawaida na Maendeleo
45.
Mheshimiwa Spika, ili Wizara ya Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa iweze kutekeleza majukumu yake katika mwaka 2014/15 inaomba
kuidhinishiwa jumla ya shilingi
1,269,076,056,000.00 ambazo kati yake shilingi
1,020,076,056,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi 249,000,000,000.00 ni kwa
ajili ya Matumizi ya Maendeleo. Mchanganuo wa bajeti hiyo kwa kuzingatia
mafungu ya Wizara ni ufuatao:-
|
|
FUNGU 38 NGOME
|
|
Matumizi ya Kawaida shilingi
|
803,542,549,000.00
|
Matumizi ya Maendeleo shilingi
|
12,000,000,000.00
|
Jumla
ya Makadirio kwa Fungu 38 shilingi
|
815,542,549,000.00
|
FUNGU
39 JKT
Matumizi ya Kawaida shilingi
|
196,822,661,000.00
|
Matumizi ya Maendeleo shilingi
|
7,000,000,000.00
|
Jumla
ya Makadirio kwa Fungu 39 shilingi
|
203,822,661,000.00
|
FUNGU 57 WIZARA YA ULINZI
Matumizi ya Kawaida
shilingi
|
19,710,846,000.00
|
Matumizi ya Maendeleo shilingi
|
230,000,000,000.00
|
Jumla
ya Makadirio kwa Fungu 57 shilingi
|
249,710,846,000.00
|
MWISHO
46.
Mheshimiwa
Spika, hotuba hii inapatikana pia katika tovuti
ya Wizara (www.modans.go.tz). Naomba kutoa Hoja.
No comments:
Post a Comment