Kituo
cha Uwekezaji (TIC) kitaendelea kusaidia wajasiriamali wadogo, kujenga uwezo
katika biashara zao, ili wakue na kukuza uchumi wao na wa nchi kwa ujumla.
Mkurugenzi
wa Huduma wa kituo hicho, Nakuala Senzia, ameyasema hayo hivi karibuni, wakati
wa kufunga mafunzo ya siku sita ya wajasiriamali wadogo 27, wanaojishughulisha
na ufugaji wa ng’ombe wa maziwa kutoka mikoa ya Pwani, Morogoro na Tanga.
“Mafunzo
haya ni mwanzo tu wa kukuza wafugaji hawa ili waendelee kuuza maziwa kwa
ufanisi zaidi,” alisema huku akikitaja kiwanda cha Tanga Fresh Ltd, kuwa ni
soko ambalo wafugaji hao wanaweza kuuza maziwa yao.
Alisisitiza
kuwa kituo hicho kitaendelea kushirikiana na uongozi wa Mkoa wa Tanga na wadau wengine, kuhakikisha wanawakuza wajasiriamali wadogo
pamoja na kutangaza shughuli za uwekezaji katika mkoa huo.
“Mkoa
wa Tanga una fursa nyingi, hivyo ni jukumu letu kushirikiana na taasisi
nyingine kukuza wajasiriamali hawa na kutangaza uwekezaji katika jiji hili,”
alisisitiza.
Aliongeza
kuwa moja ya majukumu makubwa kwa sasa ni kuhakikisha wajasiriamali wadogo
wanakuwa katika kila kona ya nchi, ili kupunguza wimbi la utegemezi katika
jamii na kuhakikisha fursa za uwekezaji zinatangazwa ndani na nje ya nchi.
“TIC
ni taasisi za Serikali ambayo inatambua uwepo wa wajasiriamali wadogo na
tunatambua kuwa wanahitaji kukuza kibiashara na kwa kufanya hivi tunatimiza
azma ya Serikali katika kuwainua watu wetu,” aliongeza.
Aliishukuru
kampuni ya Tanga Fresh Ltd, kwa kusimamia
uratibu hadi kupatikana wajasiriamali 27 na kuwaingiza katika programu
hiyo ya mafunzo, yanayoendeshwa kwa ushirikiano baina ya TIC na Shirika la
Maendeleo la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Maendeleo na Biashara (UNCTAD).
Katibu
Tawala wa Wilaya ya Tanga, Marcelline Patrice, alisema TIC na Tanga Fresh Ltd
wamefungua milango ya mafanikio kwa wajasiriamali wa wilaya yake pamoja na
mikoa jirani iliyoshiriki katika mafunzo hayo.
“Muwe
makini katika kufanya biashara zenu, naamini sasa mtakua mmeiva kwa muda
mliokaa hapa,” aliwaambia washiriki hao.
Aliwataka
wajasiriamali hao kutokuwa waoga
kuchukua mikopo katika taasisi za fedha, kwani hiyo ndio njia ya kuwainua katika biashara zao.
“Wajasiriamali
wengi wamekua waoga kuingia katika taasisi za fedha…waende huko kukopa, ndio
mwanzo wa kukua kibiashara,” aliongeza.
Mmoja
kati ya wajasiriamali waliopewa mafunzo hayo,
Beatrice Chanika, alielezea mafunzo hayo kuwa ni mkombozi mkubwa katika
shughuli zao za ufugaji. “TIC waendelee kutusaidia ili tukue,” alisema
Beatrice.
No comments:
Post a Comment