Serikali
ya Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo (DRC), imesifu hatua ya Tanzania kufungua
ofisi ndogo ya mawasiliano ya Mamlaka ya Bandari (TPA), kwamba ni ya kizalendo
na inayothibitisha uhusiano mzuri uliopo baina ya nchi hizo.
Akizungumza
na waandishi wa habari hivi karibuni baada ya uzinduzi wa ofisi hiyo mjini
Lubumbashi, Waziri ya Uchukuzi wa Jimbo la Katanga, Kahozi Sumba, alisema
ufunguzi wa ofisi hiyo, utarahisisha na kuleta ufanisi katika kusafirisha
mizigo ya wafanyabiashara wa Kongo wanaotumia Bandari ya Dar es Salaam, na pia utasaidia kuboresha maisha yao.
"Kurahisisha
biashara ina maana ya kupata maendeleo na kuboresha maisha yetu, tunaishukuru
Serikali ya Tanzania kwa uamuzi huu," alisema baada uzinduzi huo, uliofanywa na
Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe.
Sumba
alisema Serikali ya nchi hiyo, inatarajia kuwa wafanyabiashara wa Kongo sasa
hawatakumbana tena na changamoto walizokuwa wanakabiliana nazo awali katika
biashara zao kati ya Kongo na Tanzania kupitia Bandari ya Dar es Salaam.
Alihimiza
Jumuiya ya Wafanyabiashara wa nchi hiyo, kuthibitisha kuwa kweli walikuwa
wanaihitaji ofisi hiyo kwa kuitumia kutatua matatizo yao.
"Thibitisheni
kwa vitendo kuwa kweli mlikuwa mnaihitaji ofisi hii," aliwaambia baadhi ya
wafanyabiashara waliokuwa katika uzinduzi huo.
Awali,
akizungumza kwa niaba ya Gavana wa Jimbo la Katanga, Moise Katumbi, Naibu
Gavana wa jimbo hilo, Yav Guilbert alimmwagia sifa Mwakyembe, akisema
amethibitisha kuwa ni mtu wa vitendo.
Katika
ziara yake Machi mwaka huu mjini Lubumbashi, Mwakyembe aliahidi kuwa ofisi hiyo
ingekuwa tayari mwishoni mwa Aprili, jambo ambalo limetekelezwa kwa wakati.
"Waziri
Mwakyembe si aina ya wanasiasa wanaotoa ahadi za uongo na ameonyesha kuwa
Tanzania inaweza kuileta Afrika pamoja na kupata maendeleo," alisema.
Awali,
Dk Mwakyembe alisema kuwa ofisi hiyo mpya itasaidia wafanyabiashara wa DRC,
kumaliza matatizo yao Lubumbashi badala ya kusafiri hadi Dar es Salaam.
"Wataweza
kufanya malipo ya bandari wakiwa Lubumbashi na kuepuka hatari ya kusafiri na
kiwango kikubwa cha fedha na kuibiwa," alisema Mwakyembe.
Alisema
tatizo lililokuwa linawakabili wafanyabiashara hao la kukabiliana na wakala wa
kupakia na kupakua mizigo wasio waaminifu, sasa litakuwa historia kwa kuwa
ofisi ya Lubumbashi itakuwa na orodha ya wakala, wanaokubalika na waaminifu.
Pia,
mienendo ya taarifa za mizigo, itafanyika mjini humo na hivyo kuharakisha
taratibu za mizigo bandarini hapo.
Waziri
Mwakyembe alisafiri kwa barabara kutoka Dar es Salaam hadi Lubumbashi kupitia
Zambia zaidi ya kilometa 2,000 ili
kupata taarifa za changamoto wanazokumbana nazo wafanyabiashara wa DRC, kuanzia
bandarini Dar es Salaam hadi njiani wanaposafiri.
No comments:
Post a Comment