SSRA YAHIMIZA UMUHIMU WA HIFADHI YA JAMII



Hifadhi ya Jamii ni haki ya kila mtu nchini katika kumhakikishia usalama wa upatikanaji wa masuala yote ya msingi pindi dharura zinapotokea.
Hayo yalisemwa na Mjumbe wa Menejimenti na Mkuu wa Ununuzi wa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii nchini (SSRA), Emmanuel Urembo wakati wa  semina ya juu ya shughuli na majukumu ya mamlaka hiyo, iliyofanyika mjini hapa juzi.
Urembo alisema haki hiyo imeainishwa vizuri katika Katiba ya nchi na kwenye Sera ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2003..
Alisema Taifa lina wajibu wa kuhakikisha kuwa kiwango cha chini cha maisha kwa kila mwananchi kinafikiwa, kwa kumpatia kila mtu mambo yote ya msingi ya kijamii bila kujali hali ya kipato, michango au ajira yake.
Aidha, alisema sheria iliyounda SSRA inaruhusu uandikishaji wa wanachama kutoka sekta isiyokuwa rasmi, mfano wakulima na wafanyabiashara ndogo, kuwa na haki ya kujiunga kwenye mfumo wa ziada.
Kwa mujibu wa Urembo, wananchi wapatao milioni moja na nusu walio kwenye sekta rasmi tu nchini, ndio wanaonufaika na Hifadhi ya Jamii, jambo ambalo ni changamoto kubwa kwa mamlaka hiyo.
Changamoto nyingine ni pamoja na mfumo uliopo hivi sasa kutoruhusu mwanachama mmoja kuhamia Mfuko mwingine, kuwepo kwa tofauti kubwa kwenye fomula za ukokotoaji wa mafao na tofauti ya mafao kuwa kubwa kati ya Mfuko mmoja na mwingine.

No comments: