SPIKA MAKINDA AMPASHA NYALANDU WIZARA ITAMSHINDA



Spika wa Bunge, Anne Makinda ameshauri Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu  kuwa kitu kimoja na watendaji wake vinginevyo, wizara itamshinda.  
Ushauri huo aliutoa baada ya Bunge kupitisha bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2014/15; bila upinzani mkubwa tofauti na ilivyozoeleka.   
Katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara ya Maliasili na Utalii iliidhinishiwa na Bunge Sh bilioni 83.1. Kati ya hizo, Sh bilioni  68.9 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh bilioni 14.1  kwa ajili ya miradi ya maendeleo.  
Makinda alisema tangu ameingia bungeni, wizara hiyo ni tete. “Tangu nimeingia bunge hili wizara hii ni tete. Mimi nilitegemea Nyalandu utafanya mabadiliko na nategemea utafanikiwa,” alisema.  
“Nendeni mkafanye  kazi kwa mujibu wa sheria na sisi tunategemea utalii ni sehemu yetu ambayo nchi inaweza kuishi vizuri zaidi bila kuleta vineno neno,” aliwaambia watendaji wa wizara hiyo wazidi kushirikiana kwani suala hilo ni la kitaifa si suala la mtu binafsi.  
Wakati wa kujadili bajeti ya wizara baadhi ya wabunge, ikiwemo Kambi Rasmi ya Upinzani, walieleza kusikitishwa kile walichosema ni mvutano baina ya Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo ya Maliasili na Utalii.  
“Hali hiyo inaonesha kuwa kuna mgongano aidha wa kimaslahi…Waziri na Katibu Mkuu wa wizara moja wanafanya kazi bila kushirikiana na kila mmoja akionekana kumvizia mwenzake hadharani, badala ya kukaa kwa pamoja kutekeleza maazimio ya Bunge,” alisema Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni wa wizara hiyo, Mchungaji Peter Msigwa. 

No comments: