Spika
wa Bunge, Anne Makinda ameshauri Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu
kuwa kitu kimoja na watendaji wake vinginevyo, wizara itamshinda.
Ushauri
huo aliutoa baada ya Bunge kupitisha bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha
2014/15; bila upinzani mkubwa tofauti na ilivyozoeleka.
Katika
mwaka wa fedha 2013/14, Wizara ya Maliasili na Utalii iliidhinishiwa na Bunge
Sh bilioni 83.1. Kati ya hizo, Sh bilioni 68.9 kwa ajili ya matumizi ya
kawaida na Sh bilioni 14.1 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Makinda
alisema tangu ameingia bungeni, wizara hiyo ni tete. “Tangu nimeingia bunge
hili wizara hii ni tete. Mimi nilitegemea Nyalandu utafanya mabadiliko na
nategemea utafanikiwa,” alisema.
“Nendeni
mkafanye kazi kwa mujibu wa sheria na sisi tunategemea utalii ni sehemu
yetu ambayo nchi inaweza kuishi vizuri zaidi bila kuleta vineno neno,”
aliwaambia watendaji wa wizara hiyo wazidi kushirikiana kwani suala hilo ni la
kitaifa si suala la mtu binafsi.
Wakati
wa kujadili bajeti ya wizara baadhi ya wabunge, ikiwemo Kambi Rasmi ya
Upinzani, walieleza kusikitishwa kile walichosema ni mvutano baina ya Waziri na
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo ya Maliasili na Utalii.
“Hali
hiyo inaonesha kuwa kuna mgongano aidha wa kimaslahi…Waziri na Katibu Mkuu wa
wizara moja wanafanya kazi bila kushirikiana na kila mmoja akionekana kumvizia
mwenzake hadharani, badala ya kukaa kwa pamoja kutekeleza maazimio ya Bunge,”
alisema Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni wa wizara hiyo, Mchungaji
Peter Msigwa.
No comments:
Post a Comment