Wizara
ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki imesema Tanzania haina tatizo na nchi yoyote
katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na ipo tayari kuingia katika
Shirikisho, lakini haitakurupuka katika maamuzi yoyote.
Hatua hiyo inatokana na kuwa ikiwa
jumuiya hiyo itavunjika tena, madhara kwa Tanzania ni makubwa kuliko nchi
nyingine yoyote, kwa kuzingatia madhara iliyopata ilipovunjika jumuiya ya
awali.
Waziri wa Wizara hiyo, Samuel Sitta
alisema hayo juzi jioni wakati akifanya majumuisho ya hotuba yake ya bajeti
pamoja na kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na wabunge.
Alisema uhusiano huo ulipovunjika
mwanzo, uliiacha Tanzania katika sintofahamu kwa sababu ofisi muhimu zilikuwa
nje.
Sitta alifafanua kuwa wakati jumuiya
hiyo ilipovunjika mwaka 1977, ofisi za Shirika la Posta na Simu zilikuwa Uganda
wakati za Bandari zilikuwa Kenya.
Alisema hatua za kiuangalifu,
zinazochukuliwa na Serikali ni nzuri na
kufanya kwa uangalifu ambayo mara nyingi Tanzania inaonekana iko sahihi kwa
misimamo hiyo.
Awali, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani
bungeni, Freeman Mbowe alihoji iwapo Serikali ina nia ya dhati ya kuingia
katika shirikisho hilo, kutokana na kuonekana ni kikwazo katika kuelekea hatua
mbalimbali.
Awali, akizungumzia kuhusu
mahusiano baina ya Rwanda na Tanzania alisema ni mazuri tu na
kwamba suala la uhasama baina ya nchi hizo linakuzwa na vyombo vya habari.
Akifafanua kuhusu mikutano
iliyozishirikisha nchi za Uganda, Rwanda na Kenya na kuitenga Tanzania na
Burundi, Sitta alisema hatua ile isiwatie wasiwasi Watanzania kwani hata mwaka
huu Tanzania, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC) watafanya
mkutano wao wa nchi za Afrika ya Kati.
Katika hatua nyingine, Waziri Sitta
alimshukuru Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) kwa kutoa ushauri mzuri wa
kimaandishi, kuhusu maandalizi ya sera ya mtangamano wa Afrika Mashariki na
kuahidi kuufanyika kazi.
Alieleza kuwa wizara inaendelea kutoa elimu kwa Watanzania, ambapo hadi sasa
wizara hiyo imefanikiwa kutoa elimu katika maeneo yote ya mipakani kuhusu
shirikisho hilo na inaendelea katika maeneo mengine.
Awali, Mbunge wa Longido, Michael
Laizer (CCM) alihoji wizara imejiandaaje
kutoa elimu kwa Watanzania hususan wa mipakani, kwa sababu wengi wao hawana
elimu kuhusu shirikisho hilo.
Aidha, Laizer alisema uzoefu unaonesha
kuwa raia wa Kenya, wameelimishwa ipasavyo ndiyo maana wamekuwa wakichangamkia
biashara hapa nchini na kwamba wanafanya bila bughudha yoyote, ukilinganisha na
Watanzania wanaoghasiwa kwa kiwango kikubwa wawapo nchini Kenya.
No comments:
Post a Comment