Jeshi la Polisi limewakamata watu 6,
wanaosadikiwa kuwa ni vinara wa vikundi hatari vya `Mbwa Mwitu’, `Watoto wa
Mbwa’ au `Panya Road’ .
Vikundi hivyo vinajihusisha na matukio
ya kihalifu jijini Dar es Salaam.
Vijana wanaounda makundi hayo, wengi
wakiwa wenye umri wa kati ya miaka 16 na 20, hutembea kwa makundi na kufanya
uhalifu kwa kutumia silaha, kama mapanga, visu, nondo na marungu.
Hayo yalisemwa na Kamanda wa Kanda
Maalum ya Dar es Salaam, Suleman Kova wakati akizungumza na waandishi wa habari
jana.
Alitaja waliokamatwa wakihusishwa na
vikundi hivyo kuwa ni Athuman Said (20), mkazi wa Kigogo, Joseph Ponela ambaye
ni dereva bodaboda, Clement Peter (25) fundi seremala, Roman Vitus (18) mfanyabiashara, Mwinshehe Adam
(37) mkazi wa Temeke na Daniel Peter (25) mkazi wa Yombo.
Alisema Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya
Dar es Salaam, limefanya msako katika maeneo mbalimbali ya Jiji ili kudhibiti
makundi ya uhalifu na vijana wahuni wasio na kazi.
Aliongeza kuwa maeneo ambayo
yameonekana kuwa na vijana hao ni Kigogo, Magomeni, Tabata, Manzese na Mbagala.
"Askari wa kutosha wa doria
wamepangwa kufanya doria ili kuthibiti milipuko yoyote ya vitendo vya kihuni
vinavyoleta hofu kwa wananchi," alisema Kova.
Aidha, alisema kumekuwa na mtindo wa watu
ambao hawafahamiki jijini hutuma ujumbe mfupi wa simu za mkononi, wakieneza
uvumi kwamba maeneo yao yamevamiwa na makundi ya Mbwa Mwitu au Panya Road.
Alisema uvumi huo, ulianza Mei 18 na 20
mwaka huu baada ya vibaka wawili wa kundi hilo, kuuawa na hofu ilikuja baada ya
mazishi ya vijana hao, kwani wangeweza kulipiza kisasi.
"Jeshi la Polisi linatoa onyo kali
mtindo huu ukome, kwani watu hao wanasababisha hofu kwa wananchi,"
aliongeza Kova.
Alisema Jeshi la Polisi limejiimarisha
kiulinzi na vijana hao, hawana uwezo wa kufanya watakavyo, kama uvumi
unavyoenezwa kimakosa.
Jeshi la Polisi limeamua kufanya msako
huo baada ya kundi la Panya Road, kuibuka wiki hii na kusababisha hofu kwa
wananchi wengi, ikiwa ni pamoja na kufanya uporaji na kujeruhi kwa kutumia
silaha za jadi, kama marungu, mapanga, visu na nondo katika maeneo mbalimbali
ya Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment