Serikali imesisisitiza
kuwa italipa madeni ya malimbikizo ya mishahara ya walimu kabla ya kumalizika kwa
mwaka huu wa fedha, 2013/14.
Naibu Waziri,
Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Kassim Majaliwa,
alieleza hayo bungeni juzi jioni wakati akichangia mjadala wa Wizara ya Elimu
na Mafunzo ya Ufundi.
Bunge
lilipitisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha
2014/15 ya Sh bilioni 799 zikiwamo Sh bilioni 344.2 za matumizi ya kawaida na
Sh bilioni 454.8 kwa ajili ya maendeleo.
Majaliwa alisema
madeni ya walimu yalielezwa kufikia Sh bilioni 61 na kwamba kumekuwa kukifanyika
uhakiki, na kwa baada ya uhakiki, Februari mwaka huu, walilipa Sh bilioni 19.
“Lakini pia
Machi na Aprili tayari kuna fedha nyingine zimelipwa, kwa bahati mbaya sikuja
na takwimu hapa, lakini Serikali itahakikisha kuwa madeni yote yanalipwa katika
mwaka huu wa fedha kabla haujamalizika,” alisema Majaliwa.
Aidha, alisema
fedha nyingine za malimbikizo yakiwamo ya likizo, matibabu, usafiri na masomo
zinalipwa kwa kupitia katika halmashauri husika.
Kuhusu ujenzi wa
nyumba za walimu, alisema tayari nyumba 1,200 zinajengwa ambapo kati yake 268
zimekamilika na zimetengwa Sh bilioni 200.
Kuhusu fedha za chenji za rada, Naibu Waziri alisema
hadi sasa zimeshanunulia madawati 93,988 ambayo yatagawanywa 600 kwa kila
halmashauri katika awamu ya kwanza na awamu ya pili madawati 400.
Akizungumzia walimu kuwa na waajiri tofauti, alisema mwajiriwa wa walimu ni Katibu Mkuu
Tamisemi, na katika ngazi ya mikoa wako chini ya Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) na
katika Halmashauri, kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya (DED).
Akichangia hoja hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia alisema
walimu wanaona unafuu zaidi tangu wawe chini ya Tamisemi, huku akiwataka
wabunge kuacha kupotosha dhana ya kuchangia maendeleo.
Naye Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru
Kawambwa, alitetea uamuzi wa kubadili madaraja ya ufaulu, akisema si kitu
kigeni duniani.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi
wa Umma, Celina Kombani, aliahidi kukutana na wadau ili kujadili kuundwa kwa
chombo kimoja cha kushughulikia masuala ya walimu.
No comments:
Post a Comment