Hadi
sasa mmiliki halali wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) ni Halmashauri ya
Jiji la Dar es Salaam na Serikali kupitia Msajili wa Hazina.
Naibu
Waziri wa Fedha, Adam Malima alisema hayo jana bungeni na kuongeza kuwa
Serikali iliondoa kesi mahakamani ya watuhumiwa wa UDA, ili kuruhusu uchunguzi
kufanyika upya.
Alikuwa
akijibu swali la Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), Mdee alitaka kauli ya
Serikali kuhusu utata wa utaratibu uliotumika katika uuzwaji wa hisa za
Serikali katika Shirika hilo.
Pia
alitaka kujua nani mmiliki halali wa hisa hizo kwa sasa pamoja na mgawanyo wa
hisa kwa wamiliki hao.
Malima
alisema hisa ndani ya Shirika la UDA hazijauzwa, mgawanyo wa hisa halali ni
kama ulivyosajiliwa kwa msajili wa makampuni, kwa maana ya Halmashauri ya Jiji
asilimia 51 na Serikali kupitia Msajili wa Hazina asilimia 49.
Naibu
Waziri alisema mwaka 2006 Serikali iliamua kuuza hisa zake kwa asilimia 49 ili
kupata mwekezaji mahiri mwenye uwezo wa kuliboresha shirika hilo.
Hata
hivyo alisema Tume ya Kurekebisha Mashirika ya Sekta ya Umma (PSRC)
ilishindwa kumpata mwekezaji aliyekidhi vigezo vilivyowekwa.
Januari
2010 kwa mujibu wa Malima, Bodi ya UDA iliiarifu Serikali kuwa amepatikana
mwekezaji ambaye ni Kampuni ya Simon Group ambayo ingeuziwa hisa za Serikali
pamoja na hisa 7,880,303 ambazo hazikugawiwa wakati UDA inaanzishwa.
Malima
alisema Serikali iliagiza Bodi kusitisha mpango wa kuizuia Simon Group Limited
hisa zozote kutokana na kukiukwa kwa taratibu na misingi ya Sheria.
Akiuliza
swali la nyongeza, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) alitaka kupata kauli
ya Serikali kuhusu kampuni hiyo kuendelea kumiliki na kuendesha Kampuni ya UDA
sasa.
Mbunge
huyo alisema Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) alishafanya
uchunguzi kuhusu uuzwaji wa hisa za UDA na kubaini kuwepo kwa ufisadi.
Alisema
ripoti hiyo iliwasilishwa kwa Waziri Mkuu Machi 30 mwaka 2011, ambapo ilibaini
ufisadi wa kutisha na kutaka Serikali itoe kauli baada ya kubaini ufisadi huo.
Aidha
Mnyika aligusia kitendo cha Mwendesha Mashitaka wa Serikali (DPP), kuwasilisha
hati mahakamani kutaka watuhumiwa wote wa UDA waachiwe kwa kuwa hawana kesi ya
kujibu.
Mnyika
alisema bila majibu watazidi kuamini kama Serikali ya CCM inawalinda vigogo
ambao ni mafisadi.
Akijibu
hoja ya Mnyika, Malima alikiri kuwepo kwa utata kwa mazingira ya uuzwaji wa UDA
kutoka pande zote mbili za umiliki yaani Serikali na Halmashauri ya Jiji.
Alisema
baada ya CAG kutoa ripoti yake ilielezea ukiukwaji wa taratibu na sheria
za uuzwaji, ndipo DPP aliamua kuondoa kesi mahakamani ili uchunguzi uendelee.
Malima
alisema sasa vyombo vya uchunguzi ikiwemo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa (TAKUKURU) vinaendelea na uchunguzi dhidi ya ufisadi uliobainishwa na
CAG.
No comments:
Post a Comment