Jumuiya ya Wazazi mkoani Kilimanjaro imefanya mabadiliko
ya Shule yake ya Sekondari Namfua wilayani Rombo na kuigeuza Chuo cha Ualimu.
Chuo hicho kitaitwa Chuo cha Ualimu cha
Mkoa wa Kilimanjaro na kinatarajia kupokea wanafunzi kuanzia Julai, mwaka huu.
Mbali na Sekondari ya Namfua, pia jumuiya hiyo imeifunga Shule ya Sekondari
Kahe wilayani Moshi, tayari kwa ajili
ya maandalizi ya kuanza kuwa Chuo cha
Kilimo. Hata hivyo, bado michakato haijaanza na sasa wanatafuta fedha.
Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo mkoani hapa, Festo Kilawe alisema tayari wanafunzi waliokuwa wakisoma
Namfua, wamehamishiwa shule nyingine za jumuiya mkoani humo kwa ajili ya
maandalizi ya kupokea wanafunzi wa Ualimu ili kukabili upungufu wa walimu
nchini.
Kilawe alisema shule hiyo iliyokuwa na
wanafunzi zaidi ya 150, wamehamishiwa katika Shule za Kibo wilayani Moshi
na Mwanga na Minja wilayani Mwanga.
Walimu wa shule hiyo, nao wamehamishiwa
katika shule hizo, walizokwenda wanafunzi hao.
"Jumuiya ina shule 11 mkoani hapa,
tumekaa tukakubaliana kwamba idadi ya shule za sekondari tulizonazo
ukichanganya na shule za kata ni nyingi mno...mfano Rombo pekee ina shule za
sekondari 48, tumeona upungufu uliopo sasa ni vyuo," alisema.
Kilawe alisema ukarabati wa Shule ya
Namfua iliyopo Kata ya Nanjararea Tarafa ya Tarakea ili kuwa Chuo cha Ualimu,
umegharimu zaidi ya Sh milioni 200, zilizotolewa na jumuiya hiyo ngazi ya
Taifa, ikiwamo Sh milioni 80 kutoka jumuiya hiyo mkoani Kilimanjaro.
Alisema wameteua Shule ya Namfua,
kutokana na kuwa na ekari 30 za ardhi ambazo zinatosha kwa ajili ya upanuzi wa
chuo hicho, ambacho kitakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 1,800 wa cheti cha
ualimu na diploma ya ualimu kwa mwaka.
Kuhusu Shule ya Kahe, Mwenyekiti huyo
alisema mipango ya kufungua Chuo cha Kilimo ipo katika hatua nzuri, kwani lengo
la jumuiya hiyo ngazi ya taifa ni kubadili mfumo wa elimu uliopo sasa,
ikiwezekana hata kufungua chuo kikuu cha jumuiya hiyo.
No comments:
Post a Comment