Serikali
imetangaza rasmi kuondoa utaratibu wa ruzuku kwa kutumia vocha za pembejeo.
Waziri
wa Kilimo Chakula na Ushirika, Mhandisi Christopher Chiza alisema hayo
jana katika hotuba ya makadirio ya matumizi ya fedha ya Wizara ya Kilimo
Chakula na Ushirika kwa mwaka 2014/2015.
Alisema
pamoja na mafanikio ya mpango wa ruzuku kumekuwepo na changamoto katika ngazi
mbalimbali ikiwemo ubadhirifu, upotevu wa vocha na ucheleweshaji wa vocha hali
inayopelekea wakulima kutopata pembejeo mapema.
“Serikali
imeondoa utaratibu wa ruzuku kwa kutumia vocha,” alisema Chiza kutokana
na changamoto hizo Serikali kuanzia msimu wa 2013/2014 ilibuni utaratibu wa
kutoa pembejeo za mbolea, mbegu za mahindi na mpunga kwa vikundi vya wakulima
na vyama vya ushirika kwa kutumia mikopo kupitia taasisi za fedha.
Hata
hivyo alisema utaratibu huo haukuweza kuendelea kutekelezwa kutokana na taasisi
za fedha kuweka sharti kwa serikali kuweka fedha taslimu kwa dhamana
kabla ya kutoa mikopo hiyo, jambo ambalo halikuwezekana.
Alisema
Serikali imekuwa ikitoa ruzuku za pembejeo za mbegu bora na mbolea kwa
wakulima kwa utaratibu wa vocha ambapo katika mwaka 2008/2009 kaya 737,000,
2009/2010 kaya milioni 1.5, 2010/2011 kaya milioni 2.01.
Pia
mwaka 2011/2012 kaya milioni 1.7 na 2012/2013 kaya 940,783 aidha
mwaka 2013/2014 Wizara ilitoa ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa kaya
932,100 ambazo zilitumia tani 124,685 za mbolea na tani 9621 za mbegu.
Alisema
uzalishaji wa mahindi uliongezeka kutoka magunia matano hadi kufikia magunia 15
kwa ekari na uzalishaji wa mpunga uliongezeka kutoka gunia nne hadi kufikia
gunia 20 kwa ekari.
Alisema
katika mwaka wa fedha 2014/2015 Serikali itaendelea kufanya mazungumzo na
taasisi za fedha zilizo tayari kutekeleza utaratibu huo ili changamoto
zilizojitokeza katika msimu uliopita zisijirudie tena.
Udhibiti
ubora wa mbolea
Juu
ya udhibiti wa ubora wa mbolea alisema, Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania
(TFRA) ilisajili jumla ya wafanyabiashara wa mbolea 533 na kuwapa leseni za
kufanya biashara hiyo.
Alisema
jumla ya tani 36.7 za mbolea zilikuwa chini ya kiwango na hatua za
kisheria zilichukuliwa dhidi ya kampuni zilizokutwa na mbolea hizo.
Pia
Waziri Chiza alisema kuanzia msimu wa 2013/2014 Hifadhi ya Taifa ya
Chakula (NFRA) ilikuwa na akiba ya nafaka tani 25,453 ambapo katika mwaka
2013/014 NFRA ilinunua tani 219,377 na kufanya jumla ya akiba ya nafaka kuwa
jumla ya tani 244,830.
Wazalishaji
wa sukari
Alisema
kumekuwa na malalamiko ya wazalishaji wa sukari nchini juu ya kushindwa kuuza
sukari katika soko la ndani kutokana na hisia kuwa kiasi kikubwa cha sukari
kimeingizwa nchini bila kuidhinishwa na Serikali.
Alisema
kutokana na hilo wizara na wadau wa sukari waliazimia kuundwa kwa kikosi kazi
kitakachotafiti na kutoa mapendekezo ya mfumo mzuri wa kuagiza sukari.
Waziri
Chiza alisema uzalishaji wa sukari katika viwanda vya Kilombero, Mtibwa, TPC na
Kagera ambapo hadi Machi 31, mwaka huu ulikuwa tani 293,011 sawa na asilimia
99.9 ya malengo.
Mbegu
za pamba
Alisema
changamoto kubwa iliyojitokeza katika msimu wa 2013/2014 ni tani 1,088 za mbegu
ya pamba isiyokuwa na manyoya inayotayarishwa na Kampuni ya Quton
zilizosambazwa kwa wakulima kutokuota.
Alisema
Wizara ilifanya tathmini ya mbegu yote iliyoharibika katika maeneo
yaliyoathirika na wakulima walipewa mbegu mbadala.
“Wizara
haitailipa Kampuni ya Quton Sh bilioni 1.7 ya ruzuku ya mbegu ambayo haikuota,”
alisema.
Kwa
upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji, Profesa Peter
Msolla alisema dhana ya kilimo kwanza haijatoa matunda ambayo yalitarajiwa.
“Kamati
imebaini pamoja na kuwepo kwa mikakati ya Kilimo Kwanza, utekelezaji wake hauko
dhahiri Kamati inashauri Serikali ifanye tathmini juu ya mafanikio na
changamoto katika utekelezaji wa azma hii,” alisema.
Alisema
pia Serikali itapima maeneo ili kupata matumizi bora ya ardhi kutokana na
migogoro mingi inayohusu matumizi ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji ,
wakulima na wawekezaji, wananchi na mamlaka za hifadhi za Taifa.
“Serikali
iweke juhudi za makusudi kupima maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya matumizi
bora ya ardhi, Serikali isisite kuchukua hatua kwa wawekezaji waliochukua
maeneo makubwa ya ardhi na hayaendelezwi mpaka sasa na kuwapa wananchi kwa
ajili ya kuendeleza sekta ya kilimo na ufugaji, ”alisema.
No comments:
Post a Comment